Hamia kwenye habari

Puneet Aggarwal, Delroy Williamson, Ashok Patel (safu ya juu, kuanzia kushoto hadi kulia); Mark Sleger, Jouni Palmu, Hiroshi Aoki (safu ya chini, kuanzia kushoto hadi kulia)

JULAI 10, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Biblia Sita Nyingine Zatolewa Katika Mwisho-Juma wa Pili Mfululizo

Biblia Sita Nyingine Zatolewa Katika Mwisho-Juma wa Pili Mfululizo

Kwa juma la pili mfululizo, Mashahidi wa Yehova wametangaza kutolewa kwa Biblia sita nyingine. Julai 4, 2020, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika Kibislama na Kioromo. Kisha siku iliyofuata, Julai 5, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika Kilatvia na Kimarathi, na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ikatolewa katika Kibengali na katika Kikaren (S’gaw). Biblia hizo zilitolewa katika mfumo wa kielektroni katika hotuba zilizokuwa zimerekodiwa mapema. Wahubiri waliunganishwa kielektroni kwenye programu hizo za pekee na walifurahi sana kupokea zawadi hizo za kiroho.

Kibislama

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa ilitolewa katika Kibislama na Ndugu Mark Sleger, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Fiji. Wahubiri walio Vanuatu waliunganishwa kwenye programu hiyo ambayo ilitolewa katika Kibislama na kutafsiriwa katika Lugha ya Ishara ya Kibislama.

Kazi ya kutafsiri Biblia hiyo ilichukua zaidi ya miaka mitatu na ilifanywa na vikundi viwili vya utafsiri. Mtafsiri mmoja alisema: “Ndugu zetu watafurahia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa kwa sababu ni rahisi kusoma na matamshi yameandikwa katika lugha ya kisasa, inayotumiwa na kila mtu. Itatusaidia sote kuelewa kweli vizuri zaidi.”

Tuna uhakika kwamba Biblia hii iliyorekebishwa itawasaidia wahubiri zaidi ya 700 wanaozungumza Kibislama katika funzo lao la kibinafsi na katika huduma.

Kioromo

Ndugu Delroy Williamson, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Ethiopia alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa katika Kioromo. Jumla ya ndugu na dada 12,548 waliunganishwa katika tukio hilo kupitia mtandao, kutia ndani wahubiri 2,000 wanaozungumza Kioromo.

Kwa sababu ya mapungufu ya kiufundi, Baraza Linaloongoza liliidhinisha programu iliyorekodiwa mapema irushwe kwenye kituo cha televisheni. Wahubiri wangeweza pia kusikiliza programu hiyo kupitia simu zao.

Watafsiri watano walitumia miaka mitano kuitafsiri Biblia hiyo. Toleo hilo litakuwa kifaa cha pekee kwa ndugu na dada zetu wanaotumikia katika eneo kubwa la lugha ya Oromo.

Kilatvia

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kilatvia imetolewa baada ya miaka 12 ya kazi ngumu. Makutaniko yote ya Kilatvia na ya Kirusi nchini Latvia yalialikwa kutazama programu hiyo.

Ndugu Jouni Palmu, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Finland alitoa hotuba ya kutolewa kwa Biblia hiyo. Alisema hivi: “Tunafurahi kuwatolea wasomaji wa lugha ya Latvia Biblia hii ambayo ni ya kisasa na iliyo rahisi kusoma. Tunatumaini kwamba, itaongeza shangwe ya kusoma na kutafakari Neno la Mungu.”

Mmoja wa watafsiri alisema hivi kuhusu sehemu za kufanyia utafiti zilizo katika Biblia hiyo mpya: “Tafsiri hii mpya ya Biblia ni kama ‘kifaa cha kielektroni’ cha kiroho, kinachopanua wigo wetu wa kuwa na funzo la kibinafsi lenye kina na kutafakari.”

Kimarathi

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kimarathi ilitolewa katika tukio ambalo liliandaliwa kwa ajili ya makutaniko yote ya lugha ya Marathi nchini India. Ndugu Puneet Aggarwal, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi nchini India, alitangaza kutolewa kwa Biblia hiyo.

Ili kukamilisha kazi ya kutafsiri Biblia hiyo, watafsiri sita walitumia miaka mitatu katika mradi huo. Mmoja wao alisema hivi: “Tafsiri hii itawasaidia sana wazazi na walimu wa Biblia wanapowafundisha watoto wao au wale wanaopendezwa na mafundisho ya kweli za Biblia.”

Mtafsiri mwingine alisema hivi: “Inaburudisha sana kujua kwamba Biblia hii inarudisha jina la Mungu, Yehova, katika sehemu zote lilipopatikana katika maandishi ya awali. Wasomaji wataweza kusoma jina la Yehova katika karibu kila ukurasa wa tafsiri hii, na jina la Yehova litapata utukufu linalostahili.”

Zaidi ya watu milioni 83 wanazungumza Kimarathi huko India ya kati.

Kibengali

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya Kibengali yalitolewa na Ndugu Ashok Patel, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya India. Zaidi ya wahubiri 1,200 nchini India na Bangladesh waliunganishwa kwenye programu hiyo.

Zaidi ya watu milioni 265 wanazungumza Kibengali, hivyo inaorodheshwa kuwa lugha ya saba inayozungumzwa zaidi duniani. Ili kutokeza tafsiri inayoweza kueleweka kwa urahisi na watu wengi, kikundi cha watafsiri kutoka sehemu tofauti-tofauti za India na Bangladesh walishirikiana kwa miaka mitatu ili kushughulikia mradi huo.

Katika hotuba yake, Ndugu Patel alisema hivi: “Kibengali kilikuwa kati ya lugha za kwanza za Kihindi kuwa na tafsiri ya Biblia. Tafsiri ya kwanza iliyokamilika ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa mwaka 1801. Jambo la pekee sana katika Biblia hiyo ni kwamba ilitumia kwa njia inayofaa jina la Mungu, Yehova. Hata hivyo, katika tafsiri za kisasa, jina la Mungu limebadilishwa na jina la cheo ‘Bwana.’ Kwa hiyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo itahakikisha kwamba watu wanapata tafsiri sahihi na inayoeleweka kwa urahisi.”

Mmoja wa watafsiri alisema hivi: “Tafsiri hii ni uthibitisho wa kwamba Yehova Mungu anawapenda watu wa namna mbalimbali na anawaalika wajifunze kumhusu yeye na mwana wake, Yesu Kristo.”

Karen (S’gaw)

Ndugu Hiroshi Aoki, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Myanmar alitangaza kutolewa kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kikaren (S’gaw). Jumla ya watu 510 kutoka makutaniko sita na vikundi vinne waliunganishwa kwenye programu hiyo.

Mradi wa kutafsiri lugha ya Karen (S’gaw) ulikamilishwa baada ya mwaka mmoja na miezi michache tu. Mmoja wa watafsiri hao alisema hivi: “Ndugu na dada pamoja na watu walio katika eneo letu watafurahia kusoma tafsiri hii ya Kikaren (S’gaw) kwa sababu inarudisha jina la Yehova mahali pake na inatumia lugha ya kisasa. Ni tafsiri ya wazi, ni sahihi, na ni rahisi kueleweka. Tunamshukuru Yehova kwa zawadi hii ya pekee itakayotusaidia kumkaribia kupitia lugha inayotugusa moyo zaidi.”

Mtafsiri mwingine alisema hivi: “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imeandikwa katika lugha ya kisasa, hivyo itawasaidia wasomaji kuelewa hisia za wahusika wa Biblia, kuwazia hali zao, na kuiga imani yao.”

Tunashangilia pamoja na ndugu na dada zetu ambao wamepokea Biblia hizo. Tuna uhakika kwamba matoleo haya ya Biblia yatawasaidia wahubiri wanaozungumza lugha hizo kuendelea kumkaribia Yehova zaidi na kuwafundisha wengine kweli.—Yohana 17:17.