Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Methali 3:5, 6​—“Usizitegemee Akili Zako Mwenyewe”

Methali 3:5, 6​—“Usizitegemee Akili Zako Mwenyewe”

 “Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote, wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Katika njia zako zote mtambue yeye, naye atavinyoosha vijia vyako.”—Methali 3:5, 6, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe. Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6, Union Version.

Maana ya Methali 3:5 6

 Badala ya kujifanyia maamuzi yoyote muhimu, tunapaswa kutafuta mwongozo wa Yehova a Mungu.

 “Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote.” Tunaonyesha kwamba tunamtumaini Mungu tunapofanya mambo kama yeye anavyoelekeza. Tunapaswa kumtumaini Mungu kikamili, kwa moyo wetu wote. Katika Biblia, mara nyingi moyo hurejelea mtu wa ndani, na hilo linahusisha hisia za mtu, mambo yanayomchochea, fikira, na mtazamo. Hivyo, kumtumaini Mungu kwa moyo wetu kunahusisha mengi zaidi ya hisia zetu. Ni uamuzi tunaofanya kwa sababu tumesadikishwa kabisa kwamba Muumba wetu anajua ni nini kinachotufaa zaidi.—Waroma 12:1.

 “Usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” Tunapaswa kumtumaini Mungu kwa sababu hatuwezi kutegemea maoni yetu yasiyokamilika. Ikiwa tutajitumaini kabisa au kuruhusu hisia zetu ziamue mambo tutakayofanya, tunaweza kufanya maamuzi ambayo mwanzoni huenda yanaonekana kuwa mazuri lakini mwishowe yakaleta matokeo mabaya. (Methali 14:12; Yeremia 17:9) Hekima ya Mungu ni bora zaidi kuliko yetu. (Isaya 55:8, 9) Tutafanikiwa sana maishani ikiwa tutaongozwa na Mungu.—Zaburi 1:1-3; Methali 2:6-9; 16:20.

 “Katika njia zako zote mtambue yeye.” Tunapaswa kutafuta maoni ya Mungu katika kila jambo muhimu maishani mwetu na kila uamuzi muhimu tunaofanya. Tunafanya hivyo kwa kusali kwake tukimwomba atupatie mwongozo na kwa kufuata anachosema katika Neno lake, Biblia.—Zaburi 25:4; 2 Timotheo 3:16, 17.

 “Atavinyoosha vijia vyako.” Mungu ananyoosha njia yetu kwa kutusaidia kuishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu. (Methali 11:5) Hivyo, tunaepuka matatizo yoyote yasiyo ya lazima na kuwa na maisha yenye furaha.—Zaburi 19:7, 8; Isaya 48:17, 18.

Muktadha wa Methali 3:5, 6

 Kitabu cha Biblia cha Methali kina kanuni za msingi zinazosaidia kuwa na maisha yenye furaha na mafanikio mbele za Mungu. Sura tisa za kwanza zimeandikwa kama ushauri wa baba kwa mtoto wake mpendwa. Sura ya 3 inataja manufaa wanayopata wale wanaothamini na kutumia hekima ya Muumba wetu.—Methali 3:13-26.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.