Hamia kwenye habari

Ndugu Sanderson akizungumza na wajitoleaji na wakimbizi nchini Poland

MEI 18, 2022
POLAND

Ziara ya Pekee kwa Wajitoleaji na Wakimbizi wa Ukrainia Walio Poland

Ziara ya Pekee kwa Wajitoleaji na Wakimbizi wa Ukrainia Walio Poland

Kuanzia Jumapili, Mei 1, Ndugu Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, pamoja na washiriki watatu wa Halmashauri za Ofisi za Tawi, waliwatembelea ndugu na dada ambao wamekimbia kutoka Ukrainia kwenda Poland. Katika ziara hiyo ndugu Sanderson na ndugu waliokuwa pamoja naye walisikiliza masimulizi kutoka kwa wakimbizi na kuwahakikishia kwamba Baraza Linaloongoza linawapenda sana na litaendelea kuwategemeza.

Kushoto hadi kulia: Tomasz Wolczko mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Poland, Mark Sanderson, Vesa Väänänen mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Poland, na Tommi Kauko mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Finland

Akina ndugu wakizungumzia jitihada za kutoa msaada mpakani

Kwa muda wa siku sita, kikundi hicho kilisafiri umbali wa kilomita 2,500, ili kuwatembelea wakimbizi waliokuwa wakikaa katika maeneo mbalimbali. Maeneo hayo yanatia ndani Majumba manne ya Kusanyiko pamoja na Majumba kadhaa ya Ufalme. Pia walikutana na wajitoleaji waliokuwa kwenye maeneo kadhaa mpakani mwa Poland na Ukrainia.

Ndugu mmoja kutoka Ukrainia anasema: “Ziara hiyo ilitutia moyo sana na ilituburudisha kama tu kikombe cha maji baridi katika siku yenye joto.”

Dada mmoja kutoka Ukrainia alisema hivi: “Hatukutazamia ziara hiyo. Kwa kweli tumejionea jinsi Yehova anavyotujali.”

Dada mwingine kutoka Ukrainia alisema hivi: “Tulipofika Poland hatukuwa na chochote, lakini sasa kwa msaada wa Yehova tuna kila kitu tunachohitaji.”

Kikundi cha madereva na wajitoleaji wengine nje ya Jumba la Kusanyiko lililo Stęszew, nchini Poland

Kikundi hicho pia kilikutana na wajitoleaji wanaowasaidia wakimbizi. Ndugu Sanderson aliwakumbusha kwamba Baraza Linaloongoza linawapenda alipotaja andiko la Waebrania 6:10 na kuwaeleza kwamba Yehova ‘hatasahau kazi yao.’ Pia, alisema, “Sisi pia hatutasahau kazi yenu.” Wajitoleaji hao walisema kwamba wanathamini sana pendeleo la kuwasaidia ndugu na dada zao.

Wakiwatembelea dada wenye umri mkubwa nje ya Jumba la Ufalme lililo Radymno, nchini Poland

Ndugu Vesa Väänänen mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Poland alisema hivi: “Ni jambo linaloimarisha sana imani kujionea moja kwa moja jinsi Yehova anavyoongoza mambo. Yehova ameandaa msaada unaohitajika kwa wakati unaofaa kupitia mwongozo wa Baraza Linaloongoza na pia kupitia ndugu na dada ambao wako tayari kuwasaidia wengine.”

Wajitoleaji walio kwenye Jumba la Kusanyiko la Stęszew, nchini Poland, ambako misaada inatayarishwa

Kadiri ndugu na dada zetu wanavyoendelea kushughulikia mahitaji ya wengine licha ya hali zilizopo, wanapata furaha inayotokana na kutoa ambayo Yesu aliahidi.​—Matendo 20:35.