Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAZUNGUMZO PAMOJA NA JIRANI

Je, Mungu Anajali Tunapoteseka?

Je, Mungu Anajali Tunapoteseka?

Mazungumzo yafuatayo yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie Shahidi anayeitwa Michelle amemtembelea mwanamke anayeitwa Sophia nyumbani kwake.

KWA NINI ALIRUHUSU JAMBO HILO LITENDEKE?

Michelle: Leo ninawapa watu trakti hii katika eneo hili. Ina kichwa Je, Ungependa Kujua Ukweli? Na hii ni nakala yako.

Sophia: Inahusu dini?

Michelle: Ndiyo. Ona maswali sita yaliyo hapa. Ni lipi kati ya maswali haya—

Sophia: Achia hapo. Utapoteza muda wako kuzungumza nami.

Michelle: Kwa nini unasema hivyo?

Sophia: Ukweli ni kwamba, siamini kuna Mungu.

Michelle: Asante, ninathamini kwa kuniambia ukweli. Lakini hebu nikuulize, siku zote umehisi hivyo?

Sophia: Hapana, nilikuwa nikienda kanisani tangu utotoni. Lakini muda mrefu umepita tangu nilipoacha kwenda.

Michelle: Sawa. Hata hivyo, naomba nijitambulishe. Ninaitwa Michelle.

Sophia: Nami naitwa Sophia.

Michelle: Nafurahi kukutana nawe, Sophia.

Sophia: Nami pia.

Michelle: Sophia, sijakuja kukulazimisha ufuate imani yangu. Lakini ningependa kujua. Je, kuna jambo lolote lililofanya uamue kwamba hakuna Mungu?

Sophia: Ndiyo. Mama yangu alihusika katika aksidenti ya gari miaka 17 iliyopita.

Michelle: Pole sana kwa hilo. Je, aliumia?

Sophia: Ndiyo, na amepooza tangu wakati huo.

Michelle: Jambo hilo linahuzunisha. Lazima uwe umeumia sana.

Sophia: Ndiyo. Na hivyo basi najiuliza kama kuna Mungu kwa nini aliruhusu jambo hilo litendeke? Kwa nini anaruhusu tuteseke hivi?

JE, NI VIBAYA KUULIZA?

Michelle: Hisia na maswali yako yanaeleweka. Tunapoteseka, ni kawaida kujiuliza kwa nini tunateseka. Hata baadhi ya wanaume na wanawake waaminifu wa nyakati za Biblia walijiuliza hivyo!

Sophia: Kweli?

Michelle: Ndiyo. Je, ungependa nikuonyeshe mfano kwenye Biblia?

Sophia: Tafadhali nionyeshe.

Michelle: Ona kile ambacho nabii mwaminifu Habakuki alimuuliza Mungu kama inavyoonyesha katika Habakuki sura ya 1, mstari wa 2 na 3: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani, nawe usisikie? Nitakuomba msaada kutokana na jeuri mpaka wakati gani, nawe usiokoe? Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru?” Je, maswali hayo yanafanana na yale ambayo umekuwa ukijiuliza?

Sophia: Ndiyo yanafanana.

Michelle: Mungu hakumkemea Habakuki alipouliza maswali hayo wala hakumwambia awe na imani zaidi.

Sophia: Inashangaza!

YEHOVA ANACHUKIA KUTESEKA

Michelle: Biblia inafundisha kwamba Mungu anaona tunapoteseka na anajali.

Sophia: Unamaanisha nini?

 Michelle: Acha nikuonyeshe mfano mmoja kwenye andiko la Kutoka 3:7. Ungependa kusoma andiko hilo?

Sophia: Sawa. Linasema: “Naye Yehova akaongezea: ‘Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.’”

Michelle: Asante. Kulingana na andiko hilo, je, Mungu anaona watu wake wanapoteseka?

Sophia: Ndiyo, ni kama anaona.

Michelle: Na si kwamba anaona tu mambo yanayotokea. Tazama tena sehemu ya mwisho ya andiko hilo. Mungu alisema “Nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” Je, maneno hayo yanaonyesha Mungu asiyejali au aliyejitenga?

Sophia: Hapana, si hivyo.

Michelle: Bila shaka, kuna tofauti kati ya kuona jambo fulani na kutamani kulirekebisha.

Sophia: Ni kweli.

Michelle: Tukiwa na hilo akilini, acha tusome tukio lingine kuhusu watu wa Mungu walipokuwa wakiteseka. Limeandikwa katika kitabu cha Isaya 63:9. Sehemu ya kwanza ya andiko hilo inasema: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.” Hivyo basi, je, unaweza kusema Mungu alisumbuka kuona watu wake wakiteseka?

Sophia: Ndiyo, inaonekana alisumbuka.

Michelle: Sophia, ukweli ni kwamba Mungu anatujali sana, na anachukia kuona tukiteseka. Tunapoumia, anaumia pia.

KWA NINI AMESUBURI MUDA MREFU?

Michelle: Kabla ya kuzungumzia hilo, kuna jambo lingine ambalo ningependa tuzungumzie.

Sophia: Ni sawa.

Michelle: Fikiria kile ambacho Biblia hufundisha kuhusu nguvu za Mungu. Ningependa tusome andiko la Yeremia 10:12. Nakuomba ulisome.

Sophia: Sawa. Linasema: “Yeye ndiye Mtengenezaji wa dunia na nguvu zake, Yeye anayeifanya imara nchi yenye kuzaa kwa hekima yake, na Yeye aliyezitandaza mbingu kwa uelewaji wake.”

Michelle: Asante sana. Acha tuzungumzie kidogo andiko hilo. Je, Mungu alihitaji nguvu nyingi ili kuumba ulimwengu wote na kila kitu?

Sophia: Bila shaka.

Michelle: Sasa, ikiwa Mungu ana nguvu za kuumba kila kitu tunachoona, je, hawezi kuondoa matatizo tunayokabili?

Sophia: Anaweza.

Michelle: Fikiria tena kuhusu mama yako. Kwa nini unaumia kuona akiteseka?

Sophia: Kwa sababu ninampenda. Ni mama yangu.

Michelle: Na kama leo ungekuwa na uwezo wa kumponya, je, ungefanya hivyo?

Sophia: Bila shaka.

Michelle: Hilo linamaanisha nini? Biblia inafundisha kwamba Mungu anaona tunapoteseka, anatuhurumia, na ana nguvu nyingi. Hivyo basi, je, unaona jinsi ambavyo Mungu amejizuia sana kutochukua hatua ili kukomesha mateso?

Sophia: Sijawahi kufikiria hivyo.

Michelle: Je, unafikiri ana sababu nzuri ya kusubiri kabla hajakomesha matatizo yanayotupata? *

Sophia: Ninafikiri ana sababu.

Michelle: Nasikia simu yako ikilia, acha nije siku nyingine ili tuzungumzie jambo hili zaidi.

Sophia: Asante sana. Nitafurahia jambo hilo. *

Je, kuna jambo lolote kuhusu Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, utakapokutana tena na Shahidi wa Yehova usikose kumwuliza. Atafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

^ fu. 61 Kwa habari zaidi ona sura 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 64 Makala inayofuata katika mfululizo huu itazungumzia sababu inayofanya Mungu aruhusu kuteseka.