Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Nilikubali Kweli ya Biblia Hata Kama Sina Mikono

Nilikubali Kweli ya Biblia Hata Kama Sina Mikono

Wakati mutu anaona kama anataka kuanguka, anaweza kukamata kwenye kitu fulani ili asianguke. Lakini mimi siwezi kufanya hivyo kwa sababu sina mikono. Nilikuwa na miaka saba wakati mikono yangu ilipaswa kukatwa ili nibakie muzima.

Mama yangu alikuwa na miaka 17 wakati nilizaliwa katika mwaka wa 1960. Baba yangu alituacha mbele nizaliwe. Mimi na mama yangu tuliishi kwa wazazi wake katika Burg, muji mudogo wa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani ya zamani, ao Ujerumani ya Mashariki. Watu wengi hawakuamini kama kuko Mungu, na familia yetu pia ilikuwa inaunga mukono jambo hilo. Mungu hakumaanisha kitu kwetu.

Kadiri niliendelea kukomaa, nilifurahia kuwa na baba ya mama yangu kwa sababu alinihangaikia. Aliniingiza katika mambo mengi, kama vile kunituma juu ya miti ili kukata matawi. Wakati nilikuwa mutoto, nilipenda mambo hayo. Nilikuwa na maisha ya muzuri na yenye furaha.

AKSIDENTI YENYE ILIBADILISHA MAISHA YANGU

Jambo fulani la kuogopesha sana lilitokea siku moja wakati nilikuwa na miaka saba. Nilikuwa nimetoka tu kuanza mwaka wangu wa pili kwenye masomo. Wakati nilikuwa ninarudia nyumbani, nilipanda kwenye poteau ya umeme. Nguvu ya umeme ilinipiga na kufanya nipoteze ufahamu, wakati nilikuwa nimepanda juu kwenye metre 8. Wakati nilirudisha ufahamu kwenye hospitali, singeweza kusikia tena kama niko na mikono. Mikono yangu iliungua mubaya sana, na kwa sababu vidonda vilikuwa vibaya kabisa, iliomba mikono yangu ikatwe ili damu yangu isipate sumu. Kwa kweli, mama yangu na wazazi wake walivurugika sana. Lakini, kwa sababu nilikuwa mutoto, sikuelewa kabisa kama kukosa mikono kungekuwa na matokeo gani katika maisha yangu.

Kisha kupitisha masiku fulani kwenye hospitali, nilirudia kwenye masomo. Watoto wengine walinicheka, walinisukuma, na walinitupia vitu kwa sababu singeweza kufanya kitu ili kujilinda. Nilihuzunishwa sana na maneno yao yenye kuumiza na yenye mazarau. Mwishowe nilitumwa kwenye Masomo ya Vilema ya Birkenwerder, kwenye wanafunzi vilema walikuwa wanaishi. Kwa sababu masomo ilikuwa mbali na kwetu, mama yangu na wazazi wake hawangeweza kunitembelea. Nilionana nao tu wakati wa mapumuziko. Kwa muda wa miaka kumi yenye ilifuata, nilikomaa bila mama yangu na wazazi wake.

KUKOMAA BILA KUWA NA MIKONO

Nilijifunza kutumia miguu yangu ili kufanya mambo mbalimbali. Waza kidogo namna inaweza kuwa nguvu kwa mutu kukamata kanya ao kijiko kwa kutumia vidole vya miguu ili kula chakula! Hata hivyo, nilijikaza sana kujua namna ya kufanya hivyo. Nilijifunza pia kusafisha meno na kuchanua nywele kwa kutumia miguu. Nilianza hata kufanya ishara na miguu yangu wakati nilikuwa ninazungumuza na watu. Kwa kweli, miguu yangu ilifikia kuwa mikono yangu.

Nilipenda kusoma vitabu vya sayansi vya mambo ya kuwazia wakati nilikuwa kijana. Wakati fulani nilijiwazia kuwa niko na mikono ya kiteknolojia ya hali ya juu yenye ingeniwezesha kufanya kila kitu. Wakati nilikuwa na miaka 14, nilianza kuvuta tumbako. Niliona kama tumbako ilinisaidie nijitumainie na kujiona kama watu wengine. Ilikuwa kama vile nilikuwa ninasema: ‘Ndiyo, na mimi pia naweza kufanya jambo hilo. Watu wenye kuvuta tumbako wanaonekana kuwa wenye kukomaa, hata wakuwe na mikono ao hapana.’

Nilijiingiza katika mambo mbalimbali yenye kufanywa na watu. Niliingia katika kikundi fulani cha vijana chenye kiliungwa mukono na serikali, chenye kuitwa Free German Youth, na nilitumika kama vile muandishi, cheo cha juu katika kikundi cha eneo letu. Tena, nilijiunga na kikundi cha wapiga-muziki, nilifanya mazoezi ya mashairi ao maandishi yenye kupangwa kwa utaratibu fulani, na nilijiingiza pia katika michezo ya vilema. Kisha kupata mazoezi fulani, nilianza kutumika katika kompanyi moja ya muji wetu. Wakati nilikuwa ninakomaa, mara kwa mara nilivaa mikono yenye kutengenezwa kwa sababu nilipenda kuwa mwanaume mwenye kuenea.

KUKUBALI KWELI YA BIBLIA

Siku moja wakati nilikuwa ninachunga train juu ya kuenda kwenye kazi, mwanaume mumoja alinikaribia. Aliniuliza kama ninaweza kuwazia kwamba Mungu iko na uwezo wa kunirudishia mikono yangu tena. Nilivurugika sana. Ni kweli kwamba nilipenda kuwa tena na mikono, lakini niliona kama jambo hilo haliwezekane kabisa! Tangu zamani niliamini kwamba hakuna Mungu. Kuanzia ile siku, nilifanya yangu yote ili kumuepuka mwanaume huyo.

Kisha masiku fulani, mufanyakazi mwenzangu alinialika nitembelee familia yake. Wakati tulikuwa tunakunywa café, wazazi wake walianza kuzungumuza juu ya Yehova Mungu. Kwa mara ya kwanza, nilisikia kama Mungu ana jina. (Zaburi 83:18) Lakini, katika moyo wangu, nilisema hivi: ‘Hakuwezi kuwa Mungu, hata kama ana jina gani. Nitaonyesha watu hawa kama wanasema uongo.’ Kwa sababu nilitumainia mawazo yangu, nilikubali kuwa na mazungumuzo juu ya Biblia. Jambo la kushangaza ni hili: Sikuweza kuleta ushuhuda wenye kuonyesha kwamba hakuna Mungu.

Mawazo yenye nilikuwa nayo kwamba hakuna Mungu, yalianza kubadilika polepole wakati nilikuwa ninachunguza unabii mbalimbali wa Biblia. Unabii mwingi wa Mungu wenye ulitabiriwa zamani ulifikia kutimia, hata kama uliandikwa miaka mingi sana mbele. Siku moja wakati tulikuwa tunazungumuzia Biblia, tulilinganisha mambo yenye kutokea leo katika dunia na unabii wenye kuwa katika Mathayo sura ya 24, Luka sura ya 21, na 2 Timotheo sura ya 3. Kama vile alama mbalimbali zinaweza kusaidia munganga afikie kujua ugonjwa wa mutu fulani, mambo yote yenye kuonyeshwa katika unabii mbalimbali yalinisaidia kuona kama tunaishi katika wakati wenye Biblia inaita “siku za mwisho.” * Nilishangaa sana. Unabii huo mbalimbali ulikuwa unatimia mbele ya macho yangu.

Nilisadiki kwamba mambo yenye nilikuwa ninajifunza yalikuwa ya kweli. Nilianza kusali kwa Yehova Mungu na niliacha kuvuta, hata kama nilikuwa muvutaji wa tumbako kwa miaka mingi. Niliendelea kujifunza Biblia kwa mwaka moja hivi. Tarehe 27 Mwezi wa 4, 1986, nilibatizwa kwa uficho katika beseni kubwa ya kunawia, kwa sababu wakati huo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa yenye kukatazwa katika Ujerumani ya Mashariki.

KUJITOA KWA AJILI YA WATU WENGINE

Kwa sababu kazi yetu ilikatazwa, tulikusanyika katika vikundi vidogo-vidogo katika nyumba za watu na sikujua Mashahidi wengi. Bila kuwazia, wakubwa wa serikali waliniruhusu kufanya safari ya kuenda katika Ujerumani ya Mangaribi, kwenye kazi ya Mashahidi haikukatazwa. Kwa mara ya kwanza, niliweza kuhuzuria mikusanyiko mikubwa yenye kutegemea Biblia na kuonana na ndugu na dada zangu wengi. Siwezi kusahau wakati huo.

Kisha kuanguka kwa ukuta wa Berlin, kazi ya Mashahidi wa Yehova iliruhusiwa. Sasa tungeweza kumuabudu Yehova Mungu kwa uhuru. Nilipenda kuongeza bidii yangu katika kazi ya kuhubiri. Lakini, niliogopa sana kuzungumuza na watu wenye sijue. Nilijisikia kuwa mutu wa bure kwa sababu ya ulemavu wangu na kwa sababu niliishi katika nyumba ya walemavu kwa miaka mingi. Hata hivyo, katika mwaka wa 1992, nilijaribu kuhubiri saa 60 kwa mwezi moja. Niliweza kufanya hivyo na nilipata furaha nyingi. Kwa hiyo, niliamua kuendelea kuhubiri saa 60 kila mwezi na nilijikaza kufanya hivyo muda wa miaka tatu hivi.

Ninaendelea kukumbuka maneno haya ya Biblia: ‘Ni nani aliye zaifu, nami si zaifu?’ (2 Wakorintho 11:29) Hata kama niko kilema, ningali na akili na sauti. Kwa hiyo, ninajikaza sana kuwasaidia wengine. Kwa sababu sina mikono, ninaweza kuelewa kabisa watu wengine wenye kuwa na ulemavu fulani. Ninajua namna mutu anajisikiaka wakati anapenda kabisa kufanya jambo fulani lenye hawezi kufanya. Ninajikaza kutia moyo wale wenye kujisikia hivyo. Kujitoa kwa ajili ya watu wengine katika njia hiyo kunaniletea furaha.

Kutangazia watu wengine habari njema kunaniletea furaha

YEHOVA ANANISAIDIA KILA SIKU

Kusema kweli, wakati fulani, ninavunjika moyo. Ninapenda tu kuwa mwanaume mwenye kuenea. Ninaweza kujifanyia kazi mbalimbali za kila siku, lakini ninatumia nguvu na wakati mwingi kuliko watu wenye kuwa na mikono. Musimamo wangu wa kila siku ni huu: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Kila siku, Yehova ananipatia nguvu yenye niko nayo lazima ili kutimiza mambo ya “kawaida.” Nimeona kwamba Yehova anaendelea kunisaidia. Ndiyo sababu sipendi kumuacha hata kidogo.

Yehova amenibariki kwa kunipatia familia; jambo lenye nilikosa wakati nilikuwa mutoto na kijana. Niko na bibi muzuri sana mwenye kuitwa Elke, ambaye ananipenda na ni mwenye huruma. Tena, Mashahidi wa Yehova wengi sana wamekuwa ndugu na dada zangu wa kiroho, wenye ni familia ya ulimwenguni pote.

Nikiwa pamoja na Elke, bibi yangu mupendwa

Ninatiwa moyo pia na ahadi ya Mungu ya Paradiso. Katika Paradiso hiyo, Mungu atafanya “vitu vyote kuwa vipya,” kutia ndani mikono yangu. (Ufunuo 21:5) Ninaelewa muzuri sana ahadi hiyo wakati ninafikiria mambo yenye Yesu alifanya wakati alikuwa duniani. Wakati fulani, aliponyesha mutu mwenye kuwa kilema na hata kurudisha sikio la mutu fulani lenye lilikatwa. (Mathayo 12:13; Luka 22:50, 51) Ahadi za Yehova na miujiza ya Yesu vinanifanya nisadiki kwamba karibuni nitakuwa tena mwanaume mwenye kuenea.

Lakini, baraka kubwa sana, ni kufikia kumujua Yehova Mungu. Amekuwa baba yangu na rafiki yangu, mwenye kunipatia kitulizo na nguvu. Ninajisikia kama Mufalme Daudi, mwenye aliandika hivi: “Yehova ni nguvu zangu . . . Nami nimesaidiwa, hivi kwamba moyo wangu unashangilia.” (Zaburi 28:7) Ninapenda kuendelea kushikamana na kweli hiyo ya ajabu katika maisha yangu yote. Ninakubali kweli hiyo hata kama sina mikono.

^ fu. 17 Ili kupata habari zaidi kuhusu alama ya siku za mwisho, soma sura ya 9 yenye kichwa “Tunaishi Kweli Katika ‘Siku za Mwisho’?” katika kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? chenye kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova na kinapatikana pia kwenye adresi yetu ya Internete www.mr1310.com.