Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sura ya Kenda

Alitenda kwa Busara

Alitenda kwa Busara

1-3. (a) Namna gani watu wa nyumba ya Abigaili wanajikuta katika hatari? (b) Tutajifunza nini kuhusu mwanamuke huyo mwenye sifa za pekee?

ABIGAILI anaona kwamba kijana anayesimama mbele yake mi mwenye kuogopa kabisa. Kijana huyo ana sababu nzuri ya kuogopa. Kuna hatari mulangoni! Wapiganaji 400 hivi wako njiani; wameazimia kuua kila mwanaume katika nyumba ya Nabali, bwana ya Abigaili. Sababu gani?

2 Hatari hiyo inaletwa na Nabali. Yeye ana tabia ya kutenda kwa ukali na kiburi. Lakini, sasa alimutukana mutu ambaye haifae kutukana, alimutukana mukubwa anayependwa wa kikundi cha wapiganaji washikamanifu waliozoezwa vizuri kupigana vita. Sasa, kijana mumoja mufanyakazi wa Nabali, labda muchungaji, amekuja kumuona Abigaili, anatumaini Abigaili atapata namna ya kuwaokoa. Lakini yeye ni mwanamuke tu, atafanya nini ili kuzuia jeshi nzima?

Lakini yeye ni mwanamuke tu, atafanya nini ili kuzuia jeshi nzima?

3 Kwanza, acheni tujifunze mengi juu ya mwanamuke huyo mwenye sifa za pekee. Abigaili alikuwa nani? Hali hiyo ya hatari ilitokea namna gani? Na imani yake inatufundisha nini?

‘Alikuwa Mwenye Busara na Murembo wa Umbo’

4. Nabali ni mutu wa namna gani?

4 Abigaili na Nabali ni watu tofauti kabisa. Abigaili ni mwanamuke mwema sana, lakini ameolewa na mwanaume mubaya sana, Nabali. Ni kweli kwamba, mwanaume huyo ana mali, kwa hiyo anajiona kuwa mutu wa maana sana. Lakini watu wengine wanamuona namna gani? Katika Biblia, ni vigumu kupata mutu anayesemwa vibaya sana hivyo kama Nabali. Kwanza jina lake tu linamaanisha “Mutu Asiye na Akili” ao “Mupumbavu.” Je, ni wazazi wake waliomupa jina hilo alipozaliwa, ao alilipata baadaye kwa sababu ya tabia zake? Iwe ni hivyo ao hapana, jina hilo linamustahili kabisa. Nabali ni ‘mukali na mwenye matendo mabaya.’ Watu wanamuchukia na kumuogopa sana kwa sababu ya ukali na ulevi wake.—1 Sam. 25:2, 3, 17, 21, 25.

5, 6. (a) Ni sifa gani za Abigaili zilizokuwa zenye kuvutia zaidi? (b) Ni nini labda ilimufanya Abigaili akubali kuolewa na mwanaume asiyefaa kitu?

5 Abigaili ni tofauti kabisa na bwana yake. Jina lake linamaanisha “Baba Yangu Mwenyewe Ameshangilia.” Baba wengi wanajivunia kuwa na binti wenye sura nzuri ao warembo; baba mwenye hekima anafurahi zaidi anapotambua kuwa binti wake ana sifa nzuri. Mara nyingi, mwanamuke mwenye sura nzuri haone sababu ya kuwa na sifa kama vile busara, hekima, ujasiri, ao imani. Lakini Abigaili hakuwa hivyo. Biblia inamusifu kwa sababu ya busara yake na pia sura yake nzuri.—Soma 1 Samweli 25:3.

6 Watu fulani leo wanaweza kujiuliza sababu gani mwanamuke kijana kama huyo na mwenye akili aliolewa na mwanaume kama huyo asiyefaa kitu. Kumbuka kwamba nyakati za zamani ndoa nyingi zilipangwa na wazazi. Hata hali katika ndoa iwe namna gani, makubaliano ya wazazi yaliheshimiwa sana. Je, wazazi wa Abigaili walimutia moyo aolewe na Nabali ao ni wao ndio waliopanga ndoa hiyo, kwa sababu waliona tu utajiri wa Nabali ao kwa sababu alikuwa mutu mwenye kujulikana? Je, walikubali aolewe naye kwa sababu tu walikuwa masikini kabisa? Hata sababu iwe gani, feza za Nabali hazikumufanya awe bwana muzuri.

7. (a) Leo wazazi wanapaswa kuepuka nini ikiwa wanataka kuwafundisha watoto wao wawe na maoni yanayofaa kuhusu ndoa? (b) Abigaili anaazimia kufanya nini?

7 Wazazi wenye hekima wanajikaza kuwafundisha watoto wao wawe na maoni yenye kufaa kuhusu ndoa. Hawawatie moyo watoto wao kuolewa ao kuoa kwa sababu ya feza, wala hawawasukume waanze uchumba mbele ya wao kukomaa vya kutosha ili kuweza kutimiza madaraka ya mutu mwenye kuoa ao kuolewa. (1 Kor. 7:36) Hata hivyo, kuhusu Abigaili maji yamekwisha kumwangika; kwa hiyo, yeye hafikirie tena mambo hayo. Amekwisha kuolewa na Nabali, na anaazimia kufanya yote anayoweza ili kutuliza hali hiyo ngumu.

Nabali ‘Anawakemea kwa Sauti Kali’

8. Nabali amemutukana nani, na sababu gani ulikuwa upumbavu kabisa kufanya hivyo?

8 Nabali amefanya hali ya Abigaili iwe ngumu hata zaidi. Mwanaume ambaye Nabali ametukana si mutu wa burebure, ni Daudi. Daudi ni mutumishi mwaminifu wa Yehova ambaye nabii Samweli alitia mafuta ili kuonyesha kwamba amechaguliwa na Mungu awe mufalme baada ya Sauli. (1 Sam. 16:1, 2, 11-13) Mufalme Sauli anasikia wivu na anataka kumuua; basi Daudi anakimbilia jangwani ambamo anaishi pamoja na wapiganaji wake washikamanifu 600.

9, 10. (a) Daudi na wanaume wake wanafanya nini ili wapate kuishi? (b) Sababu gani Nabali angepaswa kufurahia yale ambayo Daudi na wanaume wake wanamufanyia? (Soma pia maelezo yaliyo chini yanayohusiana na fungu la 10.)

9 Nabali anaishi huko Maoni, lakini anafanya kazi katika muji wa karibu wa Karmeli ambako inawezekana ana mashamba. * Miji hiyo miwili inapatikana katikati ya maeneo yanayoinuka yenye majani mazuri kwa ufugaji wa kondoo, huko Nabali ana kondoo 3000. Hata hivyo, hakuna mashamba katika maeneo yote ya kandokando. Kuna jangwa kubwa la Parani upande wa kusini. Upande wa mashariki, kuna barabara inayoelekea kwenye Bahari ya Chumvi inayopitia maeneo yenye kukauka, yenye mabonde na mapango. Daudi na watu wake wanajikaza sana kuishi katika maeneo hayo. Ili kupata chakula, wanawinda wanyama, na pia wanavumilia hali nyingi ngumu. Mara nyingi wanakutana na vijana wachungaji ambao ni watumishi wa Nabali, mwanaume tajiri.

10 Askari hao wenye bidii wa Daudi wanawatendea wachungaji hao wa Nabali namna gani? Ingekuwa rahisi kwao kunyanganya kondoo mara kwa mara, lakini hawafanye hivyo. Kuliko kufanya hivyo, wanalinda wanyama wa Nabali na watumishi wake. (Soma 1 Samweli 25:15, 16.) Siku hizo, kondoo na wachungaji walikuwa wanapambana na hatari nyingi. Wanyama hatari wa porini walikuwa wengi, na mupaka wa kusini wa Israeli ulikuwa karibu sana, kwa hiyo, vikundi vya wanyanganyi na wezi kutoka upande huo vilishambulia watu mara kwa mara. *

11, 12. (a) Namna gani Daudi anaonyesha heshima na busara anapomutumia Nabali ujumbe? (b) Sababu gani namna ambayo Nabali anamujibu Daudi si nzuri?

11 Bila shaka, ilikuwa vigumu kuendelea kuwalisha wanaume hao wote jangwani. Kwa hiyo, siku moja Daudi anamutumia Nabali wajumbe kumi ili kuomba musaada. Daudi anachagua kwa hekima wakati wa kufanya hivyo. Ni wakati wa sikukuu ya kukata kondoo manyoya, wakati huo kwa kawaida watu wanafanya karamu na kutendeana kwa ukarimu. Tena Daudi anachagua kwa uangalifu maneno ya adabu watakayomuambia Nabali. Hata anajitambulisha kwa Nabali kwa kutumia maneno “Daudi mwana wako,” labda anatambua kwa adabu kama Nabali anamushinda miaka. Nabali anafanya nini?​—1 Sam. 25:5-8.

12 Anakasirika sana! Yule kijana aliyetajwa mwanzoni anamuelezea Abigaili jinsi Nabali ‘aliwakemea kwa sauti kali,’ watumishi wa Daudi. Kwa sababu ya uchoyo, Nabali anafoka vikali kwa kuwa wanamuomba maji, nyama, na mukate wake wenye bei sana. Anamuchekelea Daudi, anamuona kuwa mutu wa bure na hata anamulinganisha na mutumishi anayetoroka bwana wake. Inawezekana Nabali ana mawazo kama ya Sauli, ambaye anamuchukia Daudi. Nabali na Sauli hawaone mambo kama Yehova. Mungu anamupenda Daudi na hamuone kuwa mutumwa muasi, lakini anamuona kuwa mufalme wa Israeli wa wakati ujao.​—1 Sam. 25:10, 11, 14.

13. (a) Daudi anafanya nini mara tu anaposikia jibu mbaya la Nabali? (b) Kanuni iliyo katika andiko la Yakobo 1:20 inatusaidia namna gani kujua kwamba Daudi anafanya vibaya?

13 Wakati wajumbe wa Daudi wanarudia na kumuambia mambo yote, Daudi anakasirika sana. Anaamuru hivi: ‘Kila mutu ajifunge upanga wake!’ Daudi mwenyewe anachukua silaha na yuko mbele ya wanaume wake 400 ili kushambulia nyumba ya Nabali. Anaapa kwamba ataangamiza kabisa kila mwanaume katika nyumba hiyo. (1 Sam. 25:12, 13, 21, 22) Daudi ana sheria ya kukasirika, lakini haonyeshe hasira yake kwa njia inayofaa. Biblia inasema: ‘Gazabu ya mwanadamu haitokeze uadilifu [ao haki] wa Mungu.’ (Yak. 1:20) Sasa, Abigaili atafanya nini ili kuokoa watu wa nyumba yake?

“Busara Yako na Ibarikiwe”

14. (a) Ni katika njia gani tayari Abigaili amekwisha kufanya hatua ya kwanza ili kutengeneza kosa kubwa la Nabali? (b) Tofauti kati ya Nabali na Abigaili inatufundisha nini? (Soma pia maelezo yaliyo chini.)

14 Kwa njia fulani, tumeona kwamba tayari Abigaili amekwisha kufanya hatua ya kwanza ili kutengeneza kosa kubwa la Nabali. Tofauti na bwana yake, Abigaili iko tayari kusikiliza. Kuliko yule kijana mutumishi aende kumuelezea Nabali hatari inayokuja, yeye anasema hivi juu ya Nabali: ‘Yeye ni mutu asiyefaa kitu sana hata mutu hawezi kusema naye.’ * (1 Sam. 25:17) Inasikitisha kwamba Nabali hana wakati wa kusikiliza wengine kwa sababu anajiona kuwa mutu wa maana sana. Leo, watu wengi wana kiburi kama hicho. Lakini kijana huyo anajua kama Abigaili iko tofauti, na ndio sababu anamuendea ili kumujulisha tatizo hilo.

Tofauti na Nabali, Abigaili iko tayari kusikiliza

15, 16. (a) Abigaili anaonyesha namna gani kwamba yeye ni kama yule mwanamuke mwenye uwezo aliyezungumuziwa katika kitabu cha Methali? (b) Sababu gani jambo ambalo Abigaili anafanya halimaanishe kama ni mwenye kuasi ukichwa wa bwana yake?

15 Abigaili anafikiri na kutenda kwa haraka. Tunasoma hivi: “Mara moja Abigaili akafanya haraka.” Habari hii ya Biblia inatumia mara ine maneno “kufanya haraka” inapozungumuzia mwanamuke huyo. Anatayarisha zawadi kubwa ya kumupatia Daudi na wanaume wake. Zawadi hiyo ni mikate, divai, kondoo, nafaka iliyokaangwa, keki za zabibu, na keki za tini. Inaonekana wazi kama Abigaili anajua vizuri vitu alivyo navyo na anajua daraka lake katika nyumba yao, kama yule mwanamuke mwenye uwezo aliyezungumuziwa baadaye katika kitabu cha Methali. (Met. 31:10-31) Anawatuma watumishi wake watangulie na zawadi hiyo, kisha anawafuata akiwa peke yake. Biblia inasema hivi: ‘Lakini hakumuambia Nabali [bwana yake] jambo lolote.’—1 Sam. 25:18, 19.

16 Je, hilo linamaanisha kama Abigaili ni mwenye kuasi ukichwa wa bwana yake? Hapana; kumbuka kwamba Nabali alimutukana vibaya mutumishi mutiwa​-mafuta wa Yehova, tendo ambalo linaweza kufanya watu wengi wasio na kosa katika nyumba ya Nabali wauawe. Ikiwa Abigaili hafanye jambo lolote, kosa la bwana yake linaweza pia kuwa juu yake. Kwa hiyo, anapaswa kwanza kumutii Mungu kuliko kumutii bwana yake.

17, 18. Abigaili anamukaribia Daudi namna gani, anamuambia nini, na sababu gani maneno anayosema yana matokeo mazuri?

17 Kisha muda mufupi, Abigaili anakutana na Daudi na wanaume wake. Kwa mara hii tena anafanya haraka, anashuka mbio kwenye punda wake, na kujinyenyekeza mbele ya Daudi. (1 Sam. 25:20, 23) Kisha, anamufunulia yote yaliyo katika moyo wake, anamulilia sana Daudi amuhurumie bwana yake na watu wa nyumba yake. Ni nini kinachofanya maneno yake yawe yenye matokeo mazuri?

‘Tafazali muache kijakazi wako aseme masikioni mwako’

18 Anabeba kosa la bwana yake na anamuomba Daudi amusamehe yeye. Anakubali kama bwana yake ni mutu asiyefaa kitu kama jina lake linavyoonyesha, labda ili kumusaidia Daudi atambue kwamba kumuazibu mutu kama huyo ni kujishushia heshima. Anaonyesha kwamba anaamini Daudi ni mutumishi wa Yehova, na anatambua kama vita ambayo Daudi anapigana ni ‘vita ya Yehova.’ Pia, Abigaili anaonyesha kama anajua ahadi ya Yehova kumuhusu Daudi na ufalme, kwa sababu anasema hivi: “Yehova . . . hakika atakuweka kuwa kiongozi juu ya Israeli.” Zaidi ya hayo, anamushauri Daudi asifanye jambo lolote ambalo linaweza kumufanya awe na deni la damu ao asifanye jambo lolote ambalo baadaye litakuwa ‘sababu ya kufazaika,’ ni kusema, litasumbua zamiri yake. (Soma 1 Samweli 25:24-31.) Hayo ni maneno mema na yenye kugusa moyo kabisa!

19. Daudi anamujibu Abigaili namna gani, na sababu gani anamusifu mwanamuke huyo?

19 Sasa Daudi anaposikia maneno hayo, anafanya nini? Anakubali zawadi ambayo Abigaili ameleta na kisha anasema hivi: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.” Daudi anamusifu Abigaili kwa sababu amekuja haraka kwa ujasiri ili kukutana naye, na anatambua kama amemuepusha kuwa na deni la damu. Daudi anamuambia Abigaili, “Panda uende kwa amani nyumbani kwako,” kisha anaongeza hivi kwa unyenyekevu: “Nimeisikiliza sauti yako.”​—1 Sam. 25:32-35.

“Tazama, Mimi Ni Kijakazi Wako”

20, 21. (a) Sababu gani ni jambo lenye kushangaza kuona Abigaili iko tayari kurudi kwa bwana yake? (b) Namna gani Abigaili anaonyesha ujasiri na busara kwa kuchagua wakati wa kuongea na Nabali?

20 Kisha kuachana, Abigaili hangeweza kusahau wakati huo ambao amekutana na Daudi; na bila shaka, anaona tofauti kati ya mwanaume huyo mwaminifu na mwema, na Nabali, bwana yake, ambaye ni mutu mukali. Lakini haendelee kufikiria mambo hayo. Tunasoma hivi: “Baadaye Abigaili akaingia kwa Nabali.” Ndiyo, anarudia kwa bwana yake na anaazimia kabisa kuendelea kutimiza daraka lake la mwanamuke mwenye kuolewa kadiri ya uwezo wake. Anapaswa kumuambia bwana yake juu ya zawadi aliyomupa Daudi na wanaume wake. Nabali ana haki ya kujua jambo hilo. Pia, Abigaili anapaswa kumuelezea Nabali hatua aliyochukua ili kuzuia hali ya hatari iliyotaka kutukia, kwa sababu ikiwa Nabali anaisikia kupitia watu wengine, hilo linaweza kumupatisha haya sana. Lakini kwa sasa Abigaili hawezi kumuambia mambo hayo. Nabali ni mwenye kufanya karamu kama ya mufalme na amelewa sana.​—1 Sam. 25:36.

Kwa ujasiri, Abigaili alimuambia Nabali mambo aliyofanya ili kuokoa uzima wake

21 Kwa mara ingine tena, Abigaili anaonyesha ujasiri na busara, anangojea mupaka asubuhi wakati ulevi wa Nabali unamutoka. Katika hali hiyo, Nabali anaweza kumusikiliza bibi yake, lakini tabia yake ya kukasirika bado ni yenye kuogopesha. Hata hivyo, Abigaili anamukaribia na kumuelezea habari yote. Bila shaka, Abigaili anawaza kwamba bwana yake atatomboka kwa hasira, ao labda kumutendea vibaya. Badala yake, Nabali anabaki bila kutikisika.​—1 Sam. 25:37.

22. Nabali anapatwa na nini, na habari hiyo inatufundisha nini kuhusu watu wote wanaotendewa vibaya ao kwa ukali katika familia?

22 Mwanaume huyo anapatwa na nini? Biblia inasema kwamba ‘moyo wake ukafa ndani yake, naye akawa kama jiwe.’ Labda ameshikwa na aina fulani ya ugonjwa unaofanya kiungo fulani cha mwili kiache kufanya kazi. Hata hivyo, kisha siku kumi hivi, anakufa, na si kwa sababu tu ya ugonjwa huo. Biblia inaeleza hivi: ‘Yehova akamupiga Nabali, naye akafa.’ (1 Sam. 25:38) Hivyo, kifo hicho cha haki kinavunja ndoa ya taabu ya miaka mingi ya Abigaili. Hata ikiwa leo Yehova hawaue watu kimuujiza, habari hiyo inatufundisha kwamba kila mara mutu anapotendewa vibaya ao kwa ukali katika familia, Yehova anaona hilo. Kwa wakati wake, Yehova hatakosa kutengeneza mambo.​—Soma Luka 8:17.

23. Abigaili anapata baraka ingine gani, na anaonyesha namna gani kama habadilike kwa sababu ya baraka hiyo?

23 Kifo hicho kinamukomboa Abigaili, na zaidi ya hilo, anapata baraka ingine. Wakati Daudi anapata habari ya kifo cha Nabali, anawatuma wajumbe kwa Abigaili ili kumuomba awe bibi yake. Abigaili anajibu hivi: ‘Tazama, mimi ni kijakazi wako, niwe mujakazi wa kuosha miguu ya watumishi wa bwana wangu.’ Ni wazi kama Abigaili habadilike kwa sababu ya baraka hiyo ya kuwa bibi ya Daudi; anajitolea hata kuwa kijakazi wa watumishi wa Daudi! Kisha hapo, Abigaili anatuonyesha tena sifa yake ya kutochelewesha mambo, anajitayarisha haraka ili kuenda kuishi na Daudi.​—1 Sam. 25:39-42.

24. Abigaili alipambana na matatizo gani maishani mwake, lakini bwana yake Daudi na Mungu wake walimuona namna gani?

24 Hilo halimaanishe kama Abigaili hatakuwa tena na matatizo katika maisha yake; si kusema kwamba maisha ya Abigaili na Daudi yatakuwa tu ya raha sikuzote. Tayari Daudi ana bibi mwengine, Ahinoamu; wakati huo Mungu aliwaruhusu wanaume kuwa na bibi wengi, kwa hiyo, wanawake wengi waaminifu wa zamani waliokuwa katika ndoa ya bibi wengi walipambana na matatizo. Jambo lingine ni kwamba Daudi hajakuwa bado mufalme, itamuomba kupambana na vipingamizi na matatizo mengi mbele aanze kumutumikia Yehova katika daraka hilo. Lakini Abigaili anamusaidia na kumutegemeza Daudi katika maisha yake yote, na hata kumuzalia mutoto mwanaume; kwa kufanya hivyo, anafikia kutambua kama ana bwana ambaye anamuona kuwa wa maana na kumulinda. Na siku moja Daudi alimuokoa hata kutoka katika mikono ya wanyanganyi walioshambulia muji wa Siklagi! (1 Sam. 30:1-19) Kwa kufanya hivyo, Daudi alimuiga Yehova Mungu, ambaye anawapenda na kuwaheshimu wanawake kama hao, wenye busara, ujasiri, na waaminifu.

^ fu. 9 Huo si ule Mulima Karmeli unaojulikana na ulio mbali huko kaskazini ambako baadaye nabii Eliya alishindana na manabii wa Baali. (Soma Sura ya 10.) Lakini ni muji ulio kwenye ukingo wa jangwa la kusini.

^ fu. 10 Inaonekana kwamba Daudi aliona jambo la kuwalinda walimaji Waisraeli na wanyama wao wa kufugwa kuwa sehemu ya utumishi wake kwa Yehova Mungu. Katika siku hizo, Yehova alikusudia wazao wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo waishi katika eneo hilo. Kwa hiyo, kulinda eneo hilo ili wageni na wanyanganyi wasilishambulie ilikuwa sehemu ya utumishi mutakatifu.

^ fu. 14 Maneno ambayo kijana huyo alitumia yanamaanisha “mwana wa beliali (mutu ovyo, wa burebure).” Tafsiri zingine za Biblia zinazozungumuzia andiko hilo zinaonyesha pia kama Nabali ni mwanaume “asiyemusikiliza yeyote,” na kwa hiyo, “hakuna faida ya kuzungumuza naye.”