Hamia kwenye habari

DESEMBA 30, 2013
KYRGYZSTAN

Mahakama ya Kyrgyzstan Yatoa Uamuzi wa Kuwatetea Wanaokataa Kujiunga na Jeshi kwa Sababu ya Dhamiri

Mahakama ya Kyrgyzstan Yatoa Uamuzi wa Kuwatetea Wanaokataa Kujiunga na Jeshi kwa Sababu ya Dhamiri

BISHKEK, Kyrgyzstan—Novemba 19, 2013, Baraza la Katiba la Mahakama Kuu ya Kyrgyzstan lilifikia uamuzi wa pamoja kwamba sheria ya nchi hiyo inayohusu utumishi wa badala haipatani na katiba na kwamba inakiuka haki ya kibinadamu ya uhuru wa kidini. Mahakama hiyo iliomba serikali ya Kyrgyzstan irekebishe sheria hiyo ili wale ambao hawawezi kufanya utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri wafanye utumishi mwingine wa kiraia usiohusisha kabisa mambo ya kijeshi.

Katika mwaka wa 2009, serikali ya Kyrgyzstan ilianzisha sheria iliyoruhusu utumishi wa badala. Hata hivyo, baadaye ilibainika wazi kwamba utumishi huo wa badala ulisimamiwa moja kwa moja na jeshi. Wale waliofanya utumishi huo walisimamiwa na wanajeshi, na hata wengine waliamriwa watoe pesa ili kuendeleza shughuli za kijeshi. Baada ya kumaliza kipindi cha utumishi huo, waliandikishwa moja kwa moja kuwa wanajeshi wa akiba. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova walikataa utumishi huo wa badala, jambo ambalo liliwaudhi wenye mamlaka hivi kwamba waliwafungulia mashtaka kadhaa ya uhalifu.

Uamuzi huo wa Novemba wa Baraza la Katiba la Mahakama Kuu ya Kyrgyzstan ulifunua wazi kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na sababu halali za kuukataa utumishi huo wa badala, na si kwamba walikuwa wakiepuka kutimiza wajibu wao wa kiraia. Isitoshe, Mahakama hiyo ilitambua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa tayari kufanya utumishi wa badala usiohusisha mambo ya kijeshi. Tunatarajia kwamba kesi zote dhidi ya Mashahidi wa Yehova zitachunguzwa upya na uamuzi utolewe kupatana na sheria mpya iliyofanyiwa marekebisho.

Khamit Iskakov, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Kyrgyzstan anasema hivi: “Mbali na kusuluhisha suala hili la kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri, uamuzi huu utawasaidia wenye mamlaka wa Kyrgyzstan waelewe kwamba Mashahidi wa Yehova ni dini inayoheshimika kimataifa.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000

Kyrgyzstan: Khamit Iskakov, simu +996 770 778 885