Hamia kwenye habari

Dhambi ya Kwanza Ilikuwa Nini?

Dhambi ya Kwanza Ilikuwa Nini?

Jibu la Biblia

 Adamu na Hawa ndio waliokuwa wanadamu wa kwanza kutenda dhambi. Walipokosa kumtii Mungu kwa kula kutokana na “mti wa ujuzi wa mema na mabaya,” walifanya kosa ambalo watu wengi huliita dhambi ya kwanza. a (Mwanzo 2:16, 17; 3:6; Waroma 5:19) Adamu na Hawa hawakupaswa kula matunda ya mti huo kwa sababu uliwakilisha mamlaka ya Mungu, au haki ya kuwaamulia wanadamu yaliyo sawa na yasiyo sawa. Kwa kula kutokana na mti huo, waliamua kwamba wao ndio watakaojiamulia yaliyo sawa na yasiyo sawa. Kufanya hivyo kulionyesha kwamba walikuwa wakikataa mamlaka ya Mungu.

 “Dhambi ya kwanza” iliwaathirije Adamu na Hawa?

 Kwa sababu walitenda dhambi, hatimaye Adamu na Hawa walizeeka na kufa. Waliharibu uhusiano wao pamoja na Mungu na kupoteza uwezekano na kuishi milele wakiwa na afya kamilifu.—Mwanzo 3:19.

 “Dhambi ya kwanza” inatuathirije?

 Wazao wote wa Adamu na Hawa walirithi dhambi. Hilo linaweza kulinganishwa na jinsi wazazi wanavyowapitishia watoto wao kasoro fulani za chembe za urithi. (Waroma 5:12) Hivyo, wanadamu wote wamezaliwa “katika dhambi.” b Hilo linamaanisha kwamba sisi sote tunazaliwa tukiwa wasio wakamilifu na tuna mwelekeo wa kufanya makosa.—Zaburi 51:5; Waefeso 2:3.

 Kwa kuwa tumerithi dhambi, au kutokamilika, tunakuwa wagonjwa, tunazeeka, na kufa. (Waroma 6:23) Pia, tunateseka kwa sababu ya makosa yetu wenyewe na makosa ya wengine.—Mhubiri 8:9; Yakobo 3:2.

 Je, tunaweza kukombolewa kutokana na madhara ya “dhambi ya kwanza”?

 Ndiyo. Biblia inasema kwamba Yesu alikufa na kuwa “dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yohana 4:10) Dhabihu ya Yesu inaweza kutuokoa dhidi ya matokeo ya dhambi tuliyorithi na kuturuhusu kupata kile ambacho Adamu na Hawa walipoteza—uwezekano wa kuishi milele tukiwa na afya kamilifu.—Yohana 3:16. c

 Maoni yasiyo sahihi kuhusu “dhambi ya kwanza”

 Maoni yasiyo sahihi: Dhambi ya kwanza inatutenga na Mungu milele.

 Ukweli: Mungu hatulaumu kwa kosa ambalo Adamu na Hawa walifanya. Anaelewa kwamba sisi si wakamilifu, na hatarajii mengi kutoka kwetu zaidi ya kile ambacho anajua tunaweza kutimiza. (Zaburi 103:14) Ijapokuwa tunapata matokeo mabaya ya dhambi tuliyorithi, tuna nafasi na pendeleo la kuwa na urafiki wa karibu na Yehova.—Methali 3:32.

 Maoni yasiyo sahihi: Ubatizo unamweka mtu huru kutokana na dhambi ya kwanza, hivyo watoto wachanga wanahitaji kubatizwa.

 Ukweli: Ijapokuwa ubatizo ni hatua muhimu ya kupata uzima, imani katika dhabihu ya Yesu tu ndiyo inayoweza kumtakasa mtu kutokana na dhambi. (1 Petro 3:21; 1 Yohana 1:7) Kwa kuwa lazima mtu awe na ujuzi ili awe na imani inayozungumziwa katika Biblia, haiwezekani kwa watoto kuwa na imani. Hivyo basi Biblia haikubaliani na ubatizo wa watoto wadogo. Ukweli huu ulionekana wazi kati ya Wakristo wa karne ya kwanza. Hawakubatiza watoto wachanga, bali walibatiza waamini—“wanaume na pia wanawake” waliokuwa na imani katika Neno la Mungu.—Matendo 2:41; 8:12.

 Maoni yasiyo sahihi: Mungu aliwalaani wanawake kwa sababu Hawa alikuwa wa kwanza kula tunda lililokatazwa.

 Ukweli: Badala ya kuwalaani wanawake, Mungu alimlaani “yule nyoka wa zamani, anayeitwa Ibilisi na Shetani,” aliyemshawishi Hawa kufanya dhambi. (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:14) Zaidi ya hilo, Mungu alionyesha kwamba Adamu ndiye aliyewajibika zaidi kutokana na dhambi ya kwanza na si mke wake.—Waroma 5:12.

 Kwa nini Mungu alisema kwamba Adamu angemtawala mke wake? (Mwanzo 3:16) Aliposema maneno hayo, Mungu hakuwa akitetea tabia hiyo. Alikuwa tu akitabiri matokeo mabaya ya dhambi. Mungu anatarajia mwanamume ampende na kumheshimu mke wake na kuwaonyesha heshima kubwa wanawake kwa ujumla.—Waefeso 5:25, 1 Petro 3:7.

 Maoni yasiyo sahihi: Dhambi ya kwanza ilikuwa mahusiano ya kingono.

 Ukweli: Haiwezekani kwamba dhambi ya kwanza ilikuwa mahusiano ya kingono kwa sababu ya sababu zifuatazo:

  •   Mungu alipomwamuru Adamu asile kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya, Adamu alikuwa peke yake, hakuwa na mke.—Mwanzo 2:17, 18.

  •   Mungu aliwaamuru Adamu na Hawa hivi, “zaeni, muwe wengi”—hilo linamaanisha walipaswa kupata watoto. (Mwanzo 1:28) Ungekuwa ukatili ikiwa Mungu angewaadhibu kwa jambo ambalo yeye mwenyewe aliwaamuru kufanya.

  •   Adamu na Hawa hawakutenda dhambi wakati uleule—Hawa ndiye aliyeanza kisha mume wake akatenda dhambi baadaye.—Mwanzo 3:6.

  •   Biblia haikatazi mahusiano ya kingono kati ya mume na mke.—Methali 5:18, 19; 1 Wakorintho 7:3.

a Maneno “dhambi ya kwanza” hayapatikani ndani ya Biblia. Ukweli ni kwamba dhambi ya kwanza kabisa kurekodiwa katika Biblia ni maneno ya Shetani ya udanganyifu na uwongo aliomwambia Hawa.—Mwanzo 3:4, 5; Yohana 8:44.

b Katika Biblia, neno “dhambi” halirejelei tu matendo mabaya, bali pia hali yetu ya kutokamilika na dhambi ambayo tumerithi.

c Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu dhabihu ya Yesu na jinsi tunavyoweza kunufaika nayo, ona makala yenye kichwa, “Yesu Huokoa—Jinsi gani?