Hamia kwenye habari

Unaweza Kufanya Nini Ili Umjue Mungu Kibinafsi?

Unaweza Kufanya Nini Ili Umjue Mungu Kibinafsi?

Jibu la Biblia

 Unaweza kumjua Mungu kibinafsi kwa kujifunza kumhusu na kuchukua hatua za kumpendeza. Kisha Mungu ‘atakukaribia wewe.’ (Yakobo 4:8) Biblia inatuhakikishia kwamba “hayuko mbali na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

 Hatua za kumjua Mungu

 Soma Biblia

  •  Biblia inasema nini: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu.”—2 Timotheo 3:16.

  •  Maana: Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia. Aliingiza mawazo yake katika akili za waandikaji wa Biblia. Kupitia kitabu chake cha pekee, Mungu ametufunulia mapenzi yake. Pia, amefunua sehemu mbalimbali za utu wake, kutia ndani upendo, haki, na rehema yake.—Kutoka 34:6; Kumbukumbu la Torati 32:4.

  •  Unachoweza kufanya: Soma Biblia kila siku. (Yoshua 1:8) Tafakari unayosoma kwa kujiuliza: ‘Jambo hili linanifundisha nini kumhusu Mungu?’—Zaburi 77:12.

 Kwa mfano, soma Yeremia 29:11, kisha ujiulize: ‘Mungu ananitakia nini—amani au msiba? Je, yeye ni Mungu mwenye kinyongo, au anataka niwe na wakati ujao mzuri?’

 Chunguza uumbaji

  •  Biblia inasema nini: “Sifa [za Mungu] zisizoonekana, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kupitia vitu vilivyoumbwa.”—Waroma 1:20.

  •  Maana: Uumbaji wa Mungu unaoonekana unafunua sehemu mbalimbali za utu wake, kama vile sanaa inavyoweza kufunua mambo mengi kuhusu msanii au jinsi mashine tata inavyoweza kufunua mengi kuhusu mbuni wake. Kwa mfano, uwezo na utata wa ubongo wa mwanadamu hufunua hekima ya Mungu, na nishati iliyodhibitiwa katika jua na nyota nyingine huonyesha nguvu zake.—Zaburi 104:24; Isaya 40:26.

  •  Unachoweza kufanya: Tenga wakati wa kuchunguza na kujifunza mengi kuhusu uumbaji. Unapofanya hivyo, jiulize: ‘Miundo yenye kustaajabisha inayoonekana katika uumbaji inafunua nini kumhusu Mungu?’ a Bila shaka, kuna mambo mengi ambayo uumbaji hauwezi kutufunza kumhusu Muumba wetu. Ndiyo sababu ametupa Biblia.

 Tumia jina la Mungu

  •  Biblia inasema nini: “Nitamlinda kwa sababu analijua jina langu. Ataniita, nami nitamjibu.”—Zaburi 91:14, 15.

  •  Maana: Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, anawakazia uangalifu wa pekee wale wanaolijua jina lake na kulitumia kwa heshima. b (Zaburi 83:18; Malaki 3:16) Kwa kutujulisha jina lake, Mungu anajitambulisha kwetu. Anasema hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu.”—Isaya 42:8.

  •  Unachoweza kufanya: Tumia jina la Yehova unapozungumza kumhusu.

 Zungumza na Yehova katika sala

  •  Biblia inasema nini: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.”—Zaburi 145:18.

  •  Maana: Yehova anawakaribia wale wanaosali kwake wakiwa na imani. Sala ni sehemu ya ibada inayoonyesha kwamba tunamheshimu Mungu.

  •  Unachoweza kufanya: Sali kwa Mungu mara nyingi. (1 Wathesalonike 5:17) Mweleze mahangaiko yako na jinsi unavyohisi.—Zaburi 62:8. c

 Sitawisha imani katika Mungu

  •  Biblia inasema nini: “Bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema.”—Waebrania 11:6.

  •  Maana: Ili kumkaribia Mungu, lazima tumwamini. Katika Biblia, kuwa na imani kunamaanisha mengi zaidi ya kuamini kwamba Mungu yupo. Kunamaanisha pia kumtumaini kabisa, kutia ndani ahadi na viwango vyake. Ili uwe na uhusiano mzuri na mtu mwingine, lazima umtumaini.

  •  Unachoweza kufanya: Imani ya kweli inategemea ujuzi. (Waroma 10:17) Kwa hiyo, jifunze Biblia na ujithibitishie mwenyewe kwamba unaweza kumtumaini Mungu na mashauri yake. Mashahidi wa Yehova watafurahi kujifunza Biblia pamoja nawe. d

 Fanya mambo yanayompendeza Mungu

  •  Biblia inasema nini: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.”—1 Yohana 5:3.

  •  Maana: Yehova yuko karibu na wale wanaoonyesha kwamba wanampenda kwa kujitahidi kutii amri zake.

  •  Unachoweza kufanya: Unapojifunza Biblia, tambua mambo ambayo Mungu anapenda na anayochukia. Jiulize, ‘Ninaweza kufanya mabadiliko gani ili nimpendeze Muumba wangu?’—1 Wathesalonike 4:1.

 Tumia mashauri ya Mungu, ujionee upendo wake

  •  Biblia inasema nini: “Onjeni mwone kwamba Yehova ni mwema.”—Zaburi 34:8.

  •  Maana: Mungu anakualika ujionee jinsi alivyo mwema. Unapojionea upendo na utegemezo wake, utatamani kumkaribia.

  •  Unachoweza kufanya: Unaposoma Biblia, tumia mashauri ya Mungu na ujionee baraka utakazopata. (Isaya 48:17, 18) Pia, chunguza mifano ya watu ambao, kwa msaada wa Mungu, walikabiliana na matatizo, wakaboresha maisha yao na maisha ya familia zao, na kupata furaha ya kweli. e

 Maoni yasiyo sahihi kuhusu kumjua Mungu

 Maoni yasiyo sahihi: Mungu ni mwenye nguvu na ana cheo cha juu sana kwa hiyo hawezi kutukaribia.

 Ukweli: Hata ingawa Mungu ndiye mwenye nguvu na cheo cha juu zaidi katika ulimwengu wote, anatualika tumkaribie. Biblia ina mifano mingi ya wanaume na wanawake ambao walikuwa rafiki zake wa karibu.—Matendo 13:22; Yakobo 2:23.

 Maoni yasiyo sahihi: Hatuwezi kumjua Mungu kwa sababu yeye ni fumbo.

 Ukweli: Ni vigumu kuelewa mambo fulani kumhusu Mungu, kama vile, ana mwili wa Roho. Hata hivyo, tunaweza kumjua Mungu. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba tunahitaji kumjua ili tupate uzima wa milele. (Yohana 17:3) Biblia inatumia maneno tunayoweza kuelewa inapozungumza kumhusu Muumba wetu, na inatufunulia utu wake, kusudi lake kwa wanadamu na dunia, na viwango vyake. (Isaya 45:18, 19; 1 Timotheo 2:4) Na kama ilivyotajwa, Biblia inatufunulia jina la Mungu. (Zaburi 83:18) Hivyo, tunaweza kumjua Mungu na pia kumkaribia.—Yakobo 4:8.

a Ili uone mifano ya jinsi hekima ya Mungu inavyofunuliwa kupitia uumbaji, ona mfululizo wa makala wenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?

b Watu wengi wanaelewa kwamba jina Yehova linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Kwa kutufunulia jina lake, Mungu anatuambia: ‘Nitasababisha mapenzi na kusudi langu litimie. Sikuzote nitatimiza neno langu.’

c Ona makala yenye kichwa “Kwa Nini Nisali? Je, Mungu Atanijibu?

d Ili upate habari zaidi, tazama video yenye kichwa Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia?

e Ona mfululizo wa makala “Biblia Inabadili Maisha.”