Hamia kwenye habari

Je, Biblia Imebadilishwa au Kupotoshwa?

Je, Biblia Imebadilishwa au Kupotoshwa?

 Hapana. Inapolinganishwa na hati za kale inaonekana kwamba kwa ujumla Biblia haijabadilishwa licha ya kunakiliwa tangu zamani kwenye vifaa vinavyoharibika.

Je, hilo linamaanisha kwamba makosa hayakufanywa ilipokuwa ikinakiliwa?

 Maelfu ya hati za zamani za Biblia zimepatikana. Baadhi yake zina tofauti kadhaa, kuonyesha kwamba makosa yalifanywa ziliponakiliwa. Nyingi kati ya tofauti hizo ni ndogo sana na hazibadili maana ya habari. Hata hivyo, kuna tofauti chache muhimu ambazo zimegunduliwa. Baadhi yake zinaonekana kuwa jitihada za kimakusudi zilizofanywa zamani ili kubadili ujumbe wa Biblia. Fikiria mifano miwili:

  1.   Kwenye 1 Yohana 5:7, Biblia fulani za zamani zina maneno yafuatayo: “mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu: na watatu hawa ni umoja.” Hata hivyo, hati zinazotegemeka zinathibitisha kwamba maneno hayo hayakuwepo katika maandishi ya awali. Yaliongezwa baadaye. a Hivyo, tafsiri za Biblia za kisasa zinazoaminika hazina maneno hayo.

  2.   Jina la kibinafsi la Mungu linapatikana mara elfu nyingi katika hati za kale za Biblia. Hata hivyo, tafsiri nyingi za Biblia zimelibadili na kuandika majina ya cheo kama vile “Bwana” au “Mungu.”

Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba hakuna makosa mengine ambayo bado hayajapatikana?

 Kufikia sasa, hati nyingi sana zimegunduliwa hivi kwamba ni rahisi kuliko wakati mwingine wowote kutambua makosa. b Kulinganisha hati hizo kumeonyesha nini kuhusu usahihi wa Biblia leo?

  •   Msomi William H. Green, alisema hivi alipokuwa akizungumza kuhusu Maandiko ya Kiebrania (kwa kawaida yanajulikana kama “Agano la Kale”): “Yaweza kusemwa kwa uhakika kwamba hakuna kazi yoyote nyingine ya kale ambayo imepitishwa kwa usahihi hivyo.”

  •   Kuhusu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya,” msomi wa Biblia F. F. Bruce aliandika hivi: “Kila mara uthibitisho wa maandishi yetu ya Agano Jipya unakuwa mwingi zaidi kuliko uthibitisho wa maandishi ya waandikaji wengi wa zamani, na hakuna mtu anayeweza kujaribu kupinga maandishi hayo.”

  •   Bwana Frederic Kenyon, msomi anayeheshimika wa hati za Biblia, alisema kwamba mtu “anaweza kuchukua Biblia nzima mkononi mwake na kusema bila hofu au kusitasita kwamba anashika Neno la Mungu la kweli, lililopitishwa bila mabadiliko makubwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine katika muda wa karne nyingi.”

Kuna sababu gani za ziada za kuwa na uhakika kwamba Biblia imepitishwa kwa usahihi?

  •   Waandikaji Wayahudi na Wakristo walihifadhi masimulizi yanayoonyesha makosa mazito yaliyofanywa na watu wa Mungu. c (Hesabu 20:12; 2 Samweli 11:​2-4; Wagalatia 2:​11-​14) Vivyo hivyo, walihifadhi masimulizi yaliyoshutumu kutotii kwa taifa la Kiyahudi na yanayofichua mafundisho yaliyotungwa na wanadamu. (Hosea 4:2; Malaki 2:​8, 9; Mathayo 23:​8, 9; 1 Yohana 5:​21) Kwa kunakili masimulizi hayo kwa usahihi, waandikaji hao walionyesha kwamba wanategemeka na wanaheshimu sana Neno takatifu la Mungu.

  •   Je, haipatani na akili kwamba baada ya Mungu kutumia roho yake kuongoza Biblia iandikwe, angehakikisha pia inahifadhiwa kwa usahihi? d (Isaya 40:8; 1 Petro 1:​24, 25) Isitoshe, hakukusudia iwanufaishe watu walioishi katika nyakati za kale tu, bali pia itunufaishe sisi leo. (1 Wakorintho 10:11) Kwa kweli, “mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.”​—Waroma 15:4.

  •   Yesu na wafuasi wake walinukuu kutoka katika nakala za Maandiko ya Kiebrania bila kuhofu usahihi wa maandishi hayo ya kale.​—Luka 4:​16-​21; Matendo 17:​1-3.

a Maneno hayo hayapatikani katika Kodeksi ya Sinai, Kodeksi ya Aleksandria, Hati Na. 1209 ya Vatikani, Vulgate ya Kilatini ya awali, Tafsiri ya Kisiria ya Philoxenia-Harclea, au Peshitta ya Kisiria.

b Kwa mfano, zaidi ya hati 5,000 za Kigiriki za ile inayoitwa Agano Jipya, au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, zimepatikana.

c Biblia haisemi kwamba watumishi wa kibinadamu wa Mungu hawawezi kufanya makosa. Inasema hivi kihalisi: “Hakuna mwanadamu asiyetenda dhambi”​—1 Wafalme 8:46.

d Biblia inasema kwamba ingawa Mungu hakuwaambia waandikaji kila neno walilopaswa kuandika, aliongoza mawazo yao.​—2 Timotheo 3:​16, 17; 2 Petro 1:​21.