Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Nzuri ya Kumwamini Mungu

Sababu Nzuri ya Kumwamini Mungu

Sababu Nzuri ya Kumwamini Mungu

KITABU cha Kikorea kinachoitwa 31 Reasons Why Young People Leave the Church kinasisitiza kwamba wengi wanaacha kwenda kanisani kwa sababu hawapati majibu yenye kuridhisha kwa maswali yao. Kwa mfano, wanauliza, ‘Kwa nini watu wanaomwamini Mungu wanateseka?’ na ‘Kwa nini ni lazima tuamini kila jambo linalofundishwa katika makanisa na huku mengi ya mafundisho hayo yanatatanisha na kupingana?’

Kwa sababu wamekatishwa tamaa na majibu wanayopewa na makasisi wao, wengi huamua kwamba hakuna jibu katika Biblia. Kasisi anapotoa maelezo yanayotegemea maoni yake tu, mara nyingi matokeo huwa kutomwelewa, hata kumkataa, Mungu na Biblia.

Hayo ndiyo yaliyompata Abel, aliyelelewa katika Kanisa la Kilutheri nchini Afrika Kusini. Anakumbuka hivi: “Kanisa hufundisha kwamba kila mtu anayekufa ‘huchukuliwa’ na Mungu. Lakini sikuelewa kwa nini Mungu mwenye upendo ‘angewachukua’ wazazi na kuwaacha watoto peke yao. Katika maeneo ya vijijini Afrika, nilikokulia, hatukumchinja kuku akiwa na vifaranga wachanga. Tukitambua kwamba ng’ombe alikuwa na mimba, hatukumchinja mpaka alipozaa na kumaliza kunyonyesha. Sikuweza kuelewa kwa nini Mungu mwenye upendo hakuwajali wanadamu kwa njia hiyohiyo.”

Aram, kutoka Kanada, alikuwa na shaka hizohizo. Yeye anasema, “baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miaka 13. Katika mazishi, kasisi mashuhuri alisema kwamba Mungu alitaka baba yangu afe ili amkaribie mbinguni. Alisema, ‘Mungu huwachukua watu wazuri kwa sababu anawapenda watu waadilifu.’ Sikuelewa kwa nini Mungu awe mchoyo kiasi hicho.”

Mwishowe, Abel na Aram walikutana na Mashahidi wa Yehova, wakajifunza Biblia nao, na wakapata majibu kwa maswali yao. Walisitawisha upendo kwa Mungu na wakawa na imani thabiti kwake. Kisha wakajiweka wakfu kwa Yehova na kuwa watumishi wake washikamanifu.

Ujuzi Sahihi Ni Muhimu Ili Kumwamini Mungu

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo hayo? Tunajifunza kwamba ili tumwamini Mungu, ni lazima tuwe na ujuzi sahihi. Mtume Paulo aliwaambia Wakristo katika jiji la kale la Filipi hivi: “Hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba upendo wenu uwe mwingi hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na utambuzi kamili.” (Wafilipi 1:9) Hapa, Paulo anasema kwamba upendo kwa Mungu na kwa waamini wenzetu unahusiana na ujuzi sahihi wa Mungu na kutambua mapenzi yake.

Jambo hilo linafaa, kwa kuwa takwa la kwanza la kumtumaini na kumtegemea mtu ni kumjua mtu huyo—tunapomjua kwa ukamili na kwa usahihi zaidi, ndivyo tunavyomtumaini zaidi. Vivyo hivyo, ujuzi sahihi unahitajiwa ili uchochewe kumwamini Mungu. Paulo alisema kwamba “imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Kumwamini Mungu bila ujuzi sahihi wa Biblia ni kama nyumba iliyojengwa kwa karata. Ukiipulizia kidogo tu, nyumba hiyo inaanguka.

Kujifunza Biblia kutakusaidia kupata majibu ya maswali kama lile lililowatatanisha Abel na Aram kwa muda mrefu, Kwa nini watu wanakufa? Biblia inaeleza kwamba “kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Wanadamu huzeeka na kufa kwa sababu Adamu alifanya dhambi, wala si kwa sababu Mungu huwachukua wawe pamoja naye. (Mwanzo 2:16, 17; 3:6, 17-19) Zaidi ya hayo, Biblia hufunua tumaini la kweli ambalo Yehova Mungu hutoa. Kupitia Mwana wake, Yesu Kristo, anatoa tumaini la ufufuo kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

Ili kutusaidia kuelewa ukweli kuhusu ufufuo, Biblia ina mifano mingi ya watu ambao Yesu aliwafufua. (Luka 7:11-17; 8:40-56; Yohana 11:17-45) Unaposoma habari hizo za Biblia, ona shangwe na furaha waliyokuwa nayo marafiki na familia za watu waliofufuliwa. Ona pia kwamba walichochewa kumtukuza Mungu na kumwamini Yesu.

Ujuzi sahihi kumhusu Mungu na makusudi yake unaweza kuwa na matokeo kama hayo kwa watu leo. Wengi walikuwa wametatanishwa, wamelemewa, na hata kukwazwa kwa sababu hawakuweza kupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali muhimu. Lakini walipoendelea kujifunza Biblia, walipata majibu, nayo yakabadili maisha yao kabisa.

Kumpenda Mungu—Sababu ya Kwanza Kabisa ya Kumtumikia

Ingawa ni lazima mtu awe na ujuzi sahihi ili amwamini Mungu, mengi zaidi yanahitajiwa ili achochewe kumtii na kumtumikia. Yesu alipoulizwa kuhusu amri kuu kutoka kwa Mungu, alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Mtu akimpenda Mungu jinsi Yesu alivyoonyesha, atakuwa tayari zaidi kumtii na kumtumikia Mungu. Je, ndivyo ilivyo kwako?

Rachel, ambaye ametumikia akiwa mishonari kwa miaka mingi huko Korea, anasema hivi kuhusu sababu yake ya kuwa na imani: “Ninaufikiria ukarimu wa Yehova kwa viumbe vyake, jinsi anavyowasamehe watu wake, na tamaa yake ya kutaka sisi tufaidike kwa kutupa nafasi ya kujua matakwa yake. Mambo hayo yote husitawisha upendo wangu kwa Mungu. Na upendo huo hunifanya nitake kumtumikia.”

Martha, mjane kutoka Ujerumani, amemtumikia Yehova kwa miaka 48. Yeye anasema: “Kwa nini namtumikia Yehova? Kwa sababu nampenda. Kila jioni mimi huzungumza na Yehova katika sala na kumwambia jinsi nilivyo na shukrani nyingi kwa ajili ya baraka zake, hasa kwa ajili ya dhabihu ya fidia.”

Naam, kumpenda Mungu hutufanya tutake kumtumikia kutoka moyoni. Lakini mtu huupataje upendo huo? Kichocheo chenye nguvu zaidi cha kumpenda Mungu ni kuthamini sana upendo ambao ametuonyesha. Ona kikumbusho chake katika Biblia kinachotuchangamsha moyo: “Yeye ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo. Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye. Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.”—1 Yohana 4:8-10.

Je, unatambua jinsi upendo huo ulivyo mkuu? Hebu wazia kwamba unazama mtoni na mtu ahatarishe maisha yake ili akuokoe. Je, utamsahau, au je, utamshukuru sana? Je, hutakuwa tayari kufanya chochote unachoweza kwa ajili yake? Upendo ambao Mungu alionyesha kwa kumtoa Mwana wake, Yesu Kristo, kuwa dhabihu ya fidia ni mkuu zaidi. (Yohana 3:16; Waroma 8:38, 39) Moyo wako unapoguswa na upendo wa Mungu, utachochewa kumpenda na kumtumikia kwa moyo wote.

Baraka za Sasa na za Wakati Ujao

Ingawa kumpenda Mungu kunapaswa kuwa sababu ya kwanza kabisa ya kufanya mapenzi yake, inachangamsha moyo kujua kwamba Mungu huwathawabisha wale wanaomtumikia. Mtume Paulo anasema: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

Mungu huwabariki kwelikweli wale wanaompenda na kumtii. Wengi huwa na afya bora kwa sababu ya kuzifuata kanuni za Biblia. (Methali 23:20, 21; 2 Wakorintho 7:1) Wale wanaofuata kanuni za Biblia kuhusu unyoofu na bidii kwa ujumla hutumainiwa na waajiri wao na hivyo huwa na usalama zaidi wa kiuchumi. (Wakolosai 3:23) Kwa kumtegemea Yehova, watumishi wa Mungu hupata baraka ya kuwa na amani ya akili hata wakiwa katika majaribu. (Methali 28:25; Wafilipi 4:6, 7) Zaidi ya hayo, wanatazamia wakiwa na uhakika kupata uzima wa milele wakati ujao katika Paradiso duniani.—Zaburi 37:11, 29.

Wale wanaopata baraka hizo kutoka kwa Yehova wana maoni gani kumhusu? Jacqueline, Mkristo huko Kanada, anaonyesha uthamini wake kwa Mungu: “Yeye sikuzote hutupa zawadi hizi nzuri ajabu, naye hutoa tumaini hakika la uzima wa milele.” Abel, aliyetangulia kutajwa, anaeleza hivi: “Tazamio la kuishi milele katika Paradiso duniani lilikuwa jambo jipya kwangu, nami nalitarajia kwa hamu. Hata hivyo, hata kama Paradiso haingekuwapo, bado ingekuwa furaha yangu kuonyesha kwamba nampenda Mungu kwa kumtumikia.”

Wewe Pia Unaweza Kuwa na Imani ya Kweli

Biblia inasema, “Yehova wa majeshi anahukumu kwa uadilifu; anachunguza figo na moyo.” (Yeremia 11:20) Naam, Yehova anachunguza kile kilicho ndani kabisa moyoni mwetu. Kila mtu anapaswa kujichunguza aone nia yake hasa ya kumtumikia Mungu. Imani na mawazo yenye makosa kumhusu Mungu huenda yalichangia matendo mabaya ambayo mtu alifanya zamani. Lakini ujuzi sahihi wa Biblia unaweza kuleta uhusiano mzuri pamoja na Muumba, Yehova Mungu.—1 Timotheo 2:3, 4.

Kupitia mpango wao wa funzo la Biblia la nyumbani bila malipo, Mashahidi wa Yehova wanawasaidia watu kupata ujuzi sahihi wa Mungu. (Mathayo 28:20) Wengi ambao wamekubali msaada huo, wamempenda Mungu na kusitawisha imani ya kweli kwake. Kupitia kujifunza Biblia, wamepata “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri,” ambao huwasaidia ‘kutembea kwa usalama’ katika siku hizi zenye hatari. (Methali 3:21-23) Zaidi ya yote, sasa wana tumaini “hakika na imara” kuhusu wakati ujao. (Waebrania 6:19) Wewe pia unaweza kuwa na imani ya kweli na kufurahia baraka hizo.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Maswali Magumu Yaliyohitaji Majibu

“Nilipokuwa nikizoezwa hospitalini nikiwa mwanafunzi wa udaktari, niliona watu wema wakiugua kwa maumivu kwa sababu ya magonjwa na misiba. Ikiwa kuna Mungu, kwa nini mambo hayo yanatendeka? Je, dini ni njia tu ya kupata amani ya akili?”—Aliyekuwa Mpresibiteri nchini Korea.

“Mara nyingi nilijiuliza ikiwa baba yangu, aliyekuwa mlevi, alienda motoni au mbinguni. Niliwaogopa sana wafu na moto wa mateso. Sikuelewa kwa nini Mungu mwenye upendo angeweza kumpeleka mtu ateseke milele motoni.”—Aliyekuwa Mkatoliki nchini Brazili.

“Kuna tazamio gani la wakati ujao kwa ajili ya dunia na wanadamu? Wanadamu watawezaje kuishi milele? Wanadamu watapataje amani ya kweli?”—Aliyekuwa Mkatoliki nchini Ujerumani.

“Sikuelewa fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine. Wanyama hawaabudu, kwa hiyo ikiwa unazaliwa upya katika umbo jingine ukiwa mnyama ili kulipia dhambi zako, utarekebishaje mambo na kufanya maendeleo ukiwa mnyama?”—Aliyekuwa Mhindu nchini Afrika Kusini.

“Nililelewa katika familia ya Wakonfyushasi, nami nilishiriki katika sherehe za kuwatuliza mababu Wetu waliokufa. Nilipokuwa nikishiriki katika kupanga meza ya dhabihu na kusujudu, nilijiuliza ikiwa hao mababu waliokufa walikuja kula chakula hicho na kuona tukiwasujudia.”—Aliyekuwa Mkonfyushasi nchini Korea.

Watu hao wote walipata majibu kwa maswali yao walipojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.