Hamia kwenye habari

Nambari 666 Inamaanisha Nini?

Nambari 666 Inamaanisha Nini?

Jibu la Biblia

 Kulingana na kitabu cha mwisho cha Biblia, 666 ndiyo nambari, au jina, la yule mnyama-mwitu aliye na vichwa saba na pembe kumi anayepanda kutoka katika bahari. (Ufunuo 13:​1, 17, 18) Mnyama-mwitu huyo anawakilisha mfumo wa kisiasa wa ulimwenguni pote, ambao unatawala juu ya “kila kabila na watu na lugha na taifa.” (Ufunuo 13:7) Jina 666 linaonyesha kwamba kwa maoni ya Mungu mfumo wa kisiasa umeshindwa kabisa. Linaonyeshaje hivyo?

  Si kibandiko tu. Kwa kawaida Mungu anapompa mtu au kitu jina linakuwa na maana fulani. Kwa mfano, jina Abramu linamaanisha “Baba Ametukuzwa (Amekwezwa).” Mungu alimpa mwanamume huyo jina Abrahamu linalomaanisha “Baba ya Umati (Halaiki),” wakati ambapo Mungu aliahidi kumfanya Abrahamu “kuwa baba ya umati wa mataifa.” (Mwanzo 17:5) Vivyo hivyo, Mungu alimpa huyo mnyama-mwitu jina 666 kuwa ishara ya sifa zinazomtambulisha.

  Nambari sita inaashiria kutokamilika. Mara nyingi, namba hutumiwa kama ishara katika Biblia. Nambari saba huwakilisha ukamili au ukamilifu. Kwa kuwa nambari sita imepungua kwa nambari moja kutoka saba, inaweza kumaanisha kitu ambacho si kamili au kilicho na kasoro machoni pa Mungu, na inaweza kuhusianishwa na maadui wa Mungu.​—1 Mambo ya Nyakati 20:6; Danieli 3:1.

  Mara tatu ili kutia mkazo. Nyakati nyingine Biblia hukazia jambo kwa kulitaja mara tatu. (Ufunuo 4:8; 8:​13) Kwa hiyo jina 666 linakazia kwa msisitizo kwamba Mungu huiona mifumo ya kisiasa inayoongozwa na wanadamu kuwa imeshindwa kabisa. Wanadamu wameshindwa kuleta amani na usalama wa kudumu​—mambo ambayo yanaweza kuletwa tu na Ufalme wa Mungu.

Alama ya yule mnyama-mwitu

 Biblia inasema kwamba watu hupata ile “alama ya yule mnyama-mwitu” kwa sababu wanamfuata “kwa mshangao,” kufikia hatua ya kumwabudu. (Ufunuo 13:3, 4; 16:2) Wanafanya hivyo kwa kutukuza nchi yao kutia ndani nembo zake na uwezo wa kijeshi, kufikia hatua ya kuabudu mambo hayo. Kitabu The Encyclopedia of Religion kinasema hivi: “Utaifa umekuwa dini kuu katika ulimwengu wa leo.” a

 Mtu anapewaje alama hiyo ya mnyama-mwitu juu ya mkono na paji la uso wake? (Ufunuo 13:16) Mungu alipolipatia taifa la Israeli amri, alisema hivi: ‘Myafunge kama ishara juu ya mkono wenu, nayo yatakuwa kama utepe wa kipaji katikati ya macho yenu.’ (Kumbukumbu la Torati 11:18) Hilo halikumaanisha kwamba Waisraeli walipaswa kutia alama juu ya mikono na vipaji vyao kihalisi, bali kwamba maneno ya Mungu yangeongoza matendo na mawazo yao. Vivyo hivyo, ingawa kihalisi nambari 666 haipaswi kuonwa kuwa kama chanjo au chale ambayo mtu amechorwa, kwa njia ya mfano wale ambao huruhusu mifumo ya kisiasa itawale maisha yao wanatambulishwa kwa alama hiyo ya huyo mnyama-mwitu. Wale walio na alama ya mnyama-mwitu wanampinga Mungu.​—Ufunuo 14:​9, 10; 19:19-​21.

a Ona pia Nationalism in a Global Era, ukurasa wa 134, na Nationalism and the Mind: Essays on Modern Culture, ukurasa wa 94.