Hamia kwenye habari

Dhambi Ni Nini?

Dhambi Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Dhambi ni tendo, hisia, au wazo lolote linalopingana na viwango vya Mungu. Inatia ndani kuvunja sheria za Mungu kwa kutenda mabaya, au ukosefu wa uadilifu, kwa maoni ya Mungu. (1 Yohana 3:4; 5:​17) Biblia pia inaeleza kuhusu dhambi ya kutofanya lililo sawa ingawa mtu anajua alipaswa kulifanya.​—Yakobo 4:​17.

 Katika lugha za awali za Biblia, neno dhambi linamaanisha, “kukosa shabaha.” Kwa mfano, askari fulani katika Israeli la kale walikuwa na ustadi wa kutupa mawe kwa kombeo “bila kukosea.” Maneno hayo yanapotafsiriwa kihalisi yanamaanisha “bila kufanya dhambi.” (Waamuzi 20:16) Hivyo, kufanya dhambi ni kukosa shabaha ya viwango vikamilifu vya Mungu.

 Kwa kuwa Mungu ndiye Muumba, ana haki ya kuwawekea wanadamu viwango. (Ufunuo 4:​11) Tunawajibika kwake kwa matendo yetu.​—Waroma 14:12.

Je, inawezekana kuepuka kabisa kutenda dhambi?

 Hapana. Biblia inasema kwamba “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23; 1 Wafalme 8:46; Mhubiri 7:20; 1 Yohana 1:8) Kwa nini?

 Mwanzoni, wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, hawakuwa na dhambi. Sababu ni kwamba waliumbwa wakiwa wakamilifu, kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:​27) Hata hivyo, walipoteza ukamilifu wao walipomwasi Mungu. (Mwanzo 3:​5, 6, 17-​19) Walipozaa watoto, waliwapitishia dhambi na kutokamilika. (Waroma 5:​12) Mfalme Daudi wa Israeli alisema, “nilizaliwa kwa maumivu nikiwa na kosa.”​—Zaburi 51:5.

Je, dhambi fulani ni mbaya zaidi kuliko nyingine?

 Ndiyo. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba watu wa Sodoma walikuwa “wabaya” nao walikuwa wakitenda dhambi “nzito sana.” (Mwanzo 13:13; 18:20) Fikiria mambo matatu yanayoamua uzito wa dhambi.

  1.   Ubaya. Biblia inatuonya tuepuke dhambi nzito kama vile uasherati, kuabudu sanamu, wizi, ulevi, unyang’anyi, uuaji, na kuwasiliana na pepo. (1 Wakorintho 6:​9-​11; Ufunuo 21:8) Biblia inatofautisha dhambi hizo na dhambi zinazofanywa bila kukusudia, kama vile, maneno au matendo yanayowaumiza wengine. (Methali 12:18; Waefeso 4:​31, 32) Hata hivyo, Biblia inatusihi tusipuuze dhambi yoyote, wa kuwa zinaweza kutufanya tutende dhambi nzito zaidi.​—Mathayo 5:​27, 28.

  2.   Nia. Dhambi nyingine hufanywa kwa kuwa mtu hajui matakwa ya Mungu. (Matendo 17:30; 1 Timotheo 1:​13) Ingawa Biblia haipuuzi dhambi hizo, inazitofautisha na kuvunja sheria ya Mungu kimakusudi. (Hesabu 15:30, 31) Dhambi zinazofanywa kimakusudi zinatokana na ‘moyo mbaya.’​—Yeremia 16:12.

  3.   Kurudia dhambi. Biblia inatofautisha kati ya kufanya dhambi mara moja na zoea la kufanya dhambi kwa muda mrefu. (1 Yohana 3:​4-8) Wale walio na ‘zoea la kutenda dhambi kimakusudi,’ hata baada ya kujifunza jinsi ya kufanya jambo linalofaa, hupokea hukumu kali kutoka kwa Mungu.​—Waebrania 10:26, 27.

 Wale walio na hatia ya kutenda dhambi nzito wanaweza kulemewa na uzito wa makosa yao. Kwa mfano, Mfalme Daudi aliandika hivi: “Makosa yangu yamepita juu ya kichwa changu; kama mzigo mzito, ni mazito sana kwangu.” (Zaburi 38:4) Hata hivyo, Biblia inatoa tumaini hili: “Mtu mwovu aiache njia yake, na mtu mwenye madhara ayaache mawazo yake; naye arudi kwa Yehova, ambaye atamwonyesha rehema, na kwa Mungu wetu, kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.”​—Isaya 55:7.