Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Zaburi 23:4​—“Nijapopita Kati ya Bonde la Uvuli wa Mauti”

Zaburi 23:4​—“Nijapopita Kati ya Bonde la Uvuli wa Mauti”

 “Hata nikitembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi madhara yoyote, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako hunipa uhakika.”—Zaburi 23:4, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe upo pamoja nami, gongo lako na fimbo yako vyanifariji.”​—Zaburi 23:4, Union Version.

Maana ya Zaburi 23:4 a

 Mungu huwalinda na kuwatunza wale wanaomwabudu hata ikiwa wanakabili hali ngumu kadiri gani. Mstari huo unatumia sitiari ya kondoo anayetunzwa na mchungaji ili kuonyesha jinsi Mungu anavyowalinda waabudu wake. b Hawahisi wakiwa peke yao wanapokabili hali ngumu sana zinazofafanuliwa katika mstari huu kuwa kivuli kizito au giza na zinazohatarisha uhai wao. Wanajihisi wakiwa salama kana kwamba Mungu yuko pamoja nao.

 Katika nyakati za Biblia, mchungaji angetumia fimbo au rungu kulinda kondoo dhidi ya wanyama wakali. Angetumia pia aina nyingine ya fimbo iliyokuwa ndefu na iliyopinda mwishoni ili kuwaongoza kondoo au kuwavuta kutoka katika hatari. Vivyo hivyo, Yehova Mungu ni kama Mchungaji mwenye upendo anayewalinda na kuwaongoza wote wanaomwabudu yeye. Hata wanapokabili hali ngumu zaidi maishani mwao, Yehova anaendelea kuwatunza kupitia njia mbalimbali.

  •   Anawafundisha na kuwafariji kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia.—Waroma 15:4.

  •   Anasikiliza sala zao, kisha anawapa amani ya akili na kutuliza hisia zao.—Wafilipi 4:6, 7.

  •   Anatumia waabudu wenzao kuwafariji.—Waebrania 10:24, 25.

  •   Anawapa tumaini hakika la wakati ujao utakaokuwa bora, atakapoondoa madhara yote ambayo kwa sasa wanakabili.—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3-5.

Muktadha wa Zaburi 23:4

 Zaburi ya 23 iliandikwa na Daudi, ambaye alipokuwa kijana alikuwa mchungaji na hatimaye alikuja kuwa mfalme wa taifa la kale la Israeli. (1 Samweli 17:34, 35; 2 Samweli 7:8) Zaburi hiyo inaanza kwa kumfafanua Yehova kuwa Mchungaji anayeongoza, anayelisha, na kuburudisha waabudu wake, sawa tu na mchungaji halisi anavyowatendea kondoo wake.—Zaburi 23:1-3.

 Daudi anapozungumzia ulinzi kutoka kwa Mungu katika Zaburi 23:4, anamrejelea Mungu kwa kutumia neno “wewe.” Kuzungumza na Yehova kwa njia hiyo, kunatuonyesha jinsi Daudi alivyokuwa na uhusiano wa karibu sana na Yehova. Daudi alijua kwamba Mungu anamjali na anafahamu majaribu yake binafsi. Kwa sababu hiyo, Daudi hakuogopa kwamba atapatwa na madhara yoyote.

 Katika mistari miwili inayofuata ya Zaburi 23, yaani mstari wa 5 na 6, sitiari inabadilika kutoka kwa mchungaji na kondoo wake na kuwa ya mwenyeji na mgeni wake. Kama mwenyeji mkarimu, Yehova anamtendea Daudi kama mgeni anayeheshimika. Hata adui za Daudi hawangeweza kumzuia Mungu asimtunze Daudi. Mwishoni mwa zaburi hiyo, Daudi anaonyesha jinsi anavyosadiki kwamba Mungu atamtendea kwa wema na upendo katika maisha yake yote.

 Mfano uliotumiwa katika Zaburi 23 unaonyesha jinsi Mungu anavyoendelea kuwatunza waabudu wake kwa upendo.—1 Petro 2:25.

a Katika tafsiri fulani za Biblia, Zaburi hiyo ni namba 22. Ingawa kuna jumla ya Zaburi 150, Biblia fulani hupanga zaburi zote kulingana na maandishi ya Kiebrania ya Wamasora, huku nyingine zikifuata mpangilio ulio katika Septuajinti ya Kigiriki, ambayo ni tafsiri ya maandishi ya Kiebrania iliyokamilishwa katika karne ya pili K.W.K.

b Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, mara nyingi hufafanuliwa katika Biblia kuwa Mchungaji mwenye wororo. Waabudu wake wanaofananishwa na kondoo, humtegemea kwa ajili ulinzi na msaada.—Zaburi 100:3; Isaya 40:10, 11; Yeremia 31:10; Ezekieli 34:11-16.