Hamia kwenye habari

Kuwasaidia Viziwi Katika “Zumaridi ya Ikweta”

Kuwasaidia Viziwi Katika “Zumaridi ya Ikweta”

Mamilioni ya watu ambao ni viziwi wanaishi nchini Indonesia, ambayo nyakati nyingine huitwa Zumaridi ya Ikweta. Ili kuwasaidia watu hao, Mashahidi wa Yehova hutokeza habari nyingi zinazotegemea Biblia pamoja na programu za elimu katika Lugha ya Ishara ya Indonesia. Jitihada hizo hazijakosa kutambuliwa.

Kusanyiko la Eneo la Lugha ya Ishara

Katika mwaka wa 2016, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko la eneo katika Lugha ya Ishara ya Indonesia, huko Medan, Sumatra Kaskazini. Ofisa wa ngazi za juu anayeshughulikia masuala ya usalama katika eneo hilo alihudhuria tukio hilo na kuwasifu Mashahidi kwa kuandaa programu hiyo ya elimu bila malipo. Mambo aliyoona yalimchochea sana hivi kwamba akajaribu kuiga ishara za wahudhuriaji walipokuwa wakiimba.

Msimamizi wa ukumbi ambamo kusanyiko hilo lilifanyiwa alisema kwamba “lilifanywa chini ya hali zenye usalama na kwa njia inayofaa. Ninatumaini kwamba Mashahidi wataendelea kupanga matukio kama hayo yanayowafaidi majirani wetu wasio na uwezo wa kusikia.” Aliongezea kusema kwamba mmiliki wa ukumbi huo aliposikia kwamba kusanyiko hilo lilikuwa kwa ajili ya viziwi, “alitaka kufanya jambo fulani zuri kwa ajili ya Mashahidi. Kwa hiyo, aliniagiza niwaandalie chakula cha mchana [wote 300] waliohudhuria.”

Kushukuru kwa Ajili ya Video za Lugha ya Ishara

Pia, Mashahidi wa Yehova huwatembelea viziwi ili kuzungumza nao kibinafsi kuhusu ujumbe wa Biblia. Mara nyingi Mashahidi hutumia video za Lugha ya Ishara ya Indonesia zilizokusudiwa kuwasaidia watu kufurahia maisha yenye kuridhisha na yenye kusudi.

Mahendra Teguh Priswanto, naibu msimamizi wa Shirika la Indonesia la Kuwatunza Viziwi katika jiji la Semarang, Java ya Kati alisema hivi: “Mnastahili kusifiwa kwa kazi mnayofanya ya kuwatunza viziwi na kushughulikia mahitaji yao. Kwa mfano, video Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha inasaidia sana. Tutathamini sana ikiwa kazi hii itaendelea kufanywa.”

“Wanawaonyesha Upendo”

Yanti, mwanamke ambaye ni kiziwi, ameguswa sana na jitihada za Mashahidi. Anaeleza hivi: “Mara nyingi watu huwadhihaki viziwi, lakini Mashahidi wanawaonyesha upendo. Mashahidi wengi walio na uwezo wa kusikia wamejifunza lugha ya ishara ili kuwasaidia viziwi wamfahamu Muumba na kuboresha maisha yao. Niliguswa sana na jitihada zao za unyoofu.”

Yanti alikuja kuwa Shahidi wa Yehova na sasa yeye ni mmoja wa watafsiri wanaotokeza video za Lugha ya Ishara ya Indonesia. Anasema hivi: “Habari tunazotokeza huwasaidia wale ambao hawajui sana lugha ya ishara kuboresha uwezo wao wa kutumia lugha hiyo. Lakini pia zinawafundisha watu jinsi ya kuwa na maisha yenye furaha na yenye kusudi.”