Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA

Jinsi ya Kumsaidia Mtoto Wako Afanye Vizuri Shuleni

Jinsi ya Kumsaidia Mtoto Wako Afanye Vizuri Shuleni

 Umetambua kwamba mtoto wako hajali kuhusu shule, hajifunzi nyumbani, wala hafanyi kazi za shule anazopaswa kufanyia nyumbani. Hali inakuwaje? Anapata matokeo ya chini na mtazamo wake kuelekea shule unaharibika zaidi. Unaweza kumsaidiaje mtoto wako afanye vizuri zaidi shuleni?

 Unachopaswa kujua

 Kumshinikiza kunaongeza tatizo. Kumshinikiza mtoto wako kutamfanya awe na mahangaiko shuleni na nyumbani! Ili kupunguza mkazo huo, huenda akasema uwongo, akaficha alama zake za chini, akatia sahihi yako kwenye ripoti ya shule, au akakosa kwenda shuleni. Tatizo litazidi tu kuongezeka.

 Kumpa zawadi kunaweza kuwa na matokeo mabaya. Baba anayeitwa Andrew anasema hivi: “Ili kumchochea binti yetu, tulijaribu kumpa zawadi alipofaulu shuleni, lakini hilo lilimfanya azingatie tu kupata zawadi. Alipokosa kufaulu, alihuzunishwa zaidi na kukosa zawadi badala ya kusikitishwa na alama zake za chini.”

 Kuwalaumu walimu hakutamsaidia mtoto. Huenda mtoto wako akafikia mkataa kwamba hahitaji kutia jitihada ili apate matokeo mazuri. Huenda pia akajifunza kuwalaumu wengine anapokosea na kutarajia kwamba watu wengine watatatua matatizo yake. Kwa ufupi, mtoto wako anaweza kukosa kujifunza ustadi muhimu sana atakaohitaji anapokuwa mtu mzima, yaani, kukubali kuwajibika kwa ajili ya matendo yake.

 Unachoweza kufanya

 Dhibiti hisia zako. Unapokasirika, panga wakati mwingine wa kuzungumzia matokeo pamoja na mtoto wako. Baba anayeitwa Brett anasema hivi: “Mimi na mke wangu tumefaulu kwa sababu ya kuzungumza tunapokuwa tumetulia na wakati ambapo tunaweza kuzingatia hisia za mtoto wetu.”

 Kanuni ya Biblia: ‘Uwe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.’​—Yakobo 1:​19.

 Kutambua tatizo lenyewe. Sababu za kawaida zinazoweza kumfanya mtoto apate alama za chini ni kuonewa, kuhama shule, kupatwa na woga kabla au wakati wa mitihani, matatizo ya familia, kukosa usingizi, kukosa kuwa na ratiba nzuri, au kukosa kukaza fikira. Usiamue haraka kwamba mtoto wako ni mvivu.

 Kanuni ya Biblia: “Mtu anayeonyesha ufahamu katika jambo atapata mafanikio.”​—Methali 16:20.

 Hakikisha kuna mazingira yanayofaa kujifunza. Tayarisha ratiba ya kufanya migawo ya shule na ya kujifunza. Tenga mahali ambapo mtoto wako anaweza kufanya migawo aliyopewa shuleni bila kukengeushwa (iwe na televisheni au na simu za mkononi). Panga vipindi vya kufanya migawo ya shule viwe vifupi-vifupi ili kumsaidia mtoto wako akaze fikira. Hector, baba nchini Ujerumani anasema, “Ikiwa kuna mtihani utakaofanywa karibuni, tunajikumbusha mambo machache pamoja naye kila siku badala ya kusubiri hadi dakika ya mwisho.”

 Kanuni ya Biblia: “Kuna wakati uliowekwa wa kila jambo.”​—Mhubiri 3:1.”

 Mtie moyo ajifunze. Mtoto wako anapoelewa jinsi shule inavyomnufaisha sasa, atachochewa kujifunza. Kwa mfano, hesabu inaweza kumsaidia kupanga bajeti ya pesa unazompa.

 Kanuni ya Biblia: “Jipatie hekima, jipatie uelewaji. . . . Ithamini sana.”​—Methali 4:​5, 8.

 Dokezo: Msaidie mtoto wako kufanya migawo yake ya shule, lakini usiifanye kwa niaba yake. Andrew anakubali hivi, “Binti yetu alitegemea akili zetu kupata majibu na hakutumia akili yake.” Mfundishe mtoto wako jinsi ya kujifanyia kazi zake za shule.