Hamia kwenye habari

Kwa Nini Wayahudi Wengi Waliuawa? Kwa Nini Mungu Hakuzuia?

Kwa Nini Wayahudi Wengi Waliuawa? Kwa Nini Mungu Hakuzuia?

 Watu wengi ambao wanauliza maswali hayo wamepata hasara kubwa sana na si kwamba wanatafuta majibu tu bali pia faraja. Wengine wanaona Mauaji Makubwa ya Wayahudi kuwa kilele cha uovu wa mwanadamu, hivyo inakuwa vigumu kwao kumwamini Mungu.

Maoni yasiyofaa kuhusu Mungu na Kuuawa kwa Wayahudi

 Uwongo: Ni vibaya kuuliza kwa nini Mungu aliruhusu Wayahudi wengi wauawe.

 Jambo la hakika: Watu wenye imani yenye nguvu wameuliza kwa nini Mungu anaruhusu uovu. Kwa mfano, nabii Habakuki alimuuliza Mungu hivi: “Kwa nini unaruhusu jeuri, uasi-sheria, uhalifu na ukatili uenee kotekote?” (Habakuki 1:3, Contemporary English Version) Badala ya kumkemea Habakuki, Mungu aliruhusu maswali aliyouliza yarekodiwe kwenye Biblia ili watu wote wayasome.

 Uwongo: Mungu hajali kuhusu kuteseka kwa wanadamu.

 Jambo la hakika: Mungu anachukia uovu na kuteseka kunakosababishwa na uovu. (Methali 6:16-19) Katika siku za Noa, Mungu ‘aliumia moyoni mwake’ kwa sababu ya jeuri iliyokuwa imesambaa duniani. (Mwanzo 6:5, 6) Bila shaka, Mungu aliumia sana Wayahudi wengi walipouawa.—Malaki 3:6.

 Uwongo: Kuuawa kwa Wayahudi kulikuwa adhabu kutoka kwa Mungu.

 Jambo la hakika: Mungu aliruhusu Waroma waliharibu jiji la Yerusalemu katika karne ya kwanza. (Mathayo 23:37–24:2) Hata hivyo, tangu wakati huo Mungu hajachagua kabila au jamii yoyote ya watu ili kuionyesha upendeleo wa pekee au kuiadhibu. Kwa maoni ya Mungu, “hakuna tofauti kati ya Wayahudi na wasio Wayahudi.”—Waroma 10:12, Biblia Habari Njema.

 Uwongo: Ikiwa kungekuwa na Mungu mwenye upendo na nguvu zote, basi angezuia Wayahudi wasiuawe.

 Jambo la hakika: Ingawa Mungu hasababishi kamwe kuteseka, wakati fulani anaruhusu kuteseka kwa muda mfupi.—Yakobo 1:13; 5:11.

Kwa nini Mungu aliruhusu Wayahudi wauawe?

 Mungu aliruhusu Wayahudi wauawe kwa sababu ileile ambayo imemfanya aruhusu kuteseka kwa wanadamu wote: ili asuluhishe suala muhimu lililozushwa miaka miaka mingi iliyopita. Biblia inaonyesha wazi kwamba anayetawala ulimwengu huu sasa ni Ibilisi na wala si Mungu. (Luka 4:1, 2, 6; Yohana 12:31) Mambo mawili ya hakika kutoka katika Biblia yanaweza kusaidia kufafanua kwa nini Mungu aliruhusu Wayahudi wengi wauawe.

  1.   Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua. Mungu aliwaambia wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, mambo aliyotarajia kutoka kwao, lakini hakuwalazimisha wamtii. Walichagua kujiamulia wenyewe kuhusu jema na baya, na uchaguzi wao mbaya—na uchaguzi mwingine unaofanana na huo ambao umefanywa na watu katika historia yote ya mwanadamu—umewasababishia wanadamu matokeo mabaya sana. (Mwanzo 2:17; 3:6; Waroma 5:12) Ni kama vile kitabu Statement of Principles of Conservative Judaism kinavyosema: “Mateso mengi yaliyo ulimwenguni ni matokeo ya moja kwa moja ya matumizi yetu mabaya ya zawadi ya uhuru wa kuchagua tuliyopewa.” Badala ya kutunyang’anya uhuru wetu wa kuchagua, Mungu amewapa wanadamu muda ili wajaribu kufanya shughuli zao kwa uhuru bila yeye mwenyewe kuingilia kati.

  2.   Mungu anaweza naye ataondoa madhara yote yaliyosababishwa na kuuawa kwa Wayahudi. Mungu anaahidi kuwarudisha tena kwenye uhai mamilioni ya watu ambao wamekufa, kutia ndani wale waliouawa wakati wa maangamizi ya Wayahudi. Pia ataondoa kabisa uchungu unaosababishwa na kumbukumbu mbaya kwa wale walioponea chupuchupu kuuawa wakati wa maangamizi hayo. (Isaya 65:17; Matendo 24:15) Upendo wa Mungu kwa wanadamu unatuhakikishia kwamba atatimiza ahadi hizo.—Yohana 3:16.

 Watu wengi waliookoka kuuawa kwa Wayahudi waliweza kuendelea kuwa na imani na kupata kusudi la maisha kwa kuelewa ni kwa nini Mungu ameruhusu uovu na jinsi ambavyo amekusudia kuondoa madhara yote ya uovu.