Hamia kwenye habari

JANUARI 22, 2024
ANGOLA

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Kichokwe

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Kichokwe

Januari 13, 2024, Ndugu Jeffrey Winder ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kichokwe. Tangazo hilo lilitolewa wakati wa programu ya pekee iliyofanywa kwenye ofisi ya tawi iliyo Luanda, nchini Angola. Ndugu na dada 187 walifika hapo ili kuhudhuria programu hiyo na wengine 353,427 waliunganishwa kupitia video mtandaoni. Idadi hiyo inatia ndani ndugu na dada 1,644 wanaozungumza Kichokwe. Wale waliohudhuria programu hiyo ana kwa ana walipewa nakala zilizochapishwa za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Nakala za kielektroni pia zilipatikana mtandaoni tayari kupakuliwa.

Inakadiriwa kwamba watu milioni tatu hivi wanazungumza Kichokwe nchini Angola, Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, na Zambia. Kwa sasa, ndugu na dada 462 wanatumikia katika makutaniko kumi ya Kichokwe nchini Angola. Ndugu wengine 734 wanatumikia katika makutaniko 21 ya Kichowe katika Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo.

Katika hotuba ya Ndugu Winder alitaja kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo imetumia jina la Mungu la kibinafsi mara 237. Ndugu mmoja alisema: “Waroma 10:13 inasema kwamba ‘kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.’ Lakini baadhi ya tafsiri za Biblia za Kichokwe hazifafanui waziwazi maana ya andiko hili. Basi, ninatazamia kwa hamu kutumia Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ili kuwasaidia watu waelewe uhusiano uliopo kati ya jina la Yehova na wokovu wetu. Ni zawadi nzuri iliyoje!”

Tuna uhakika kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya Kichokwe itawasaidia wengi zaidi kujifunza kumhusu Yehova na kumpenda kwa moyo na nguvu zote.​—Marko 12:33.