Hamia kwenye habari

Zile Amri Kumi za Mungu Ni Nini?

Zile Amri Kumi za Mungu Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Zile Amri Kumi ni sheria ambazo Mungu alilipatia taifa la kale la Israeli. Sheria hizo zinajulikana pia kama yale Maneno Kumi, usemi ambao umetafsiriwa neno kwa neno kutokana na maneno ya Kiebrania ʽaseʹreth had·deva·rimʹ. Maneno hayo yanapatikana mara tatu katika Pentateuki (Torati), yaani, vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. (Kutoka 34:28; Kumbukumbu la Torati 4:​13; 10:4) Maneno yanayolingana na hayo katika Kigiriki, deʹka (kumi) loʹgous (maneno), yanatokeza neno “Dekalogi.”

 Mungu aliandika zile Amri Kumi kwenye mabamba mawili ya mawe na kumpa nabii wake Musa kwenye Mlima Sinai. (Kutoka 24:12-​18) Zile Amri Kumi zimeorodheshwa kwenye Kutoka 20:​1-​17 na Kumbukumbu la Torati 5:​6-​21.

 Orodha ya zile Amri Kumi

  1.   Mwabudu Yehova Mungu pekee.​—Kutoka 20:3.

  2.   Usiabudu sanamu.​—Kutoka 20:​4-6.

  3.   Usilitumie jina la Mungu kwa njia isiyofaa.​—Kutoka 20:7.

  4.   Ishike Sabato.​—Kutoka 20:​8-​11.

  5.   Waheshimu wazazi wako.​—Kutoka 20:12.

  6.   Usiue.​—Kutoka 20:13.

  7.   Usifanye uzinzi.​—Kutoka 20:14.

  8.   . Usiibe.​—Kutoka 20:15.

  9.   Usitoe ushahidi wa uwongo.​—Kutoka 20:16.

  10.   Usitamani chochote cha mwenzako.​—Kutoka 20:17.

 Kwa nini orodha ya zile Amri Kumi hutofautiana?

 Biblia haijaorodhesha kila amri kulingana na namba. Hivyo, maoni ya watu hutofautiana kuhusu jinsi amri hizo zinavyopaswa kupangwa. Orodha iliyoonyeshwa hapo juu ndio mpangilio wa kawaida wa sheria hizo. Hata hivyo, watu wengine huorodhesha zile Amri Kumi kwa njia tofauti. Tofauti hizo huonekana katika amri ya kwanza, ya pili, na ya mwisho. a

 Kusudi la zile Amri Kumi lilikuwa nini?

 Zile Amri Kumi zilikuwa sehemu ya Sheria ya Musa. Sheria hiyo ilitia ndani amri zaidi ya 600 na zilifanyiza sera ya makubaliano, au agano, kati ya Mungu na taifa la Israeli la kale. (Kutoka 34:27) Mungu aliwaahidi watu wa Israeli kwamba wangefanikiwa ikiwa wangetii Sheria ya Musa. (Kumbukumbu la Torati 28:​1-​14) Hata hivyo, kusudi kuu la Sheria lilikuwa kuwatayarisha Waisraeli kwa ajili ya Masihi aliyeahidiwa, au Kristo.​—Wagalatia 3:​24.

 Je, Wakristo wanapaswa kushika zile Amri Kumi?

 Hapana. Mungu alitoa Sheria yake, kutia ndani zile Amri Kumi, kwa taifa la Israeli la kale hasa. (Kumbukumbu la Torati 5:​2, 3; Zaburi 147:19, 20) Sheria ya Musa haitumiki kwa Wakristo, na hata Wakristo waliokuwa Wayahudi ‘waliwekwa huru kutoka katika Sheria.’ (Waroma 7:6) b Sheria ya Musa ilibadilishwa na “sheria ya Kristo,” inayotia ndani mambo yote ambayo Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye.​—Wagalatia 6:2; Mathayo 28:19, 20.

 Je, zile Amri Kumi zinatufaa leo?

 Ndiyo. Kwa sababu zile Amri Kumi zinafunua kufikiri kwa Mungu, tunaweza kunufaika kwa kujifunza amri hizo. (2 Timotheo 3:​16, 17) Zile Amri Kumi zinategemea kanuni zinazotegemeka ambazo hazitawahi kupitwa na wakati. (Zaburi 111:​7, 8) Kwa kweli, kanuni nyingi kati ya hizo ndizo msingi wa mafundisho ya ile inayoitwa kwa kawaida Agano Jipya.​—Ona “ Kanuni za zile Amri Kumi zinaonekana katika Agano Jipya.”

 Yesu alifundisha kwamba Sheria yote ya Musa, kutia ndani zile Amri Kumi, ilitegemea amri mbili za msingi. Alisema hivi: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri ya kwanza na iliyo kuu zaidi. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’ Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.” (Mathayo 22:34-​40) Kwa hiyo, ingawa Wakristo hawatazamiwi kushika Sheria ya Musa, wanaamriwa kumpenda Mungu na wanadamu wenzao.​—Yohana 13:34; 1 Yohana 4:​20, 21.

  Kanuni za zile Amri Kumi zinaonekana katika Agano Jipya

Kanuni

Andiko la Agano Jipya

Mwabudu Yehova Mungu pekee

Ufunuo 22:​8, 9

Usiabudu sanamu

1 Wakorintho 10:14

Liheshimu jina la Mungu

Mathayo 6:9

Mwabudu Mungu kwa ukawaida

Waebrania 10:24, 25

Waheshimu wazazi wako

Waefeso 6:​1, 2

Usiue

1 Yohana 3:​15

Usifanye uzinzi

Waebrania 13:4

Usiibe

Waefeso 4:​28

Usitoe ushahidi wa uwongo

Waefeso 4:​25

Usitamani chochote cha mwenzako

Luka 12:15

a Kulingana na mpangilio wa Kiyahudi “Kut[oka] 20:2 ndiyo ‘amri’ ya kwanza, na mstari wa 3-6 huonekana kuwa amri moja; ya pili.” (The Jewish Encyclopedia) Kwa upande mwingine, Wakatoliki huona Kutoka sura ya 20, mstari wa 1-6, kuwa amri moja. Hivyo, agizo la kuepuka kulivunjia jina la Mungu heshima huonekana kuwa amri ya pili. Ili kudumisha idadi ya amri hizo, wao hugawa agizo la mwisho dhidi ya kutamani mke wa jirani kuwa amri tofauti na kutamani mali za mwenzako.

b Waroma 7:7 inatumia amri ya kumi kama mfano wa “Sheria,” na hilo linathibitisha kwamba Sheria ya Musa ilitia ndani zile Amri Kumi.