Hamia kwenye habari

Je, Biblia Inafundisha Kwamba Dunia Ni Tambarare?

Je, Biblia Inafundisha Kwamba Dunia Ni Tambarare?

Jibu la Biblia

 Hapana, Biblia haifundishi kwamba dunia ni tambarare. a Biblia si kitabu cha kisayansi. Wakati huohuo, hakuna kitu katika Biblia kinachopingana na sayansi iliyothibitishwa. Mambo ambayo Biblia inasema “yanategemeka sikuzote, sasa na milele.”​—Zaburi 111:8.

 Biblia inamaanisha nini inaposema “pembe nne za dunia”?

 Maneno “pembe nne za dunia” na “miisho ya dunia” yanayopatikana katika Biblia hayapaswi kueleweka kihalisi, kana kwamba dunia ni ya mraba au ina miisho. (Isaya 11:12; Ayubu 37:3) Badala yake, hiyo ni misemo inayorejelea dunia yote. Biblia inatumia pande zote nne za dira kwa njia hiyohiyo.​—Luka 13:29.

 Inaonekana kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kona” au “miisho” ni msemo unaotegemea neno “mabawa.” Kulingana na The International Standard Bible Encyclopedia, “kwa sababu bawa la ndege linatumiwa kufunika makinda yake, [neno hilo la Kiebrania] linatumiwa kumaanisha miisho ya chochote kilichonyooshwa.” Kitabu hichohicho kinaongezea kwamba kwenye Ayubu 37:3 na Isaya 11:12, “neno hilo linamaanisha pwani, mipaka, au miisho ya ardhi duniani.” b

 Vipi kuhusu kishawishi ambacho Ibilisi alimletea Yesu?

 Ili kumjaribu Yesu, ‘Ibilisi alimpeleka Yesu kwenye mlima mrefu sana, akamwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.’ (Mathayo 4:8) Watu fulani wanadai kwamba simulizi hili la Biblia linafundisha kwamba ulimwengu mzima ungeweza kuonekana kutoka kwenye sehemu moja tambarare duniani. Hata hivyo, katika simulizi hili inaonekana kwamba huo “mlima mrefu sana” ni msemo na si sehemu fulani halisi. Fikiria kwa nini mkataa huo unapatana na akili.

  •   Hakuna mlima halisi duniani ambapo falme zote za dunia zinaweza kuonekana kutoka juu yake.

  •   Ibilisi alimwonyesha Yesu si falme zote tu bali pia “utukufu wazo.” Mambo hususa kama hayo hayawezi kuonekana kutoka mbali, kwa hiyo, inaonekana kwamba Ibilisi alitumia aina fulani ya maono kumwonyesha Yesu vitu hivyo. Inaweza kulinganishwa na jinsi mtu anavyotumia projekta na skrini kumwonyesha mwenzake picha za sehemu mbalimbali duniani.

  •   Simulizi linalopatana na hilo kwenye Luka 4:5 linasema kwamba Ibilisi alimwonyesha Yesu “mara moja falme zote za dunia inayokaliwa.” Jambo hilo haliwezekani kwa macho ya kawaida ya mwanadamu. Hilo linadokeza kwamba Ibilisi alimletea Yesu kishawishi hicho kwa njia nyingine tofauti na macho halisi ya kibinadamu.

a Biblia inamtaja Mungu kuwa “Yule anayekaa juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22) Baadhi ya vitabu vya marejeo vinakubali kwamba kuna uwezekano kwamba neno “duara” linalotajwa hapa linaweza kumaanisha tufe, ingawa si wasomi wote wanaokubaliana kuhusu jambo hilo. Vyovyote vile, Biblia haiungi mkono wazo la kwamba dunia ni tambarare.

b Toleo Lililorekebishwa, Buku la 2, ukurasa wa 4.