Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhai wa Mwanadamu Unaanza Wakati Gani?

Uhai wa Mwanadamu Unaanza Wakati Gani?

Uhai wa Mwanadamu Unaanza Wakati Gani?

“MAMA yangu alikuwa na umri wa miaka 17 na mimba ya miezi saba na nusu alipoamua kutoa mimba hiyo kwa kutumia maji ya chumvi,” anaeleza Gianna. * Akaongeza hivi: “Mimi ndiye mtu aliyetolewa katika mimba hiyo. Lakini niliendelea kuishi badala ya kufa.”

Maneno hayo yalisemwa mnamo 1996 na Gianna mwenye umri wa miaka 19 mbele ya halmashauri fulani ya serikali ya Marekani kuhusu utoaji-mimba. Kufikia wakati ambapo Gianna alikuwa ndani ya tumbo la uzazi la mama yake kwa miezi saba na nusu, alikuwa na viungo vyote vya mwili. Huenda ukakubali kwamba tayari alikuwa mtu, kwa kuwa aliendelea kuishi nje ya tumbo la uzazi.

Lakini vipi Gianna alipokuwa kiini-tete cha majuma matano tu, chenye urefu wa sentimita moja? Ni kweli kwamba viungo vya mwili wake havikuwa vimekua kabisa, lakini chembe za mfumo wake wa neva kutia ndani zile za ubongo wake, zilikuwa zimefanyizwa. Alikuwa na moyo unaopiga mara 80 kwa dakika ambao ulifanya damu ipite kwenye mishipa yake. Kwa hiyo, ikiwa Gianna alikuwa mtu baada ya kuishi miezi saba na nusu ndani ya tumbo la uzazi, je, haipatani na akili kukata kauli kwamba alikuwa mtu baada ya majuma matano—ingawa viungo vyake havikuwa vimekua kabisa?

Muujiza wa Kutunga Mimba

Sehemu zote za kiini-tete huanza kutengenezwa mara tu mimba inapotungwa, wakati mbegu ya uzazi ya kike inapotungishwa na mbegu ya uzazi ya kiume. Maendeleo katika tekinolojia yamewawezesha wanasayansi kuona mabadiliko ya ajabu yanayotukia ndani ya chembe ya mbegu ya uzazi iliyotungishwa. Molekuli zinazofanyiza DNA au chembe za urithi za baba na mama huungana na kutokeza uhai wa mwanadamu ambaye hakuwepo.

Chembe hiyo moja huanza kuchukua hatua za kufanyiza mwanadamu kamili. Maagizo ya mradi huo wa “ujenzi” hutolewa na chembe zetu za urithi ambazo ni sehemu ya mnyororo unaofanyiza DNA. Chembe hizo za urithi huamua mambo yote kutuhusu, kama vile, kimo chetu, sura yetu, rangi ya macho na nywele na mambo mengine mengi.

Baadaye, chembe hiyo moja inapogawanyika, maagizo hayohayo hupitishwa kwenye kila chembe mpya. Kwa kushangaza, kila chembe imepangiwa kuwa kiungo fulani. Viungo hivyo vinatia ndani moyo, ubongo, mifupa, ngozi, na hata chembe nyembamba za macho. Hatua ya kwanza ya kupanga jinsi chembe zitakavyokua na kutokeza mtu wa pekee imeitwa kwa kufaa “muujiza.”

“Tangu unapokuwa na chembe moja, mwili wa mwanadamu umepangiwa jinsi utakavyokua na kukomaa katika maisha yake yote,” anaripoti mwanabiolojia mashuhuri, Dakt. David Fu-Chi Mark. Alimalizia kwa kusema hivi: “Hatuwezi kamwe kushuku kwamba kila mwanadamu huwa wa pekee sana tangu uhai wake unapoanza mimba inapotungwa.”

Mwanadamu Ndani ya Tumbo la Uzazi

Tangu mimba inapotungwa katika tumbo la uzazi, mtoto si sehemu nyingine tu ya mwili wa mama, bali ni mwanadamu mwingine. Mwili wa mama unamwona kuwa kitu kigeni na ungemkataa mtoto huyo kama hangekuwa ndani ya tumbo la uzazi ambapo anapata ulinzi wa pekee. Uhai huo mpya wa mwanadamu ambao umetenganishwa na mama kwa kuzingirwa na tumbo la uzazi, ni mwanadamu aliye na chembe za pekee za urithi.

Wengine hubisha kwamba kwa sababu ya kasoro fulani mwili wa mwanamke huharibu mimba nyingi zilizotungwa, kwa hiyo kwa nini daktari asitoe mimba? Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kifo kisichotarajiwa na uuaji wa kukusudia. Katika nchi moja ya Amerika Kusini, watoto 71 kati ya 1,000 hufa katika mwaka wao wa kwanza. Lakini kwa kuwa watoto wengi hufa mapema, je, ni sawa kuwaua watoto walio chini ya umri wa mwaka mmoja? Jibu ni la!

Kwa kweli, Biblia inataja kuhusu uhai wa mwanadamu ukiwa katika tumbo la uzazi. Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi kumhusu Mungu: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.” (Zaburi 139:16) Daudi hasemi tu “kiini-tete fulani” bali anasema “kiini-tete CHANGU,” na hivyo kuonyesha kwa usahihi kwamba uhai wa Daudi ulianza mama yake alipotungwa mimba, muda mrefu kabla ya Daudi kuzaliwa. Akiongozwa na roho ya Mungu, Daudi alifunua pia kwamba mimba ilipotungwa viungo vyake vya mwili vilikua kulingana na mpango fulani au maagizo ‘yaliyoandikwa.’

Pia ona kwamba Biblia haisemi mwanamke hutungwa mkusanyo wa chembe zisizo na uhai. Badala yake, inasema: “Mwanamume amechukuliwa mimba!” (Ayubu 3:3) Hilo pia linaonyesha kwamba kulingana na Biblia, mtoto huwa mtu hai mimba inapotungwa. Naam, huo ndio wakati uhai wa mwanadamu unapoanza.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kutoa mimba kwa njia hii kunahusisha mama kudungwa sindano ya maji ya chumvi yenye sumu katika tumbo lake la uzazi, kisha mtoto anameza maji hayo ya chumvi na kufa katika muda wa saa mbili. Mama hujifungua baada ya saa 24 na kuzaa mtoto aliyekufa au—katika visa vichache—anayekaribia kufa.

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Kiini-tete cha majuma matano si mkusanyo wa chembe zisizo na uhai—ndani yake kuna chembe za kila kiungo cha mtu mzima

(ukubwa halisi)