Hamia kwenye habari

Ni kwa Njia Gani Dhabihu ya Yesu Ilikuwa ‘Fidia kwa Ajili ya Wengi’?

Ni kwa Njia Gani Dhabihu ya Yesu Ilikuwa ‘Fidia kwa Ajili ya Wengi’?

Jibu la Biblia

 Dhabihu ya Yesu ndiyo njia ambayo Mungu anatumia kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Biblia inaitaja damu ya Yesu iliyomwagwa kuwa bei ya fidia. (Waefeso 1:7; 1 Petro 1:18, 19) Hivyo, Yesu alisema kwamba alikuja “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.”​—Mathayo 20:28.

Kwa nini ‘fidia kwa ajili ya wengi’ ilihitajika?

 Mwanamume wa kwanza, Adamu, aliumbwa akiwa mkamilifu, au bila dhambi. Alikuwa na taraja la kuishi milele lakini alipoteza uwezo huo kwa kuamua kumwasi Mungu. (Mwanzo 3:17-19) Alipopata watoto, aliwapitishia dhambi. (Waroma 5:12) Kwa sababu hiyo, Biblia inaonyesha kwamba Adamu ‘alijiuza’ pamoja na watoto wake katika utumwa wa dhambi na kifo. (Waroma 7:14) Kwa kuwa hawakuwa wakamilifu, hakuna yeyote kati yao ambaye angeweza kununua kile ambacho Adamu alipoteza.​—Zaburi 49:7, 8.

 Mungu aliwahurumia wazao wa Adamu kwa sababu ya hali yao isiyo na tumaini. (Yohana 3:16) Hata hivyo, kiwango cha Mungu cha haki kilidai kwamba asipuuze au kuachilia dhambi zao bila msingi hususa. (Zaburi 89:14; Waroma 3:23-26) Mungu anawapenda wanadamu, kwa hiyo aliandaa msingi wa kisheria ili kuwasamehe na kuwaondolea dhambi. (Waroma 5:6-8) Fidia ndiyo iliyokuwa msingi huo wa kisheria.

Fidia inahusisha mambo gani?

 Katika Biblia, neno “fidia” linahusisha mambo matatu:

  1.   Ni malipo.​—Hesabu 3:46, 47.

  2.   Inaandaa kuachiliwa huru, au kukomboa.​—Kutoka 21:30.

  3.   Inalingana na thamani ya kitu kilichoharibiwa. a

 Fikiria jinsi mambo hayo matatu yanavyohusiana na dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.

  1.   Malipo. Biblia inasema kwamba Wakristo ‘walinunuliwa kwa bei.’ (1 Wakorintho 6:20; 7:23) Bei hiyo ni damu ya Yesu, ambayo ‘alimnunulia Mungu watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.’​—Ufunuo 5:8, 9.

  2.   Kuachilia huru. Dhabihu ya Yesu inaandaa ‘kuachiliwa huru kutoka kwa dhambi kupitia fidia.’​—1 Wakorintho 1:30; Wakolosai 1:14; Waebrania 9:15.

  3.   Kulingana. Dhabihu ya Yesu inalingana kabisa na kile ambacho Adamu alipoteza​—uhai mkamilifu wa kibinadamu. (1 Wakorintho 15:21, 22, 45, 46) Biblia inasema: “Kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja [Adamu] wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja [Yesu Kristo] wengi watafanywa kuwa waadilifu.” (Waroma 5:19) Hilo linatusaidia kuelewa jinsi kifo cha mtu mmoja kinavyoweza kulipa fidia ya watenda-dhambi wengi. Kwa kweli, dhabihu ya Yesu ni “fidia inayolingana kwa ajili ya wote” wanaochukua hatua zinazohitajika ili kufaidika kutokana nayo.​—1 Timotheo 2:5, 6.

a Katika Biblia, maneno ya awali yaliyotafsiriwa “fidia” yanatoa wazo la bei, au kitu chenye thamani, kinacholipwa. Kwa mfano, kitenzi cha Kiebrania ka·pharʹ kimsingi kinamaanisha “funiko.” (Mwanzo 6:14) Kwa kawaida kinamaanisha kufunika dhambi. (Zaburi 65:3) Nomino inayopatana na neno hilo koʹpher inawakilisha bei iliyolipwa ili kutimiza tendo hilo la kufunika, au kukomboa. (Kutoka 21:30) Vivyo hivyo, neno la Kigiriki lyʹtron, ambalo kawaida hutafsiriwa kuwa “fidia,” pia, linaweza kuwa “bei ya ukombozi.” (Matthew 20:28; The New Testament in Modern Speech, ya R. F. Weymouth) Waandikaji wa Kigiriki walitumia neno hilo kumaanisha malipo yanayotolewa kumkomboa mtu aliyetekwa nyara vitani au kumwachilia huru mtumwa.