Ona video zinazopatikana

Biblia Inasema Nini Kuhusu Uhuru wa Kuchagua? Je, Mungu Anapanga Mbele ya Wakati Mambo Yatakayotupata?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Uhuru wa Kuchagua? Je, Mungu Anapanga Mbele ya Wakati Mambo Yatakayotupata?

Jibu la Biblia

 Mungu anatuheshimu kwa kututolea uhuru wa kuchagua, ni kusema, uwezo wa kuchukua maamuzi yetu kuliko tu kutupangia mambo yatakayotupata. Ona yale ambayo Biblia inafundisha.

  •   Mungu aliumba wanadamu kwa mufano wake. (Mwanzo 1:26) Tofauti na wanyama, wanaoongozwa na silika (instinct), sisi tuna uwezo wa kuonyesha sifa kama za Muumbaji wetu kama vile upendo na haki. Na kama Muumbaji wetu, sisi tuna uhuru wa kuchagua.

  •   Katika mambo mengi, tunaweza kuchukua maamuzi kuhusu wakati wetu ujao. Biblia inatutia moyo ‘tuchague uzima . . . kwa kusikiliza sauti ya [Mungu],’ ni kusema, kwa kuchagua kutii amri zake. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Maneno hayo hayangekuwa na maana yoyote, na yangekuwa ya unafiki, ikiwa hatungekuwa na uhuru wa kuchagua. Kuliko kutukaza tufanye mambo anayosema, Mungu anatuambia hivi kwa furaha: ‘Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama muto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.’—Isaya 48:18.

  •   Mungu hatupangie maisha mazuri ao mabaya. Ikiwa tunataka kufanikiwa, tunapaswa kujikaza. Biblia inatuambia hivi: ‘Yote ambayo mukono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.’ (Mhubiri 9:10) Pia inasema hivi: ‘Mipango ya mwenye bidii bila shaka inaleta faida.’—Methali 21:5.

 Uhuru wa kuchagua ni zawadi ya maana sana kutoka kwa Mungu, kwa kuwa inatusaidia tumupende “kwa moyo wote”—kwa sababu tunapenda kufanya hivyo.—Mathayo 22:37.

Je, Mungu ndiye anapanga mambo yote?

 Biblia inafundisha kwamba Mungu ni Mweza-Yote, kwamba hakuna mutu anayeweza kumuzuia kufanya jambo fulani. (Ayubu 37:23; Isaya 40:26) Lakini, hatumie nguvu zake kuhusiana na kila jambo. Kwa mufano, Biblia inasema kwamba ‘aliendelea kujizuia” kuhusiana na Babiloni, aliyekuwa adui wa watu wake. (Isaya 42:14) Vivyo hivyo, anaamua leo kuwavumilia wale wanaotumia vibaya uhuru wao ili kuwatesa wengine. Lakini, Mungu hatawavumilia milele.—Zaburi 37:10, 11.