Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Siku za Kuzaliwa?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Siku za Kuzaliwa?

 Mashahidi wa Yehova hawasherehekei siku za kuzaliwa kwa sababu tunaamini kwamba sherehe hizo hazimpendezi Mungu. Ingawa Biblia haikatazi moja kwa moja kusherehekea siku za kuzaliwa, inatusaidia kuchanganua mambo ya msingi ya sherehe hizo na kuelewa maoni ya Mungu kuhusiana nayo. Fikiria mambo manne kuhusu sherehe hizo na kanuni za Biblia zinazohusika.

  1.   Sherehe za siku ya kuzaliwa zina chanzo cha kipagani. Kulingana na kitabu Funk & Wagnalls Standard Dictionary of Folklore, Mythology, and Legend, sherehe hizo zilitokana na imani ya kwamba siku ambayo mtu alizaliwa inapofika, “roho waovu wana nafasi ya kumshambulia” na kwamba “kuwepo kwa marafiki na maneno yao ya kumtakia heri humlinda.” Kitabu The Lore of Birthdays kinasema kwamba katika nyakati za kale, rekodi za siku ya kuzaliwa zilikuwa “muhimu kwa ajili ya kupigwa kwa falaki” kwa kutegemea “elimu ya nyota isiyoeleweka kwa urahisi.” Kitabu hicho kinaongezea kwamba “kulingana na imani za kijamii, mishumaa ya siku za kuzaliwa ina nguvu zisizo za kawaida za kumtimizia mtu anachotaka.”

     Hata hivyo, Biblia inashutumu uchawi, uaguzi, kuwasiliana na pepo, au “chochote kama hicho.” (Kumbukumbu la Torati 18:14; Wagalatia 5:​19-​21) Sababu moja iliyomfanya Mungu ahukumu jiji la kale la Babiloni ni kwamba wakazi wake walijihusisha katika unajimu, ambao ni aina ya uaguzi. (Isaya 47:11-​15) Mashahidi wa Yehova hawachunguzi kupita kiasi vyanzo vya desturi zote; lakini Maandiko yanapotoa miongozo ya wazi, hatuyapuuzi.

  2.   Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku za kuzaliwa. Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema kwamba “waliona kusherehekea siku ya kuzaliwa ya mtu yeyote kuwa desturi ya kipagani.” Biblia inaonyesha kwamba mitume na wengine waliofundishwa moja kwa moja na Yesu waliweka mfano ambao Wakristo wote wanapaswa kufuata.​—2 Wathesalonike 3:6.

  3.   Tukio pekee ambalo Wakristo wanapaswa kukumbuka linahusiana, si na kuzaliwa, bali na kifo​—kile cha Yesu. (Luka 22:17-​20) Hilo halipaswi kutushangaza, kwa kuwa Biblia inasema kwamba “siku ya kufa [ni bora] kuliko siku ya kuzaliwa kwa mtu.” (Mhubiri 7:1) Kufikia mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alikuwa amejifanyia jina zuri na Mungu, na hilo lilifanya siku yake ya kufa kuwa muhimu zaidi kuliko siku yake ya kuzaliwa.​—Waebrania 1:4.

  4.   Biblia haijawahi kumtaja mtumishi wa Mungu aliyesherehekea siku yake ya kuzaliwa. Si eti jambo hilo lilisahaulika, kwa sababu Biblia inataja sherehe mbili za siku za kuzaliwa za watu ambao hawakuwa watumishi wa Mungu. Hata hivyo, matukio hayo mawili yanahusianishwa na matendo yasiyofaa.​—Mwanzo 40:20-​22; Marko 6:​21-​29.

Je, watoto ambao wazazi wao ni Mashahidi wanahisi kwamba wananyimwa kitu fulani kwa sababu ya kutosherehekea siku za kuzaliwa?

 Kama tu wazazi wanaojali, Mashahidi huwaonyesha watoto wao upendo mwaka mzima, kwa kuwapa zawadi na kuwa na vikusanyiko vyenye kufurahisha. Wanajaribu kufuata mfano mkamilifu wa Mungu, ambaye huwapa watoto wake vitu vizuri wakati wowote ule. (Mathayo 7:​11) Watoto walio na wazazi Mashahidi hawahisi kana kwamba wanakosa kitu chochote, kama maelezo yafutayo yanavyoonyesha:

  •   “Inafurahisha zaidi kupokea zawadi wakati usipoitazamia.”​—Tammy, umri wa miaka 12.

  •   “Hata ingawa sipati zawadi katika siku ya kuzaliwa kwangu, wazazi wangu bado huninunulia zawadi katika pindi nyinginezo. Napenda ikiwa hivyo kwa sababu napewa bila kutazamia.”​—Gregory, umri wa miaka 11.

  •   “Unafikiri eti dakika kumi, keki ndogo-ndogo chache, na wimbo mmoja hufanyiza karamu? Unapaswa uje nyumbani kwetu uone jinsi karamu halisi ilivyo!”​—Eric, umri wa miaka 6.