Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yohana 14:27​—“Amani Nawaachieni”

Yohana 14:27​—“Amani Nawaachieni”

 “Ninawaachia amani; ninawapa amani yangu. Siwapi amani kwa njia ile ambayo ulimwengu huitoa. Mioyo yenu isitaabike wala kuogopa.”​—Yohana 14:27, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga.”​—Yohana 14:27, Union Version.

Maana ya Yohana 14:27

 Kwa upendo, Yesu aliwaambia mitume wake maneno hayo ili kuwahakikishia kwamba hakuwapaswa kuwa na wasiwasi kupita kiasi walipokabili matatizo. Kama yeye, wangefaulu kudumisha amani moyoni kwa msaada wa Mungu.

 Yesu aliwapa au kuwaachia mitume wake amani ya aina gani? Yesu aliwapa amani yake, yaani, amani ambayo yeye mwenyewe alikuwa nayo. Kuwa na amani hiyo hakumaanishi kwamba mtu hatakabili matatizo au dhiki. (Yohana 15:20; 16:33) Ingawa Yesu alitendewa isivyo haki na hatimaye akauawa, bado alikuwa na amani ya akilini na moyoni. (Luka 23:27, 28, 32-34; 1 Petro 2:23) Alikuwa na amani hiyo kwa sababu alijua kwamba Yehova, a Baba yake, alimpenda na alimkubali.​—Mathayo 3:16, 17.

 Yesu aliwapa mitume wake amani kwa kuwahakikishia kwamba walikuwa na kibali chake na cha Baba yake na kwamba waliwapenda. (Yohana 14:23; 15:9, 10; Waroma 5:1) Amani hiyo, ilitegemea imani yao kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, na ilituliza hofu yao na mambo yaliyowahangaisha. (Yohana 14:1) Ingawa Yesu hangeendelea kuwa nao kimwili, aliwaahidi kwamba roho takatifu ya Mungu ingewasaidia kuwa na uhakika na amani moyoni. (Yohana 14:25-27) Wafuasi wa Yesu wangeweza kukabili matatizo kwa uhodari, wakijua kwamba walikuwa na kibali cha Yehova na angewasaidia.​—Waebrania 13:6.

 Yesu alipokuwa duniani, kutakiana amani kulikuwa sehemu ya salamu za kawaida. (Mathayo 10:12) Hata hivyo, Yesu hakuwatakia tu mitume wake amani; aliwapa amani. Isitoshe, amani ambayo Yesu aliwapa ni tofauti na amani nyingine yoyote kutoka kwa ulimwengu b. Ulimwengu unaweza kuwapa watu kiasi fulani cha amani kupitia watu wa familia na marafiki, utajiri, umashuhuri, au cheo. Lakini amani kutoka kwa Yesu haitegemei hali zetu maishani. Ni amani ya moyoni inayodumu.

Muktadha wa Yohana 14:27

 Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu maneno hayo usiku kabla ya kifo chake. Usiku huo aliwaambia kwamba angewaacha hivi karibuni. (Yohana 13:33, 36) Mitume wake waliposikia hayo, walihuzunika sana. (Yohana 16:6) Basi Yesu aliwafariji, na akawaeleza kwamba hakukuwa na sababu yoyote ya kuwa na wasiwasi kuhusu jinsi hali ingekuwa baada ya yeye kuondoka.

 Leo pia, maneno hayo ya Yesu yanaweza kuwatia moyo Wakristo. Sisi pia tunaweza kuwa na amani. (2 Wathesalonike 3:16) Tunapokuwa wanafunzi wa Yesu, tunajifunza kwamba tuna kibali chake Yesu, na cha Yehova, Baba yake, na wanatupenda. (Wakolosai 3:15; 1 Yohana 4:16) Kwa sababu hiyo hatuhangaiki kupita kiasi. Kwa nini? Kwa sababu Mungu yuko upande wetu.​—Zaburi 118:6; Wafilipi 4:6, 7; 2 Petro 1:2.

 Tazama video hii fupi ili upate habari zaidi kuhusu kitabu cha Yohana.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?”

b Katika Biblia, neno “ulimwengu” linaweza kurejelea watu ambao hawana uhusiano na Mungu.