Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Kucheza Kamari

Kucheza Kamari

Baadhi ya watu huona kwamba hakuna ubaya wowote kucheza kamari, lakini wengine huona kuwa zoea hatari.

Je, kuna ubaya wowote wa kucheza kamari?

WATU HUSEMA NINI?

Watu wengi huona kwamba kucheza kamari ni burudani isiyo na madhara ili mradi tu kufanya hivyo kunakubalika kisheria. Aina fulani ya michezo ya kamari inayokubaliwa kisheria kama vile michezo ya bahati nasibu inayofadhiliwa na serikali, imekuwa chanzo cha mapato kwa watu wengi.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia haisemi moja kwa moja kuhusu kucheza kamari. Hata hivyo, inatoa kanuni mbalimbali zinazoweza kutusaidia kujua maoni ya Mungu kuhusu kucheza kamari.

Kucheza kamari kunahusisha kushinda pesa za watu wengine, jambo linalopingana na onyo la Biblia linalosema, “mjilinde na kila namna ya tamaa.” (Luka 12:15) Pupa huchochea watu kucheza kamari. Taasisi za michezo hutangaza kuhusu mashindano makubwa ya bahati nasibu ijapokuwa hawapendi watu wajishindie pesa hizo, lakini wanafanya hivyo wakijua kwamba watu huchochewa na ndoto za kuwa matajiri na hivyo kutoa pesa nyingi katika majumba ya kucheza kamari. Kamari huchochea watu kuwa na tamaa ya kutaka kupata pesa haraka badala ya kuwasaidia kujilinda na pupa.

Kucheza kamari kunahusisha roho hii ya asili ya ubinafsi: kushinda pesa walizopoteza wengine. Hata hivyo Biblia inatia moyo mtu “aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Sheria moja kati ya zile Sheria Kumi inasema: “Usitamani . . . chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Mcheza-kamari anapoazimia kushinda pesa, kihalisi anatumaini kwamba wengine watapoteza pesa zao ili yeye afaidike.

Biblia inatoa onyo kuhusu wale wanaotegemea bahati kama chanzo kikuu cha mafanikio. Katika Israeli la kale, kulikuwa na watu waliokosa imani kumuelekea Mungu na kuanza “kuandaa meza kwa ajili ya mungu wa Bahati Njema.” Je, ujitoaji wao kuelekea “mungu wa Bahati Njema” ulikubaliwa na Mungu? Hapana, kwa kuwa aliwaambia hivi: “Nanyi mliendelea kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pangu, mlichagua jambo ambalo halikunipendeza.”—Isaya 65:11, 12.

Ni kweli kwamba katika nchi fulani, pesa zinapatikana katika michezo ya kamari iliyokubaliwa kisheria hutumika kulipia elimu, kuendeleza uchumi, na shughuli nyingine za kijamii. Lakini matumizi ya pesa hizo hayabadili njia ya upatikanaji wake, yaani, kupitia shughuli zinazochochea pupa na ubinafsi na zinazoendeleza wazo la kupata pesa kwa haraka.

“Usitamani . . . chochote cha mwenzako.”Kutoka 20:17.

Mcheza-kamari anawezaje kuathiriwa kwa kucheza kamari?

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inaonya kwamba “wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Watu hucheza kamari kwa sababu ya pupa, na “pupa” ni mbaya sana hivi kwamba Biblia inaitaja kuwa miongoni mwa tabia tunazopaswa kuepuka kabisa.—Waefeso 5:3.

Kwa kuwa hukazia hasa kutajirika haraka, uchezaji-kamari humchochea mtu kupenda pesa jambo linalotajwa na Biblia kuwa “chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” Tamaa ya pesa inaweza kwa urahisi kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwa mtu na kumfanya awe na mahangaiko mengi na kuharibu uhusiano wake na Mungu. Biblia inawataja kwa njia ya mfano wale walionaswa na upendo wa pesa kuwa “wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Pupa huwafanya watu wasiridhike na hali yao ya uchumi na hivyo kukosa furaha. “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhubiri 5:10.

Mamilioni ya watu walioshawishika kucheza kamari wamekuwa waraibu wa mchezo huo. Makadirio yanaonyesha kwamba tatizo hilo limeenea sana, huku kukiwa na mamilioni ya waraibu wa mchezo huo nchini Marekani pekee.

Methali moja inasema hivi: “Urithi hupatikana kwa pupa mwanzoni, lakini wakati wake ujao hautabarikiwa.” (Methali 20:21) Kucheza kamari kumefanya waraibu wa mchezo huo kuingia katika madeni au kufilisika, kupoteza kazi, marafiki na kuharibu ndoa. Kutumia kanuni za Biblia kunaweza kumsaidia mtu kuepuka madhara ya kucheza kamari na kumfanya awe na furaha maishani.

“Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.”1 Timotheo 6:9.