Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO YA KUFANYA ILI KUWA NA FURAHA KATIKA FAMILIA

Zungumuza na Kijana Wako Bila Kubishana-bishana Naye

Zungumuza na Kijana Wako Bila Kubishana-bishana Naye

“Wakati binti yangu alikuwa na miaka 14, alianza kuzungumuza na mimi bila adabu. Ikiwa ninamuambia, ‘ni wakati wa kula,’ alikuwa ananijibu, ‘Nitakula wakati nitapenda.’ Ikiwa ninamuuliza kama amekwisha kumaliza kazi zake, alikuwa ananiambia, ‘Acha kunisumbua!’ Mara nyingi, mimi naye tulikuwa tunapandisha sauti na kufokeana.”​—MAKI, anaishi JAPANI. *

Ikiwa wewe ni muzazi na una kijana, kubishana na kijana wako kunaweza kujaribu uwezo wako ukiwa muzazi na uvumilivu wako. Maria, mama wa mutoto aliye na miaka 14 ambaye anaishi Brazili anasema hivi: “Wakati binti yangu anapinga mamlaka yangu, jambo hilo linanikasirisha sana. Tunakasirika sana hivi kwamba tunafokeana.” Carmela, ambaye anaishi Italia, anapambana na tatizo kama hilo. Anasema hivi: “Sikuzote, tunabishana sana na mutoto wangu mwanaume, na tunaacha kubishana wakati anajifungia katika chumba chake.”

Sababu gani vijana fulani wanaonekana kuwa wenye kupenda sana mabishano? Je, ni kosa la marafiki wao? Inawezekana. Biblia inasema kwamba marafiki wa mutu wanaweza kumushawishi sana, kwa njia nzuri ao kwa njia mbaya. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Pia, mambo mengi ya kujifurahisha ambayo vijana wanapenda leo yanaonyesha uasi na kukosa heshima kuwa mambo yenye kukubalika kwa vijana.

Lakini kuna mambo mengine ya kufikiria, mambo ambayo si vigumu kuyashugulikia ikiwa unaelewa namna yanavyoweza kuwa na matokeo mabaya juu ya kijana wako. Ona mifano fulani.

KIJANA ANAKOMALISHA ‘NGUVU ZA KUFIKIRI’

Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Nilipokuwa mutoto, nilikuwa nikisema kama mutoto, nikifikiri kama mutoto, nikiwaza kama mutoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mutu muzima, nimeziondolea mbali tabia za mutoto.’ (1 Wakorintho 13:11) Kama vile maneno ya Paulo yanavyoonyesha, watoto na watu wazima hawafikiri namna moja. Katika njia gani?

Watoto wanafikiri kwa kufuata mambo ambayo wanaweza kuona kwa macho. Lakini, mara nyingi watu wazima wana uwezo wa kuelewa mambo yasiyokuwa wazi na kufikiri kwa uzito wanapofikia mwisho wa jambo fulani na wanapochukua maamuzi. Kwa mufano, watu wazima wana mwelekeo zaidi wa kufikiria kanuni za mwenendo muzuri juu ya jambo fulani na kufikiria namna matendo yao yanavyoweza kuwa na matokeo juu ya watu wengine. Wanaweza kuwa wamezoea kufikiri namna hiyo. Lakini vijana hawana uwezo wa kufanya hivyo, wakilinganishwa na watu wazima.

Biblia inatia moyo vijana kukomalisha “uwezo wa kufikiri.” (Methali 1:4) Kwa kweli, Biblia inatia moyo Wakristo wote watumie ‘nguvu zao za kufikiri.’ (Waroma 12:1, 2; Waebrania 5:14) Hata hivyo, wakati fulani, uwezo wa kufikiri wa kijana wako unaweza kumufanya awe mwenye kupenda kubishana na wewe, hata juu ya jambo ambalo linaonekana kuwa ndogo sana. * Ao anaweza kukuelezea mawazo fulani ambayo hayako sawa. (Methali 14:12) Katika hali hiyo, namna gani unaweza kufikiri pamoja naye kuliko kubishana naye?

JARIBU KUFANYA HIVI: Kumbuka kwamba labda kijana wako anajifunza namna ya kufikiri, na anaweza kuwa haamini kabisa mawazo yake. Ili ujue mambo ambayo anasadiki kabisa, kwanza umupongeze kijana wako kwa sababu ya namna yake ya kufikiri. (“Ninapenda namna yako ya kufikiri, hata ikiwa sikubaliane na mawazo yako yote.”) Kisha, umusaidie achunguze namna yake ya kufikiri. (“Unawaza kwamba mambo ambayo unatoka kusema yanaweza kutumiwa katika kila hali?”) Labda unaweza kushangaa juu ya namna kijana wako anavyochunguza tena mawazo yake na kuyanyoosha.

Angalisho: Wakati unafikiri na kijana wako, usiwaze kuwa mawazo yako tu ndiyo yanafaa. Hata ikiwa inaonekana kuwa kijana wako hakubali mambo ambayo unasema, anaweza kufaidika na mazungumuzo yenu kuliko namna ulivyowazia ao kuliko namna atakavyokubaliana na mawazo hayo baadaye. Usishangae ikiwa katika siku chache, kijana wako anakubaliana na mawazo yako, labda hata kusema kwamba hayo yalikuwa mawazo yake.

“Wakati fulani mimi na kijana wangu tulibishana juu ya mambo madogo, kwa mufano, juu ya kuepuka kutumikisha vitu kwa njia mbaya ao juu ya kumuchekelea dada yake. Lakini katika hali nyingi alionekana kuwa anapenda nimuulize mawazo yake na nionyeshe kuwa ninamuelewa na niseme, ‘Aaa, njoo vile!’ ao ‘Hivyo ndivyo unafikiri.’ Ninapokumbuka, ninaona kwamba ikiwa ningesema jambo kama hilo, tungeweza kuepuka mambo mengi ambayo yalifanya tubishane.”​—Kenji, anaishi Japani.

KUMUSAIDIA KIJANA AJIAMINII

Wazazi wenye hekima wanafanya hali za nyumbani ziwe nzuri ili kusaidia vijana wao waeleze maoni yao kwa uhuru

Sehemu kubwa ya kazi ya kulea kijana ni kumutayarisha kwa ajili ya siku ambayo ataondoka nyumbani na kuishi akiwa mutu muzima na mwenye kutimiza madaraka yake. (Mwanzo 2:24) Sehemu ya kazi hiyo inatia ndani kumusaidia kijana akomalishe sifa za kumutambulisha, ni kusema, tabia, imani, na kanuni za mwenendo ambazo zinaonyesha yeye ni mutu wa namna gani. Anapokazwa afanye mambo mabaya, kijana ambaye tayari amekomalisha sifa za kumutambulisha atafanya mambo mengi kuliko kufikiria tu matokeo ya mwenendo wake. Pia atajiuliza hivi: ‘Mimi ni mutu wa namna gani? Ni kanuni gani za mwenendo ambazo ninafuata? Mutu ambaye anafuata kanuni hizo za mwenendo anaweza kufanya nini katika hali hii?’​—2 Petro 3:11.

Biblia inatuambia juu ya Yosefu, kijana ambaye alikomalisha sifa za kumutambulisha. Kwa mufano, wakati bibi ya Potifa alimushawishi alale naye, Yosefu alisema hivi: ‘Ninaweza namna gani kufanya ubaya huu mukubwa na kwa kweli nimutendee Mungu zambi?’ (Mwanzo 39:9) Hata ikiwa Waisraeli walikuwa hawajapewa sheria inayokataza uzinifu, Yosefu alitambua maoni ya Mungu juu ya uzinifu. Zaidi ya hilo, maneno ‘ninaweza namna gani’ yanaonyesha kwamba alikubali maoni ya Mungu juu ya jambo hilo, kwa kuamua hivyo, alikuwa amekomalisha sifa za kumutambulisha.​—Waefeso 5:1.

Kijana wako pia yuko katika hatua za kukomalisha sifa za kumutambulisha. Hilo ni jambo nzuri, kwa sababu kukomalisha sifa ambazo zitamufanya ajiamini kutamusaidia kupambana na vishawishi vya marafiki wake na kupinga vishawishi vyao. (Methali 1:10-15) Kwa upande mwengine, hatua hiyohiyo ya kukomalisha sifa za kumutambulisha inaweza kumuchochea akupinge wewe pia. Ikiwa jambo hilo linatokea, unaweza kufanya nini?

JARIBU KUFANYA HIVI: Kuliko kujiingiza katika mabishano, rudilia tu mawazo yake. (“Sijui ikiwa ninakusikia vizuri. Unasema kwamba . . .”) Kisha, umuulize maulizo. (“Ni nini kinakufanya ujisikie hivyo?” ao “Ni nini kinakufanya ufikie kusema hivyo?”) Saidia kijana wako afunue mambo yaliyo katika moyo wake. Umuache aeleze maoni yake. Ikiwa muna maoni tofauti kwa sababu tu ya mapendezi ya kipekee na si kwamba jambo hilo ni mbaya, umuonyeshe kijana wako kwamba unaweza kuheshimu maoni yake hata ikiwa haukubaliane kabisa naye.

Kijana anapokomalisha sifa za kumutambulisha na sifa zitakazomufanya ajiamini, si jambo la kawaida tu lakini ni jambo lenye kufaidi pia. Kwa vyovyote, Biblia inasema kwamba Wakristo hawapaswe kuwa kama watoto wadogo ambao ‘wanarushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.’ (Waefeso 4:14) Kwa hiyo, umuruhusu na hata umutie moyo kijana wako akomalishe sifa za kumutambulisha na sifa zitakazomufanya ajiamini.

“Ninapowaonyesha mabinti wangu kwamba niko tayari kuwasikiliza, wanakuwa tayari zaidi kukubali maoni yangu, hata ikiwa maoni yangu ni tofauti na yao. Ninakuwa muangalifu ili nisiwalazimishe wakubali mawazo yangu, lakini ninawaacha wakomalishe sifa ambazo zitawafanya wajiamini.”​—Ivana, anaishi katika Jamhuri ya Cheki.

WAZAZI, MUWE NA MUSIMAMO, LAKINI MUBADILIKE KULINGANA NA HALI

Kama watoto wadogo, vijana fulani wamejifunza ufundi wa kurudilia jambo tena na tena ili wazazi wakubali maoni yao. Ikiwa jambo hilo linatokea katika familia yako, uwe muangalifu. Hata ikiwa kukubali jambo fulani kwa sababu kijana wako anakukaza kunaweza kumutuliza kwa muda, kufanya hivyo kunamufundisha kijana wako kwamba kubishana na wewe ndio njia ya kupata kitu ambacho anataka. Ni nini kinaweza kukusaidia kulinda musimamo wako? Fuata shauri hili la Yesu: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” (Mathayo 5:37) Vijana hawatabishana na wewe zaidi ikiwa wanajua kwamba wewe ni mutu ambaye ana musimamo.

Wakati huohuo, uwe mwenye kubadilika kulingana na hali. Kwa mufano, acha kijana wako aeleze sababu gani anafikiri kwamba saa ya kurudi nyumbani ambayo ulimuwekea inapaswa kubadilishwa katika hali fulani. Katika hali hiyo, haubadilishe musimamo wako kwa sababu anakukaza, lakini unafuata tu shauri hili la Biblia: “Usawaziko wenu na ujulikane.”​—Wafilipi 4:5.

JARIBU KUFANYA HIVI: Mufanye mukutano wa familia ambamo mutazungumuzia saa ambazo mulipangia vijana kurudi nyumbani na sheria zingine za nyumbani. Uwaonyeshe kama uko tayari kusikiliza na kuchunguza mambo yote yanayohusika mbele ya kuchukua uamuzi. Roberto, baba mumoja ambaye anaishi Brazili, anashauri hivi: “Vijana wanapaswa kuona kwamba wazazi wao wako tayari kukubali ombi lao ikiwa halivunje kanuni fulani ya Biblia.”

Bila shaka, hakuna muzazi mukamilifu. Biblia inasema hivi: ‘Sisi sote tunajikwaa mara nyingi.’ (Yakobo 3:2) Ikiwa unaona kwamba ulichangia kuleta mabishano kati yako na kijana wako, usisite kumuomba musamaha. Kukubali kosa lako kunamuonyesha kijana wako mufano wa unyenyekevu na kunamusaidia yeye pia atende kwa unyenyekevu.

“Kisha mabishano fulani, wakati hasira yangu iliisha, nilimuomba mutoto wangu musamaha kwa sababu ya hasira yangu kali. Jambo hilo lilimusaidia kutulia na pia lilifanya iwe vyepesi kwake kunisikiliza.”​—Kenji, anaishi Japani.

^ Majina yamebadilishwa katika habari hii.

^ Ijapokuwa katika habari hii tunazungumuza juu ya kijana mwanaume, kanuni zinazozungumuziwa zinahusu pia vijana wanawake.

UJIULIZE . . .

  • Ni katika njia gani labda ninachangia kuleta mabishano kati yangu na kijana wangu?

  • Namna gani ninaweza kutumia mashauri yaliyo katika habari hii ili kunisaidia nimuelewe vizuri kijana wangu?

  • Ninaweza kufanya nini ili kuzungumuza na kijana wangu bila kubishana-bishana naye?