Hamia kwenye habari

Kusafiri Kwenye Mto Maroni

Kusafiri Kwenye Mto Maroni

Mbali kabisa na kelele za mjini, watu wa makabila, lugha, na mataifa mbalimbali huishi katika msitu wa mvua wa Amazon huko Amerika Kusini. Basi mnamo Julai 2017, kikundi cha Mashahidi 13 wa Yehova kilisafiri kwenye Mto Maroni na vijito vyake vya mashariki huko Guiana ya Ufaransa. Walikuwa na lengo gani? Kuwapelekea watu wanaoishi kando ya mto huo ujumbe wa tumaini ulio katika Biblia.

Kujitayarisha kwa Ajili ya Safari Hiyo

Mwezi mmoja kabla ya safari hiyo ya siku 12 kuanza, wahusika wote walikutana ili kufanya mipango. “Tulijifunza kuhusu eneo hilo na historia yake, na pia tulizungumzia jinsi ya kujiandaa kwa ajili ya safari hiyo,” anakumbuka Winsley. Kila mhusika alibeba chombo kisichoingiza maji ambamo aliweka kitanda cha kamba kinachoning’inia na neti ya kujikinga na mbu. Safari hiyo ilihusisha kusafiri kwa ndege mbili na mitumbwi ya magogo yaliyochongwa.

Claude na Lisette

Wale waliochaguliwa kushiriki walihisije kuhusu mwaliko huo? Claude na Lisette, ambao wamefikia umri wa kustaafu, walikubali mwaliko huo mara moja. Claude anasema hivi: “Nilifurahi sana, lakini niliogopa kidogo. Nilikuwa nimesikia kwamba mto huo una mikondo hatari.” Lisette pia alikuwa na wasiwasi. Anasema hivi: “Nilijiuliza ikiwa ningeweza kuzungumza lugha za Wenyeji wa Asili wa Amerika.”

Ndugu mwingine anayeitwa Mickaël alihisi hivyo pia. Anasema hivi, “Hatukujua mengi kuhusu kabila la Wayana, kwa hiyo, nilifanya utafiti kwenye Intaneti ili kujifunza maneno machache na jinsi ya kuwasalimu watu katika lugha yao.”

Shirley, ambaye alisafiri pamoja na Johann, mume wake, aliandika orodha ya lugha zinazozungumzwa na watu wanaoishi kando ya mto huo. Anasema, “Tulipakua video za lugha nyingi kati ya hizo kwenye jw.org na tukatafuta kitabu cha kujifunza maneno rahisi ya lugha ya Wayana.”

Kufika Kwenye Eneo la Wenyeji wa Asili wa Amerika

Jumanne, Julai 4, kikundi hicho kilipanda ndege huko Saint-Laurent du Maroni na kusafiri hadi Maripasoula, mji mdogo ulio sehemu ya ndani ya Guiana ya Ufaransa.

Kwa siku nne zilizofuata, kikundi hicho kiliwatembelea watu wanaoishi kwenye maeneo ya juu ya vijito vinavyoingia kwenye Mto Maroni, wakisafiri kwa mitumbwi yenye injini inayoitwa pirogue. Roland, ambaye alikuwa kwenye kikundi hicho anasema hivi: “Tulitambua kwamba Wenyeji wa Asili wa Amerika wanapenda sana kuzungumzia habari za Kimaandiko. Wana maswali mengi, na baadhi yao walitaka tujifunze Biblia pamoja nao.”

Katika kijiji kimoja, Johann na Shirley walikutana na wenzi wa ndoa ambao mtu wao wa ukoo alikuwa amejiua hivi karibuni. Johann anasema: “Tuliwaonyesha video yenye kichwa A Native American Finds His Creator,” kwenye JW Broadcasting. “Wenzi hao wa ndoa waliguswa moyo sana na video hiyo. Walitupatia anwani yao ya barua-pepe kwa sababu walitaka tuendelee kuwasiliana.”

Sehemu ya mbali zaidi ambayo kikundi hicho kilifika ni Antécume Pata. Chifu wa kijiji hicho aliwaruhusu Mashahidi hao waliochoka wafunge vitanda vyao vya kuning’inia kwenye eneo la umma kijijini. Vilevile walioga kwenye mto, kama wanakijiji wa eneo hilo wanavyofanya.

Baada ya hapo, kikundi hicho kilisafiri hadi kwenye kijiji cha Twenké, ambako waliwakuta wanakijiji wakiomboleza kifo cha mpendwa wao. Éric, mmoja kati ya wale waliopanga safari hiyo anasema hivi: “Chifu wa kabila hilo alituruhusu tutembee kwa uhuru kijijini ili kuwafariji wale waliokuwa wakiomboleza. Chifu huyo na familia yake walifurahi kusikia maandiko tuliyowasomea katika Biblia ya lugha ya Wayana. Vilevile tuliwaonyesha video kadhaa kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo.”

Kutembelea Grand-Santi na Apatou

Hatua iliyofuata ilikuwa safari ya saa moja na nusu kwa ndege kutoka Maripasoula hadi kwenye mji mdogo wa Grand-Santi. Jumanne na Jumatano, kikundi hicho kiliwahubiria watu wa eneo hilo ujumbe wa Biblia. Alhamisi, Mashahidi hao walifunga safari nyingine—walisafiri kwa saa tano na nusu kwenye Mto Maroni hadi kwenye kijiji cha Apatou.

Mto Maroni na msitu wa mvua wa Amazon kati ya Maripasoula na Grand-Santi

Siku mbili kabla ya mwisho wa safari yao, kikundi hicho kilitembelea vijiji vilivyo msituni vya jamii ya Maroon, ambao ni wazao wa watumwa Waafrika waliopelekwa Amerika Kusini wakati ambapo nchi jirani ya Suriname ilikuwa chini ya wakoloni. Mashahidi walialika watu wote kwenye mkutano uliofanywa msituni katika hema kubwa ambalo lilitengenezwa hasa kwa ajili ya tukio hilo. Claude anasema: “Mioyo yetu ilijaa shangwe idadi kubwa ya watu ilipohudhuria. Tulikuwa tumewakaribisha asubuhi hiyohiyo tu!” Karsten, ambaye alikuwa amesafiri kwa mara ya kwanza kwenye maeneo hayo ya mbali, alitoa hotuba ya watu wote katika lugha ya Aukan yenye kichwa “Je, Uhai Ndio uu Huu Tu?” Watu tisini na moja kutoka vijiji mbalimbali walihudhuria mkutano huo.

“Tuko Tayari Kurudi Huko Tena!”

Mwishowe, kikundi hicho kilirudi Saint-Laurent du Maroni. Wote walifurahi sana kuona jinsi wakaaji wa sehemu hiyo walivyoitikia vizuri, wakachukua machapisho mbalimbali, na kutazama video nyingi zilizotayarishwa na Mashahidi wa Yehova.

Lisette anasema, “Siwezi kueleza kikamili jinsi nilivyofurahia kwenda kwenye safari hii.” Cindy anahisi hivyo pia. Anasema: “Ikiwa kungekuwa na nafasi nyingine ya kurudi huko, ningetamani sana kurudi. Lazima uwe umefunga safari kama hii ili uelewe shangwe tunayohisi!”

Safari hiyo iliwachochea baadhi ya wale walioenda watamani kurudi tena. Mickaël anasema: “Tuko tayari kurudi huko tena!” Winsley amehamia Saint-Laurent du Maroni. Claude na Lisette, ambao wote wana umri unaozidi miaka 60 waliamua kuhamia Apatou.