Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JE, NI KAZI YA UBUNI?

Uwezo wa Mwili wa Mwanadamu wa Kujiponya

Uwezo wa Mwili wa Mwanadamu wa Kujiponya

MIONGONI mwa mifumo inayomwezesha mwanadamu kuendeleza uhai ni uwezo wa mwili wa kuponya majeraha na kuzalisha upya tishu zilizoharibika. Jambo hilo huanza punde tu mwili unapopata jeraha.

Fikiria hili: Uwezo huo wa kujitibu hutegemea matukio yanayofuatana ya utendaji tata wa chembe:

  • Vigandisha damu hujishikiza kwenye tishu katika eneo la jeraha, kisha kufanya damu igande na kufunika mishipa ya damu iliyokuwa imejeruhiwa.

  • Eneo lililoathiriwa huvimba ili kuzuia maambukizo kupitia kidonda na kuondoa uchafu wowote uliosababishwa na jeraha.

  • Baada ya siku kadhaa, mwili huanza kuzalisha chembe mpya, hivyo kidonda kinafunga na mishipa kujirekebisha.

  • Hatimaye, tishu zinazotengeneza kovu huparekebisha na kupaimarisha mahali penye jeraha.

Uwezo wa damu kuganda umewachochea watafiti kutengeneza aina ya plastiki inayojirekebisha. Plastiki hizo zimefanyizwa na mirija midogo iliyo na kemikali mbili ambazo huvuja plastiki inapopasuka. Kemikali hizo zinapochanganyika, hutokeza umajimaji fulani ambao husambaa katika eneo lote lililoharibika na kufunika nyufa na mashimo. Umajimaji huo unapogandamana, eneo hilo huwa gumu na hivyo kurejesha hali ya awali ya plastiki hiyo. Mtafiti fulani anakiri kwamba mfumo huo wa kujirekebisha wa vitu visivyo hai unaoendelea kutengenezwa umebuniwa kwa kuiga uwezo wa kujirekebisha wa viumbe hai.

Una maoni gani? Je, uwezo wa mwili wa kujiponya ulijitokeza wenyewe? Au ulibuniwa?