Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Ndoto Kutoka kwa Mungu

Ndoto Kutoka kwa Mungu

Je, Mungu ametumia ndoto kuwasiliana na wanadamu?

“[Nabii wa Mungu] Danieli aliona ndoto . . . kitandani mwake. Ndipo akaandika ndoto hiyo. Akasimulia masimulizi kamili ya mambo hayo.” —Danieli 7:1.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mungu ametumia njia mbalimbali kuwasiliana na wanadamu. Katika nyakati za Biblia, alitumia ndoto mara kwa mara. Hata hivyo, hazikuwa ndoto za kawaida zisizoeleweka na zisizo na maana. Ndoto kutoka kwa Mungu zilikuwa zenye kueleweka, vilevile zilikuwa na ujumbe hususa. Kwa mfano, katika ndoto fulani, nabii Danieli aliona wanyama ambao waliwakilisha milki za kisiasa kuanzia Babiloni hadi wakati wetu. (Danieli 7:1-3, 17) Kupitia ndoto, Mungu alimwambia Yosefu wa Nazareti, baba mlezi wa Yesu, akimbilie Misri pamoja na mkewe na mtoto. Hivyo, Yesu aliepuka kuuawa na Mfalme Herode mkatili. Herode alipokufa, Mungu alimjulisha Yosefu kupitia ndoto, na wakati huohuo akamwagiza arudi nyumbani na familia yake.—Mathayo 2:13-15, 19-23.

 Je, Mungu anatumia ndoto kuwasiliana nasi leo?

“Msipite mambo yaliyoandikwa.”—1 Wakorintho 4:6.

BIBLIA INASEMA NINI?

Ndoto zilizoandikwa kwenye Biblia ni ujumbe wa Mungu aliowafunulia wanadamu. Kuhusiana na ujumbe huo, andiko la 2 Timotheo 3:16, 17 linasema: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”

Biblia inatupa “uwezo kamili” kwa kuwa inatufunulia yote tunayohitaji kujua kumhusu Mungu, sifa zake, viwango vyake vya maadili, na jinsi tunavyohusika katika kusudi lake kwa ajili ya dunia. Hivyo, Mungu hatumii tena ndoto kuwasiliana na wanadamu. Ikiwa tunataka kujifunza kuhusu wakati ujao na mapenzi ya Mungu kwa ajili yetu, hatuhitaji ‘kupita mambo yaliyoandikwa’—yaani, katika Biblia. Isitoshe, karibu wanadamu wote wanaweza kukipata kitabu hicho na kujifunza mambo mengi ambayo Mungu amefunua, kutia ndani ndoto.

Kwa nini unaweza kuamini ndoto na maono yaliyoandikwa kwenye Biblia?

“Wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 Petro 1:21.

BIBLIA INASEMA NINI?

Maono na ndoto nyingi zilizoandikwa kwenye Biblia zilikuwa za kinabii—yaani, zilitabiri matukio ya wakati ujao. Kwa kuandika unabii huo, waandikaji wa Biblia waliwapa wasomaji nafasi ya kuchunguza ukweli wa Maandiko na pia unyoofu wa waandikaji hao. Je, mambo waliyoandika yalikuwa sahihi? Mfano mmoja ni maono yanayopatikana kwenye Danieli 8:1-7, yaliyoandikwa mwishoni mwa utawala wa Milki ya Babiloni.

Unabii huo ulihusisha kondoo-dume na mbuzi-dume ambaye alimpiga na kumwangusha kondoo-dume. Danieli hakuhitaji kukisia maana ya maono hayo. Malaika wa Mungu alisema: “Yule kondoo-dume uliyemwona mwenye pembe mbili anawakilisha wafalme wa Umedi na Uajemi. Na yule mbuzi-dume mwenye manyoya anawakilisha mfalme wa Ugiriki.” (Danieli 8:20, 21) Historia inathibitisha kwamba milki ya Umedi na Uajemi ilitawala baada ya milki ya Babiloni. Kisha, miaka mia mbili baadaye, Aleksanda Mkuu wa Ugiriki akashinda milki ya Umedi na Uajemi. Mfano huo unathibitisha kwamba unabii wa Biblia hutimizwa kwa usahihi kutia ndani ndoto za kinabii. Jambo hilo linafanya Biblia iwe tofauti na vitabu vingine vyote vitakatifu, na hivyo tunaweza kuiamini.

Pata majibu zaidi ya maswali ya Biblia kwenye www.mr1310.com/sw