Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa Mimba?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa Mimba?

Jibu la Biblia

 Biblia haitumii maneno kutoa mimba katika maana ya mtu kutoa kimakusudi kijusi cha kibinadamu. Hata hivyo, mistari mingi ya Biblia inazungumzia maoni ya Mungu kuhusu uhai wa mwanadamu, kutia ndani ule wa kitoto ambacho hakijazaliwa.

 Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Mwanzo 9:6; Zaburi 36:9) Anauona uhai wote kuwa wenye thamani, kutia ndani uhai wa mtoto aliye bado katika tumbo la uzazi. Kwa hiyo, mtu anapomuua kimakusudi mtoto ambaye bado hajazaliwa, huo ni uuaji.

 Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilisema hivi: “Wanaume wakipambana na kumuumiza mwanamke mwenye mimba naye azae kabla ya wakati lakini kifo kisitokee, yule aliyemuumiza atalipa hasara atakayodaiwa na mume wa mwanamke huyo; naye atalipa kupitia waamuzi. Lakini kifo kikitokea, basi ni lazima mlipe uhai kwa uhai.”—Kutoka 21:22, 23. a

 Uhai wa mwanadamu unaanza wakati gani?

 Kwa maoni ya Mungu uhai wa mwanadamu huanza mimba inapotungwa. Katika Neno lake, Biblia, Mungu huzungumza tena na tena kuhusu mtoto ambaye hajazaliwa kuwa mtu halisi. Fikiria mifano kadhaa inayoonyesha kwamba Mungu hatofautishi kati ya uhai wa mtoto aliye katika tumbo la uzazi na yule ambaye amezaliwa.

  •   Mfalme Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kumwambia Mungu hivi: “Macho yako hata yaliniona nikiwa kiinitete.” (Zaburi 139:16) Mungu alimwona Daudi kuwa mtu hata kabla hajazaliwa.

  •   Isitoshe, Mungu alijua kwamba angemtumia nabii Yeremia kutimiza kusudi muhimu hata kabla Yeremia hajazaliwa. Mungu alimwambia hivi: “Kabla sijakuumba tumboni nilikujua, na kabla hujazaliwa nilikutakasa. Nilikufanya uwe nabii kwa mataifa.”—Yeremia 1:5.

  •   Luka, mwandikaji wa Biblia aliyekuwa daktari, alitumia neno lilelile la Kigiriki kumfafanua mtoto ambaye hajazaliwa na yule ambaye tayari amezaliwa.—Luka 1:41; 2:12, 16.

 Je, Mungu atamsamehe mtu ambaye alitoa mimba?

 Wale ambao wametoa mimba wanaweza kupata msamaha wa Mungu. Ikiwa sasa wanakubali maoni ya Mungu kuhusu uhai, hawahitaji kulemewa na hisia za hatia. “Yehova ni mwenye rehema na mwenye huruma . . . Kama mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali sana na sisi.” b (Zaburi 103:8-12) Yehova atawasamehe wote ambao wanatubu kikweli dhambi walizofanya zamani, kutia ndani kutoa mimba.—Zaburi 86:5.

 Je, ni vibaya kutoa mimba ikiwa uhai wa mama au mtoto uko hatarini?

 Kutokana na kile ambacho Biblia inasema kuhusu uhai wa mtoto ambaye hajazaliwa, isingekuwa sawa kwa mtu kutoa mimba kwa sababu kuna uwezekano wa kuhatarisha afya ya mama au mtoto.

 Lakini namna gani katika hali isiyo ya kawaida wakati wa kujifungua dharura inapolazimisha uamuzi ufanywe kati ya kuokoa uhai wa mama au wa mtoto? Katika kisa hicho, wote wanaohusika watalazimika kufanya uamuzi wao wenyewe kuhusu ni uhai gani watakaojaribu kuokoa.

a Tafsiri fulani zinajaribu kuifanya ionekane kana kwamba katika sheria hii kwa Waisraeli, jambo kuu lilikuwa kilichompata mama, si kijusi. Hata hivyo, maandishi ya Kiebrania yanarejelea kifo kwa ama mama ama mtoto.

b Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.