Hamia kwenye habari

Kushoto: Kundi la mapainia na wahitimu wa Gileadi katika miaka ya 1940. Juu kulia: Ndugu na dada wa kutaniko la kwanza katika kijiji cha Xylophagou. Chini kulia: Ndugu wakitangaza hotuba ya watu wote katika mwaka wa 19522

MACHI 29, 2022
SAIPRASI

1922-2022: Miaka 100 ya Kudumisha Uaminifu wa Kikristo Nchini Saiprasi

1922-2022: Miaka 100 ya Kudumisha Uaminifu wa Kikristo Nchini Saiprasi

Kufikia mwaka huu wa 2022 Mashahidi wa Yehova wametimiza miaka 100 tangu walipoanza kuhubiri katika kisiwa cha Mediterania cha Saiprasi. Mtume Paulo alitembelea kisiwa hicho katika safari yake ya kwanza ya umishonari akiwa pamoja na Barnaba ambaye alikuwa mwenyeji wa kisiwa hicho. Katika nyakati zetu, habari njema zilifika Saiprasi kwa mara ya kwanza katika mwaka wa 1922, kasisi mmoja alipopata kijitabu Does the Soul Die?

Miaka miwili baadaye, Cyrus Charalambous, Mwanafunzi wa Biblia aliyekuwa akiishi Marekani, alirudi Saiprasi. Alianza kuhubiri kwa bidii na akatuma trakti, Where Are the Dead? kwenye kila mji na kijiji katika Saiprasi.

Antonis Spetsiotes

Antonis Spetsiotes alipata trakti hiyo. Antonis alivutiwa sana na yale aliyoyasoma na akamweleza habari hizo jirani yake, Andreas Christou. Kisha, wanaume hao wawili wakaanza kuwaeleza wengine waliyojifunza.

Kanisa la Othodoksi la Ugiriki lilipinga sana jitihada zao za kuhubiri na hatimaye Antonis na Andreas walifukuzwa kanisani. Lakini hawakuacha kuhubiri kamwe. Baada ya mwaka wa 1930, kutaniko la kwanza kisiwani humo lilianzishwa katika kijiji cha Xylophagou, kwa sababu ya bidii yao katika kazi ya kuhubiri.

Mwaka wa 1947, kazi ya kuhubiri ilisonga kwa kasi baada ya Antonios Karandinos, mmishonari wa kwanza aliyehitimu Gileadi kutumwa Saiprasi kuwasili. Kufikia mwaka wa 1948, kulikuwa na wahubiri 50 waliokuwa wakihubiri kisiwani humo, na ofisi ya kwanza ya tawi ikaanzishwa. Mwaka wa 1960, akina ndugu waliandikisha shirika la kisheria. Miaka miwili baadaye, Jumba la Ufalme la kwanza lilijengwa huko Nicosia. Idadi ya Mashahidi iliendelea kuongezeka, na Betheli mpya iliyo kubwa zaidi ikawekwa wakfu mwaka wa 1969.

Kadiri wahubiri walivyoongezeka, upinzani uliongezeka pia. Mwaka wa 1965 hivi, akina ndugu vijana waliokataa kutumikia jeshini walifungwa gerezani. Wanajeshi waliwatesa baadhi ya vijana hao wakijaribu kuwafanya walegeze msimamo wao na kujiunga na jeshi.

Misaada inawasili huko Limassol

Akina ndugu na dada walikabili changamoto zaidi mwaka wa 1974 vita vilipozuka baada ya Uturuki kuvamia Saiprasi na kudhibiti eneo kubwa katika kisiwa hicho. Ndugu na dada 300 hivi wakawa wakimbizi. Familia ya Betheli ililazimika kuondoka katika ofisi ya tawi. Ndugu na dada kutoka mataifa mengine waliwasaidia akina ndugu wa Saiprasi kwa kuwatumia misaada. Akina ndugu ambao hali zao ziliwaruhusu waliwaandalia makazi waamini wenzao waliokuwa wamelazimika kuhama.

Kwa sababu ya vita ndugu na dada zetu hawangeweza kufanya mikutano pamoja. Licha ya hali hizo, waliendelea kuhubiri. Mwaka wa 2006, akina ndugu walifanya Kusanyiko la Wilaya lenye kichwa “Ukombozi Unakaribia,” huko Limassol. Mashahidi wote wa Yehova katika Saiprasi walifaulu kukusanyika pamoja kwa mara ya kwanza tangu 1974.

Kusanyiko la Wilaya 2006 la “Ukombozi Unakaribia,” huko Limasso

Sasa kuna wahubiri 2,866 wanaotumikia katika makutaniko 41 na vikundi 17, vinavyotumia lugha 14 za kisiwani humo. Mwaka wa 2021, watu 5,588 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Tunashangilia pamoja na ndugu na dada zetu kutoka Saiprasi. Tunajua kwamba kwa msaada wa Yehova wataendelea katika mwendo huohuo unaofaa.​—Wafilipi 3:16.