Hamia kwenye habari

Mahakama Kuu ya Kanada muda mfupi kabla ya kesi kusikilizwa Novemba 2, 2017.

AGOSTI 30, 2018
KANADA

Mahakama Kuu ya Kanada Yakataa Kuingilia Mpango wa Kutenga na Ushirika

Mahakama Kuu ya Kanada Yakataa Kuingilia Mpango wa Kutenga na Ushirika

Katika kesi ya Highwood Congregation of Jehovah’s Witnesses (Judicial Committee) v. Wall, Mahakama Kuu ya Kanada ilifikia uamuzi kwa kauli moja Mei 31, 2018, kwamba “vikundi vya kidini vina uhuru wa kuamua ni nani watakaokuwa washiriki na sheria watakazofuata,” hivyo kukubali kwamba mpango wa kutenga na ushirika haupaswi kuingiliwa na mahakama.

Jengo la Mahakama Kuu ya Kanada (picha upande wa kushoto) lililo Ottawa.

Mahakama iliamua kwamba mpango wa Mashahidi wa kuchunguza dhambi nzito “hauchochewi na uadui, bali umekusudiwa kumsaidia mshiriki aendelee kuwa sehemu ya Kutaniko,” na kwamba mahakama hazipaswi kuingilia mambo kama hayo ya kibinafsi na kidini.

Akitaja sababu za kutoa uamuzi huo, Hakimu wa Mahakama Kuu Malcolm alisema hivi kwa niaba ya mahakimu tisa waliohusika: “Utaratibu na sheria za kikundi fulani cha kidini zinaweza kuhusisha kufafanua fundisho la kidini, kama katika kisa hiki. Mahakama hazina haki au uwezo wa kushughulikia mambo yanayoleta utata kuhusiana na mafundisho ya kidini.”

Philip Brumley, wakili wa Mashahidi wa Yehova anasema hivi: “Uamuzi huu wa Mahakama Kuu ya Kanada unalingana na uamuzi wa mahakama kuu za Argentina, Brazili, Hungaria, Ireland, Italia, Peru, Poland, na Marekani uliotambua haki ya kisheria ya kufuata mifano katika Maandiko ya kuchunguza ni nani anayestahili kuwa Shahidi wa Yehova.”—1 Wakorintho 5:11; 2 Yohana 9-11.