Hamia kwenye habari

Ni Nani Wanaoenda Mbinguni?

Ni Nani Wanaoenda Mbinguni?

Jibu la Biblia

 Mungu anachagua idadi ndogo ya Wakristo waaminifu ambao, baada ya kufa, watafufuliwa wakaishi mbinguni. (1 Petro 1:3, 4) Baada ya kuchaguliwa wanapaswa kudumisha imani yao na mwenendo mzuri wa Kikristo ili wasipoteze pendeleo lao la kwenda mbinguni.​—Waefeso 5:5; Wafilipi 3:12-14.

Wanaoenda mbinguni watafanya kazi gani huko?

 Watakuwa wafalme na makuhani pamoja na Yesu kwa miaka 1,000. (Ufunuo 5:9, 10; 20:6) Watafanyiza “mbingu mpya,” au serikali ya mbinguni, itakayotawala juu ya “dunia mpya,” au jamii ya wanadamu watakaoishi duniani. Watawala hao watakaokuwa mbinguni watawasaidia wanadamu warudie hali yenye uadilifu ambayo Mungu alikusudia wawe nayo tangu mwanzoni.​—Isaya 65:17; 2 Petro 3:13.

Ni watu wangapi watakaofufuliwa waishi mbinguni?

 Biblia inaonyesha kwamba watu 144,000 watafufuliwa waishi mbinguni. (Ufunuo 7:4) Katika maono yaliyorekodiwa kwenye Ufunuo 14:1-3 mtume Yohana aliona “Mwana-Kondoo amesimama juu ya Mlima Sayuni, na pamoja naye 144,000.” Katika maono hayo, “Mwana-Kondoo” anawakilisha Yesu aliyefufuliwa. (Yohana 1:29; 1 Petro 1:19) “Mlima Sayuni” unawakilisha cheo cha juu cha Yesu na wale 144,000 watakaotawala naye mbinguni.​—Zaburi 2:6; Waebrania 12:22.

 Wale “walioitwa na waliochaguliwa” ili kutawala na Kristo katika Ufalme wanaitwa “kundi dogo.” (Ufunuo 17:14; Luka 12:32) Hilo linaonyesha kwamba watakuwa wachache kwa kulinganishwa na idadi kamili ya kondoo wa Yesu.​—Yohana 10:16.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu wale wanaoenda kuishi mbinguni

 Maoni yasiyo sahihi: Watu wote wema huenda mbinguni.

 Ukweli: Mungu anaahidi kwamba watu wengi wema wataishi milele duniani.​—Zaburi 37:11, 29, 34.

  •   Yesu alisema: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni.” (Yohana 3:13) Kwa kusema hivyo alionyesha kwamba watu wema waliokufa kabla ya yeye kuja duniani kama vile, Abrahamu, Musa, Ayubu, na Daudi, hawakwenda mbinguni. (Matendo 2:29, 34) Badala yake, walikuwa na tumaini la kufufuliwa waishi duniani.​—Ayubu 14:13-15.

  •   Ufufuo wa kimbingu unaitwa “ufufuo wa kwanza.” (Ufunuo 20:6) Hilo linaonyesha kwamba kutakuwa na ufufuo mwingine. Ufufuo huo utakuwa kwa ajili ya wale watakaoishi duniani.

  •   Biblia inafundisha kwamba Ufalme wa Mungu utakapotawala, “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Lazima ahadi hiyo iwe ni kwa ajili ya watu watakaoishi duniani, kwa kuwa hakujawahi kuwa na kifo mbinguni.

 Maoni yasiyo sahihi: Kila mtu anajichagulia ikiwa ataishi mbinguni au duniani.

 Ukweli: Mungu ndiye anayechagua ni Wakristo gani waaminifu watakaopata “tuzo la mwito . . . wa kwenda juu,” yaani, tumaini la kuishi mbinguni. (Wafilipi 3:14) Uchaguzi huo hautegemei mapendezi ya mtu.​—Mathayo 20:20-23.

 Maoni yasiyo sahihi: Tumaini la kuishi milele duniani ni duni, na linatolewa kwa wale ambao hawastahili kwenda mbinguni.

 Ukweli: Mungu anawaita wale watakaoishi milele duniani “watu wangu,” “watu wangu waliochaguliwa,” na “watu wa Yehova waliobarikiwa.” (Isaya 65:21-23) Watakuwa na pendeleo la kutimiza kusudi la Mungu la awali kwa wanadamu, yaani, kuishi milele wakiwa wakamilifu katika paradiso duniani.​—Mwanzo 1:28; Zaburi 115:16; Isaya 45:18.

 Maoni yasiyo sahihi: 144,000 inayotajwa katika Ufunuo ni idadi ya mfano, si halisi.

 Ukweli: Ingawa kitabu cha ufunuo kina namba za mfano, baadhi ya namba zinazotajwa ni halisi. Kwa mfano, kinasema kuhusu “majina kumi na mawili ya mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo.” (Ufunuo  21:14) Fikiria uthibitisho unaofanya tufikie mkataa kwamba 144,000 ni idadi halisi.

 Ufunuo 7:4 inasema kwamba “hesabu ya wale waliotiwa muhuri, [au waliothibitishwa kuwa wataishi mbinguni ni] 144,000.” Muktadha wa mstari huu unataja kikundi kingine tofauti: “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu.” Watu wanaofanyiza “umati mkubwa” watapata wokovu kutoka kwa Mungu. (Ufunuo 7:9, 10) Ikiwa namba 144,000 ingekuwa ya mfano, ikiwakilisha kikundi kisicho na idadi kamili, basi tofauti kati ya vikundi hivyo viwili haingekuwa wazi. a

 Isitoshe, wale 144,000 wanafafanuliwa kuwa “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza.” (Ufunuo 14:4) Maneno “matunda ya kwanza” yanarejelea wawakilishi wachache waliochaguliwa. Yanafafanua vizuri kuhusu wale watakaotawala mbinguni pamoja na Kristo juu ya idadi isiyojulikana ya watu watakaoishi duniani.​—Ufunuo 5:10.

a Vivyo hivyo Profesa Robert L. Thomas aliandika hivi kuhusu namba 144,000 inayotajwa katika Ufunuo 7:4: “Hiyo ni namba hususa tofauti na idadi isiyojulikana inayotajwa kwenye Ufunuo 7:9. Ikiwa namba [144,000] ni ya mfano basi hakuna namba katika kitabu hicho inayopaswa kuonwa kuwa halisi.”​—Revelation 1-7: An Exegetical Commentary, ukurasa wa 474.