Hamia kwenye habari

Mungu Alianza Lini Kuumba Ulimwengu?

Mungu Alianza Lini Kuumba Ulimwengu?

Jibu la Biblia

 Biblia haisemi Mungu alianza lini kuumba ulimwengu au ilichukua kipindi gani cha wakati. Inasema tu hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Biblia haitaji kihususa “mwanzo” ulianza lini. Hata hivyo, mfululizo wa matukio unaotajwa katika Mwanzo unaiweka kabla ya vipindi sita, au “siku,” za uumbaji.

 Je, siku sita za uumbaji ni siku halisi zenye urefu wa saa 24?

 Hapana. Katika Biblia, neno “siku” linaweza kumaanisha urefu mbalimbali wa kipindi cha wakati, ikitegemea muktadha. Kwa mfano, sehemu moja ya simulizi hilo linataja kipindi chote cha uumbaji kuwa siku moja.—Mwanzo 2:4.

 Ni nini kilichotokea katika siku sita za uumbaji?

 Mungu alibadilisha dunia ambayo ‘haikuwa na umbo na ilikuwa tupu’ kuwa sayari iliyo na viumbe hai watakaoishi. (Mwanzo 1:2) Kisha akaumba uhai duniani. Biblia inataja makundi sita ya matukio yaliyotukia katika siku, au vipindi, vya uumbaji:

  •  Siku ya 1: Mungu aliumba nuru iangaze uso wa dunia na kuwezesha kuwa vipindi vya usiku na mchana.—Mwanzo 1:3-5.

  •  Siku ya 2: Mungu aliumba anga, au alitenganisha maji yaliyo chini ya anga na maji yaliyo juu ya anga.—Mwanzo 1:6-8.

  •  Siku ya 3: Mungu alitokeza nchi kavu. Aliumba pia mimea.—Mwanzo 1:9-13.

  •  Siku ya 4: Mungu aliumba jua, mwezi, na nyota ili ziangaze dunia.—Mwanzo 1:14-19.

  •  Siku ya 5: Mungu aliumba viumbe wa kwenye maji na wanaoruka.—Mwanzo 1:20-23.

  •  Siku ya 6: Mungu aliumba wanyama na wanadamu.—Mwanzo 1:24-31.

 Mwishoni mwa siku ya sita, Mungu alipumzika kufanya kazi, au aliacha kuumba.—Mwanzo 2:1, 2.

 Je, Simulizi la Mwanzo ni sahihi kisayansi?

 Simulizi la Biblia linalozungumzia jinsi ulimwengu ulivyoumbwa halidai kuwa ni ufafanuzi wa kisayansi. Badala yake, linazungumzia uumbaji katika njia ambayo wasomaji hata nyakati za Biblia wangeweza kuelewa kirahisi mfuatano wa msingi wa matukio. Simulizi la uumbaji halipingani na sayansi. Mwanasayansi wa nyota Robert Jastrow aliandika hivi: “Taarifa hutofautiana lakini mambo ya msingi katika sayansi ya nyota na masimulizi ya Biblia ya kitabu cha Mwanzo ni yaleyale; mfululizo wa matukio mpaka kufikia kuumbwa kwa mwanadamu huanza mara moja, katika kipindi hususa cha wakati.”

 Jua, mwezi, na nyota ziliumbwa lini?

 Jua, mwezi, na nyota tayari zilikuwa zimeumbwa kama sehemu ya “mbingu” zilizoumbwa “mwanzoni.” (Mwanzo 1:1) Hata hivyo, inaonekana kwamba nuru yake haikuwa ikifika katika uso wa dunia kwa kuwa angahewa lilikuwa nzito sana. (Mwanzo 1:2) Hivyo, ingawa nuru ilionekana katika siku ya kwanza, chanzo chake hakikuwa kimeonekana. Katika siku ya nne, huenda angahewa likawa angavu zaidi. Biblia inasema kwamba jua, mwezi, na nyota zilianza ‘kuangazia dunia,’ bila shaka ikifafanua namna zilivyoonekana na mtu ambaye huenda angekuwa akitazama kutokea duniani.—Mwanzo 1:17.

 Kulingana na Biblia, dunia ina umri gani?

 Biblia haisemi chochote kuhusu umri wa dunia. Mwanzo 1:1 inasema tu kwamba ulimwengu, ambao unatia ndani dunia, ulikuwa na mwanzo. Maneno hayo hayapingani na kanuni za kisayansi au kadirio la umri wa dunia linalofanywa na wanasayansi.