Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 26

Paradiso Yarudishwa!

Paradiso Yarudishwa!

Kupitia Ufalme wa Kristo, Yehova alitakasa jina Lake, atetea enzi Yake kuu, na kuondolea mbali uovu

KITABU cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, kinawapa wanadamu wote tumaini. Kitabu hicho kilichoandikwa na mtume Yohana, kina maono mbalimbali ambayo upeo wake ni kutimizwa kwa kusudi la Yehova.

Katika maono ya kwanza, Yesu aliyefufuliwa anapongeza na kurekebisha makutaniko kadhaa. Katika maono yanayofuata tunaona kiti cha Ufalme cha Mungu, ambapo viumbe wa roho wanamsifu.

Huku kusudi la Mungu likizidi kutimizwa, Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, apokea kitabu cha kukunjwa chenye mihuri saba. Anapofungua mihuri ya kwanza minne, wapanda-farasi wa mfano watokea. Mpanda-farasi wa kwanza ni Yesu akiwa juu ya farasi mweupe naye amevishwa taji la kifalme. Kisha wapanda-farasi juu ya farasi wenye rangi mbalimbali, wanaowakilisha vita, njaa, na tauni, mambo ambayo yanatendeka katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Muhuri wa saba unapofunguliwa, tarumbeta saba za mfano zinapulizwa zikiashiria kutangazwa kwa hukumu za Mungu. Kisha yafuata mapigo saba ya mfano, yanayowakilisha hasira ya Mungu.

Ufalme wa Mungu, unaofananishwa na mwana wa kiume aliyetoka kuzaliwa, wasimamishwa mbinguni. Vita vyatokea mbinguni, Shetani na malaika wake waovu watupwa duniani. Sauti kubwa inasema: “Ole wa dunia.” Ibilisi ana hasira kali, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.—Ufunuo 12:12.

Yohana amwona mwana-kondoo, Yesu, pamoja na wale 144,000 ambao wamechaguliwa kati ya wanadamu, ‘watakaotawala wakiwa wafalme pamoja’ na Yesu. Hivyo, kitabu cha Ufunuo kinafunua kwamba sehemu ya pili ya ule uzao inafanyizwa na jumla ya watu 144,000.—Ufunuo 14:1; 20:6.

Watawala wa dunia wanakusanyika pamoja kwa ajili ya Har–Magedoni, “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Wanapigana vita na yule anayeketi juu ya farasi mweupe—Yesu, anayeyaongoza majeshi ya mbinguni. Watawala wote wa ulimwengu huu wanaharibiwa. Shetani anafungwa, naye Yesu na wale 144,000 wanatawala juu ya dunia kwa “miaka elfu.” Mwishoni mwa ile miaka elfu, Shetani aharibiwa.—Ufunuo 16:14; 20:4.

Utawala huo wa Kristo na watawala wenzake utawatimizia nini wanadamu watiifu? Yohana anaandika: “[Yehova] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Kisha, dunia inakuwa paradiso!

Hivyo, kitabu cha Ufunuo kinakamilisha ujumbe wa Biblia. Ufalme wa Kimasihi, utalitakasa jina la Yehova na kuitetea enzi yake kuu milele!

—Inatoka kwenye Kitabu cha Ufunuo.