Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Ambayo Wazazi Wanaweza Kufanya

Mambo Ambayo Wazazi Wanaweza Kufanya

“Wanafunzi wengi sana walisongamana katika darasa moja! Hakukuwa na feni, na joto lilikuwa jingi sana.”​—Luis, Bolivia.

“Shule yetu ilikuwa na walimu wachache, kwa hiyo wanafunzi hawakupata uangalifu waliohitaji. Shule hiyo haikuwa na ramani, vifaa vya maabara, wala maktaba.”​—Dorcus, Myanmar.

“Walimu wengi walijitahidi kudhibiti darasa. Nyakati nyingine wanafunzi walikuwa watundu sana, jambo lililofanya iwe vigumu kujifunza.”​—Nina, Afrika Kusini.

KAMA maelezo yaliyo hapo juu yanavyoonyesha, mazingira katika shule fulani yanafanya iwe vigumu sana kujifunza. Ukiwa mzazi, unawezaje kuwasaidia watoto wako wafaidike na elimu yao licha ya magumu hayo? Yafuatayo ni mapendekezo fulani.

Chukua hatua ya kwanza.

Badala ya kukazia fikira matatizo—mengi ambayo huenda huna uwezo wa kuyasuluhisha—kazia fikira mambo ambayo wewe unaweza kufanya. Ikiwa mtoto wako haelewi somo fulani au amelemewa na kazi nyingi sana za shuleni, zungumza naye na mtafute suluhisho pamoja. Kwa mfano, je, unahitaji kumtengea mtoto wako mahali panapofaa zaidi pa kujifunzia? Je, mtoto wako anahitaji kusaidiwa kupanga ratiba ili aweze kutimiza mambo yaliyo ya maana zaidi? Je, atanufaika kwa kupata mwalimu wa ziada wa kumfunza nyumbani? Ili upate madokezo zaidi, huenda ingefaa uzungumze na walimu wa mtoto wako. Waone kuwa marafiki, si maadui.

Msaidie mtoto wako akazie fikira lengo la kupata elimu.

Elimu inapaswa kumsaidia mtoto wako awe mtu mzima mwenye usawaziko na mwenye kutegemeka. Lengo la elimu halipaswi kuwa tu kupata mali. Hata hivyo, utafiti unaonyesha kwamba vijana wengi hufuatilia elimu wakiwa na lengo hilo akilini, yaani kuwa matajiri. Biblia ina maoni yaliyosawazika kuhusu vitu vya kimwili. Ingawa inakubali kwamba “pesa ni ulinzi,” inaonya pia kwamba “wale ambao wameazimia kuwa matajiri” hawatapata furaha ya kweli.​—Mhubiri 7:12; 1 Timotheo 6:9.

Acha mtoto wako ajifunze kupitia hali ngumu anazokabili.

Walimu wengi wanasema kwamba ingawa wanafunzi fulani ni wagumu kushughulika nao, inakuwa vigumu hata zaidi kushughulika na wazazi fulani. Wazazi fulani hulalamika mwana au binti yao anapoingia matatani au anapopata alama za chini katika mtihani. Kwa mfano, ripoti moja katika gazeti Time inasema kwamba profesa fulani wa chuo kimoja alikuwa na wanafunzi fulani ambao “walikuwa na zoea la kuwapigia simu wazazi wao wakiwa darasani na kulalamika kuhusu alama za chini katika mtihani kisha, darasa likiwa bado linaendelea, wanampa profesa huyo simu kwa kuwa mzazi anataka kuingilia kati. Na pia kuna wazazi fulani ambao wamemwambia kwamba wanalipa pesa nyingi sana kwa ajili ya elimu ya mtoto wao, kwa hiyo lazima mtoto wao apate alama za juu kabisa.”

Wazazi wa aina hiyo hawawasaidii watoto wao hata kidogo. Kwa kweli, badala ya kuwasaidia watoto wao, wanawazuia “kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi, kuhisi jinsi mtu anavyohisi anapoanguka mtihani, na kukabiliana na matokeo ya maamuzi yao mabaya,” anaandika Polly Young-Eisendrath, katika kitabu chake, The Self-Esteem Trap. Mwandishi huyo anaendelea kusema: “Ikiwa wazazi wataingilia kati na kutatua matatizo ya watoto wao huku watoto wakikaa kitako bila kufanya lolote, wazazi hao watakuwa na uzoefu wa kutatua matatizo, lakini watoto wao watashindwa kutatua matatizo yao watakapokuwa mbali na wazazi.”

Uwe na usawaziko kuhusu kiasi cha elimu ambacho mtoto wako atapata.

Kama ilivyotajwa awali, elimu inaweza kumsaidia mtoto wako awe mtu mzima anayetegemeka. (Mwanzo 2:24) Lakini mtoto wako anahitaji elimu ya aina gani ili kufikia lengo hilo?

Usidhani kwamba lazima mtoto wako aende kwenye chuo kikuu ili apate kazi nzuri. Unaweza kuchagua njia nyingine ambazo hazitakugharimu sana. Kwa kweli, katika visa fulani, stadi fulani za kiufundi zinaweza kumfanya mtoto wako awe na kazi nzuri kama ile ya wahitimu wa vyuo vikuu.

Jambo kuu: Hakuna shule isiyo na kasoro, na watoto leo wanakabiliana na magumu ambayo hayakuwepo miaka michache iliyopita. Lakini kwa msaada wako, mtoto wako anaweza kufanikiwa shuleni! Mkiwa familia, mbona msizungumzie mapendekezo yaliyotajwa kwenye ukurasa wa 3 hadi wa 7 wa gazeti hili?