Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahari inaweza kutia ndani wanyama

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini Waisraeli wa kale walilipa mahari?

NYAKATI za Biblia mahari ililipwa kwa familia ya bibi-harusi wakati wa mipango ya kufunga ndoa. Huenda mahari ilitia ndani vitu vyenye thamani, wanyama, au pesa. Nyakati nyingine ililipwa kwa kufanya kazi, kama ilivyokuwa katika kisa cha Yakobo, aliyekubali kumfanyia kazi baba ya Raheli kwa miaka saba ili aweze kumwoa Raheli. (Mwa. 29:17, 18, 20) Kusudi la desturi hiyo lilikuwa nini?

Msomi wa Biblia, Carol Meyers, anasema hivi: “Huenda mahari ilifidia familia ya bibi-harusi kwa kumpoteza binti aliyekuwa akisaidia kufanya kazi, jambo ambalo lilikuwa muhimu katika familia [za wakulima].” Huenda pia mahari ilisaidia kuimarisha kifungo cha urafiki kati ya familia hizo mbili ambazo sasa zilikuwa na uhusiano kwa sababu ya ndoa hiyo. Kifungo hicho cha familia kingeweza kuwa msaada mkubwa wakati wa hali ngumu. Isitoshe, mahari ilithibitisha kwamba mwanamke alikuwa amechumbiwa na kwamba hangekuwa tena chini ya utunzaji na ulinzi wa baba yake na badala yake angekuwa chini ya mume wake.

Kulipa mahari hakukumaanisha kwamba mke alikuwa bidhaa ambayo ingeweza kununuliwa au kuuzwa. Kitabu Ancient Israel​—Its Life and Institutions, kinasema hivi: “Kwa mtazamo wa kijuu-juu, kulipa kiasi fulani cha pesa, au kitu chenye thamani inayolingana na kiasi hicho cha pesa kwa familia ya bibi-harusi, kulifanya ndoa ya Waisraeli ionekane kama biashara. Lakini inaonekana kwamba [mahari] si malipo kwa ajili ya mwanamke huyo, badala yake ni fidia ambayo familia hupewa.”

Leo, katika baadhi ya nchi, watu wanaendelea kufuata desturi ya kulipa mahari. Wazazi Wakristo wanapoomba mahari, wanaacha ‘usawaziko wao ujulikane kwa watu wote’ kwa kutodai mahari inayopita kiasi. (Flp. 4:5; 1 Kor. 10:32, 33) Kwa kufanya hivyo, wanaonyesha kwamba wao si “wenye kupenda pesa,” au wenye pupa. (2 Tim. 3:2) Pia, wazazi Wakristo wasipodai mahari inayopita kiasi, mume mtarajiwa hatalazimika kuahirisha kufunga ndoa hadi atakapopata pesa za kutosha ili kulipa mahari hiyo. Au mume mtarajiwa hatahisi kwamba analazimika kuacha upainia na kufanya kazi ya muda wote ili apate pesa zinazohitajika ili kulipa kiasi kikubwa sana cha mahari.

Katika baadhi ya nchi, sheria zimewekwa kuhusu kiasi cha mahari kinachopaswa kutolewa. Katika hali hiyo, wazazi Wakristo wanapaswa kufuata sheria. Kwa nini? Neno la Mungu linawaagiza Wakristo ‘wajitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa’ na kutii sheria ambazo hazipingani na sheria za Mungu.​—Rom. 13:1; Mdo. 5:29.