Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | PAOLA CHIOZZI

Mtaalamu wa Biokemia Anatueleza kwa Nini Anaamini Kuna Mungu

Mtaalamu wa Biokemia Anatueleza kwa Nini Anaamini Kuna Mungu

Kwa zaidi ya miaka 20, Dakt. Paola Chiozzi amekuwa mwanabiolojia wa molekuli katika Chuo Kikuu cha Ferrara nchini Italia. Mwandishi wa Amkeni! alimwuliza kuhusu taaluma yake na imani yake.

Tueleze kuhusu malezi yako.

Baba yangu alikuwa fundi wa viatu, na mama yangu alikuwa mfanyakazi wa shambani. Lakini mimi nilitaka kuwa mwanasayansi. Nilivutiwa sana na maua maridadi, ndege, na wadudu waliokuwepo nyumbani kwetu. Nilihisi kwamba lazima vitu hivyo viwe vilitokezwa na mtu aliye na hekima inayozidi ile ya wanadamu.

Kwa hiyo tangu ulipokuwa mchanga uliamini kwamba kuna Muumba?

Hapana. Kwa kweli, nilianza kutilia shaka kama kuna Mungu nilipokuwa mtoto. Baba yangu alikufa ghafula kutokana na mshtuko wa moyo, na nikajiuliza, ‘Muumba wa vitu hivyo maridadi anawezaje kuwaacha watu wateseke na kufa?’

Je, masomo yako ya sayansi yalikusaidia kupata jibu?

Si mwanzoni. Nilipokuwa mwanabiolojia wa molekuli, nilianza kujifunza kuhusu kifo, yaani, kufa kwa chembe za mwili wetu kwa njia ya kawaida. Hilo ni tofauti na kufa kwa chembe zenye afya kunakotokeza uvimbe na kuoza kwa sehemu za mwili kwa sababu ya kukosa oksijeni au damu. Hadi miaka kadhaa iliyopita wanasayansi hawakuzingatia sana jambo hilo, hata ingawa ni muhimu sana kwa afya yetu.

Kwa nini ni muhimu kwa chembe za mwili kufa kwa njia ya kawaida?

Mwili wetu una trilioni nyingi sana za chembe ndogondogo. Chembe hizo zote lazima zife na nyingine mpya zitokezwe. Kila aina ya chembe ina muda wake wa kuishi; nyingine hufa baada ya majuma machache, nyingine baada ya miaka. Mfumo wa mwili wetu wa kubadili chembe unapaswa kudhibitiwa kabisa ili kudumisha usawaziko kamili unaohitajiwa kati ya kufa kwa chembe na kutokezwa kwa chembe nyingine.

 Ni matatizo gani yanayoweza kutokea?

Uchunguzi fulani unaonyesha kwamba chembe zinapokosa kufa kama zinavyopaswa, ugonjwa wa baridi-yabisi au wa kansa unaweza kutokea. Kwa upande mwingine, chembe zinapokufa kabla ya wakati unaofaa, ugonjwa wa Parkinson au wa Alzheimer unaweza kutokea. Utafiti wangu unahusiana na kutafuta njia za kutibu magonjwa hayo.

Uchunguzi wako kuhusu kufa kwa chembe ulikuathiri jinsi gani?

Kwa kweli, ulinichanganya. Ni wazi kwamba mfumo huo ulibuniwa na mtu anayetaka tuwe na afya nzuri. Kwa hiyo, niliendelea kujiuliza, Kwa nini watu wanateseka na kufa? Sikupata jibu.

Lakini ulikuwa na uhakika kwamba mfumo wa kufa kwa chembe ulibuniwa.

Ndiyo. Inashangaza sana jinsi mfumo huo wote ulivyo tata, lakini unaonekana ulibuniwa kwa hekima ya hali ya juu. Ninaamini kwamba hiyo ni hekima ya Mungu. Mimi hutumia darubini zenye nguvu sana ili kuchunguza mifumo mingi tata inayodhibiti kufa kwa chembe. Mifumo fulani inaweza kufanya chembe zianze kufa baada ya sekunde chache iwapo inahitajika. Chembe hujiangamiza zenyewe. Mfumo huo umebuniwa kwa ustadi sana hivi kwamba ni wenye kustaajabisha.

Kwa kuwa karibu chembe zetu zote hufa na nyingine kutokezwa upya kwa ukawaida, kuishi milele ni jambo linalowezekana

Ulikuwa na maswali kumhusu Mungu na kuteseka. Ulipataje majibu?

Mashahidi fulani wa Yehova walikuja nyumbani kwangu mnamo 1991, na nikawauliza kwa nini watu hufa. Walinionyesha jibu kutoka katika Biblia: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” (Waroma 5:12) Ikiwa mtu wa kwanza angemtii Mungu, angeishi milele. Mara moja nikatambua kwamba hilo lilipatana na kile nilichokuwa nimejifunza kutokana na uchunguzi wangu. Kwa kweli, nimejifunza kwamba Mungu hakukusudia watu wafe. Kwa kuwa karibu chembe zetu zote hufa na nyingine kutokezwa upya kwa ukawaida, kuishi milele ni jambo linalowezekana.

Ni nini kilichokusadikisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu?

Nilijifunza kile ambacho Biblia inasema kumhusu Mungu kwenye Zaburi 139:16: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.” Nikiwa mtaalamu wa biokemia, mimi hujifunza kuhusu habari zilizoandikwa katika chembe zetu za urithi. Mtunga-zaburi alijuaje kuhusu mambo hayo yaliyoandikwa humo? Kadiri nilivyojifunza mengi zaidi katika Biblia, ndivyo nilivyosadikishwa kwamba imeongozwa kwa roho ya Mungu.

Ulisaidiwa jinsi gani kuelewa kile ambacho Biblia inafundisha?

Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alijitolea kujifunza Biblia pamoja nami. Hatimaye, nilijifunza kwa nini Mungu ameruhusu watu wateseke. Pia nilijifunza kwamba kama vile Biblia inavyosema, Mungu anakusudia ‘kumeza kifo milele.’ (Isaya 25:8) Itakuwa rahisi kwa Muumba wetu kufanya mifumo ya ajabu ya miili yetu itende kikamilifu ili tuweze kufurahia maisha bila mwisho.

Umetumiaje ujuzi wa Biblia ambao umepata kuwasaidia wengine?

Nilikuwa Shahidi wa Yehova katika mwaka wa 1995, na tangu wakati huo nimejaribu kutumia nafasi zote kuwaeleza wengine mambo ninayojifunza katika Biblia. Kwa mfano, mfanyakazi mwenzangu alihuzunika sana ndugu yake alipojiua. Kanisa lake linawafundisha watu kwamba Mungu hawezi kuwasamehe watu wanaojiua. Lakini nilimwonyesha kwamba Biblia inatoa tumaini la ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Alifarijika sana kujifunza kwamba Muumba anatujali. Katika pindi kama hizo, mimi hujihisi kwamba kuwaeleza wengine kweli za Biblia kunanipa uradhi mwingi sana hata kuliko kuzungumza kuhusu sayansi!

Mtaalamu wa Biokemia Anatueleza kwa Nini Anaamini Kuna MunguMtaalamu wa Biokemia anatueleza kwa nini anaamini kuna Mungu