Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ni Nani Alitia Sura na Mistari Katika Biblia?

Ni Nani Alitia Sura na Mistari Katika Biblia?

WAZIA kama uko Mukristo mwenye kuishi wakati wa mitume. Kutaniko lenu limetoka tu kupata barua ya mutume Paulo. Unasikiliza namna barua hiyo iko inasomwa, na unaona kama Paulo anataja mara nyingi “maandishi matakatifu,” ni kusema, Maandiko ya Kiebrania. (2 Timotheo 3:15) Unajiambia, ‘Ningependa kabisa kuona kwenye maandiko yenye anataja yanatoka.’ Lakini haingekuwa vyepesi kuona mahali hapo. Sababu gani?

BIBLIA HAIKUKUWA NA SURA NA MISTARI

Ona namna “maandishi matakatifu” yenye yalipatikana katika siku za Paulo yalikuwa. Maandishi fulani yanaonyeshwa hapa, ni kusema, sehemu fulani ya kitabu cha Isaya kutoka katika Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari Nyekundu. Unaona nini? Maandishi yote yako pamoja! Hakuna alama za vituo kama vile nukta, ao alama ya kuuliza. Na hakuna hata sura na mistari yenye tunatumia leo.

Waandikaji wa Biblia hawakugawanya ujumbe wao katika sura wala mistari. Waliandika tu ujumbe wote Mungu aliwapatia ili wasomaji waweze kuupata wote, kuliko kupata sehemu ndogo tu. Wewe pia unapendaka vile wakati unapata barua ya maana kutoka kwa mutu unapenda, haiko vile? Unasomaka barua yote, hapana sehemu ndogo tu.

Lakini, kukosekana kwa sura na mistari kulileta tatizo. Paulo alitambulisha tu maneno yenye alitaja kwa kusema maneno kama vile, “kama ilivyoandikwa” ao “kama Isaya alivyokuwa amesema.” (Waroma 3:10; 9:29) Na ingekuwa nguvu kupata maneno hayo kama mutu hakujua sana “maandishi matakatifu.”

Tena, “maandishi [hayo] matakatifu” hayakukuwa tu ujumbe mwepesi kutoka kwa Mungu. Kwenye mwisho wa wakati wa mitume, maandishi hayo matakatifu yalifikia kuwa vitabu vidogo-vidogo 66! Ndiyo sababu wasomaji wengi wa Biblia leo wanafurahi kuwa na sura na mistari yenye kuwasaidia kupata habari fulani, kama vile maneno mengi yenye Paulo alitaja katika barua zake.

Unaweza kujiuliza, ‘Sasa, ni nani alitia sura na mistari katika Biblia?’

NI NANI ALITIA SURA KATIKA BIBLIA?

Stephen Langton, padri Muingereza mwenye alifikia kuwa Askofu Mukubwa wa Canterbury, anasemwa kuwa yeye ndiye alitia sura mbalimbali katika Biblia. Alifanya vile mwanzoni mwa miaka kati ya 1201 na 1300 kisha kuzaliwa kwa Yesu, wakati alikuwa mwalimu kwenye Masomo ya Juu ya Paris, katika inchi ya Ufaransa.

Mbele ya Langton, wasomi fulani walikuwa wamejaribu kutumia njia mbalimbali za kugawanya Biblia katika sehemu ndogo-ndogo sana ao sura. Inawezekana walifanya vile, zaidi sana, juu ya kusaidia watu kupata maandiko katika Biblia. Unaweza kuwazia namna ingekuwa rahisi sana kwao kupata andiko fulani kama walipaswa kulitafuta katika sura moja tu kuliko katika kitabu chote, kama vile kitabu cha Isaya chenye kuwa na sura 66.

Lakini, yote hayo yalileta tatizo. Wasomi walitokeza namna mbalimbali zenye hazipatane. Kwa mufano, namna moja kati ya hizo iligawanya Injili ya Marko katika sura 50 hivi, kuliko sura 16 zenye tuko nazo leo. Wakati wa Langton, kulikuwa wanafunzi wengi katika muji wa Paris wenye walitoka katika inchi nyingi, na walileta Biblia kutoka katika inchi zao. Lakini, haikukuwa vyepesi kwa walimu na wanafunzi kuonyeshana ni wapi maandiko yenye wanazungumuzia yalikuwa yanatoka. Sababu gani? Kwa sababu namna sura ziligawanywa hazikupatana katika maandishi yao.

Kwa hiyo, Langton alitokeza njia mupya ya kugawanya sura mbalimbali. Kitabu kimoja kinasema kama, namna yake ya kugawanya Biblia “ilipendwa na wasomaji na waandishi wengi,” na “ilienea haraka katika Ulaya.” (The Book—A History of the Bible) Namna yake ya kugawanya sura za Biblia inatumikishwa katika Biblia nyingi leo.

NI NANI ALITIA MISTARI KATIKA BIBLIA?

Kisha miaka 300 hivi, katika mwaka wa 1550 hivi, Robert Estienne, musomi na pia muchapishaji Mufaransa, alifanya mambo kuwa rahisi hata zaidi. Kusudi lake lilikuwa kufanya watu wengi sana wafurahie kujifunza Biblia. Alitambua kama, kuwa na namna ileile ya kugawanya sura na mistari kulikuwa na faida.

Estienne hakuanzisha wazo la kugawanya maandishi ya Biblia katika mistari. Wengine walikuwa wamefanya vile tayari. Kwa mufano, mamia ya miaka mbele ya hapo, waandishi Wayahudi walikuwa wamegawanya Biblia yote ya Kiebrania, ao sehemu ya Biblia yenye watu wengi wanaita Agano la Kale, katika mistari tu lakini hapana sura. Tena, kama vile ilikuwa juu ya sura, hawakugawanya pia mistari namna ileile.

Estienne aligawanya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yenye kuitwa pia Agano Jipya, katika mistari na kuichanga na ile yenye ilikuwa tayari katika Biblia ya Kiebrania. Katika mwaka wa 1553, alichapisha Biblia nzima ya kwanza (katika Kifaransa) yenye kuwa na sura na mistari ileile yenye kuwa katika Biblia nyingi leo. Watu fulani walichambua na kusema kama mistari iligawanya Biblia katika vipande mbalimbali na kufanya ujumbe uonekane kama maneno mbalimbali yenye kuachana. Lakini namna yake ya kugawanya mistari ilikubaliwa haraka na kutumikishwa na wachapishaji wengine wa Biblia.

MUSAADA KWA WANAFUNZI WA BIBLIA

Wazo la kugawanya Biblia katika sura na mistari linaonekana kuwa la mwepesi. Hilo linasaidia kila andiko katika Biblia kuwa na “adresi” yake, kama vile namba ya posta. Kusema kweli, kugawanywa kwa sura na mistari hakukuongozwa na roho ya Mungu, na wakati fulani sura na mistari vinagawanya maandishi ya Biblia mahali penye tunaona kama hakustahili kugawanywa. Lakini, sura na mistari inatusaidia kupata maandiko kwa urahisi na kuyatia alama ao kuonyesha wengine maandiko yenye yanaweza kuwa na maana ya pekee kwetu. Ni vile tunafanya wakati tunatia alama maneno ao misemwa ambayo tunapenda kukumbuka katika kitabu fulani.

Hata kama iko muzuri kuwa na Biblia yenye kugawanywa katika sura na mistari, kumbuka sikuzote kama ni lazima kuelewa ujumbe wote wenye Mungu alitupatia. Uzoee kusoma habari yote kuliko kusoma mistari fulani tu. Kufanya vile kutakusaidia kujua muzuri zaidi ‘maandishi [yote] matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya ukuwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.’—2 Timotheo 3:15.