Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NJIA YA MAISHA INAYOLETA FURAHA

Kusamehe

Kusamehe

“NILIPOKUWA MDOGO, ILIKUWA NI KAWAIDA KUSIKIA MATUSI NA MAKELELE.” Hayo ni maneno ya mwanamke anayeitwa Patricia. Anaendelea kusema: “Sikujifunza kuwasamehe wengine. Hata baada ya kuwa mtu mzima, kuna nyakati ambazo kwa siku kadhaa nilifikiria kuhusu kosa nililofanyiwa na hata kukosa usingizi.” Bila shaka maisha yaliyojaa hasira na chuki humzuia mtu kuwa na furaha na huathiri afya pia. Utafiti unaonyesha kwamba huenda watu wasio na sifa ya kusamehe . . .

  • Wakaruhusu hasira na uchungu viharibu mahusiano na hivyo kufanya wajitenge na kuwa wapweke

  • Wakawa wenye kukasirika haraka, rahisi kuwa na wasiwasi, au hata kushuka moyo

  • Wakakazia sana kosa hivi kwamba wanashindwa kufurahia maisha

  • Wakasumbuliwa na hisia ya kwamba wanafanya kinyume na jinsi ambavyo Mungu anataka

  • Wakapata mkazo na kuwa na uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa, kutia ndani shinikizo la damu, ugonjwa wa moyo, na maumivu makali kama vile ya kichwa na mifupa *

KUSAMEHE KUNAMAANISHA NINI? Kusamehe kunamaanisha kuachilia kosa na kuondoa hasira, kinyongo, na mawazo ya kulipiza kisasi. Haimaanishi kuunga mkono kosa, kupuuza uzito wake, au kujifanya kana kwamba halikutendeka. Badala yake, kusamehe ni uamuzi uliofikiriwa kwa makini ambao mtu hufanya akichochewa na upendo, unaoonyesha utayari wake wa kufanya amani na kudumisha uhusiano mzuri na yule aliyemkosea.

Kusamehe wengine huonyesha pia kwamba mtu ana sifa ya uelewaji. Mtu mwenye kusamehe anaelewa kwamba sote hukosea au kutenda dhambi, kwa maneno au matendo. (Waroma 3:23) Kwa kuzingatia wazo hilo, Biblia inasema hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”—Wakolosai 3:13.

Hivyo basi, kusamehe ni sehemu muhimu ya upendo, ambao “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Kulingana na tovuti ya hospitali moja maarufu (Mayo Clinic), kusamehe huchangia . . .

  • Kuboresha mahusiano, na kusaidia kuwa mwenye huruma nyororo na kuelewa vizuri hisia za yule aliyekosea

  • Kuwa na hali nzuri ya kiroho na kiakili

  • Kupunguza wasiwasi, mkazo, na chuki

  • Kupunguza madhara yanayotokana na kushuka moyo

JISAMEHE. Jarida moja (Disability & Rehabilitation) linasema kwamba kujisamehe kunaweza kuwa “jambo gumu zaidi kufanya” ingawa ndilo “jambo muhimu zaidi ili kuwa na afya nzuri” ya akili na mwili. Ni nini kinachoweza kukusaidia ujisamehe?

  • Usitazamie kufanya mambo kwa usahihi kabisa sikuzote, badala yake, kubali kwamba kama ilivyo kwa wanadamu wote, wewe pia utakosea.—Mhubiri 7:20

  • Jifunze kutokana na makosa yako ili upunguze uwezekano wa kuyarudia tena.

  • Uwe na subira; huenda ikachukua muda kushinda udhaifu fulani au mazoea mabaya.—Waefeso 4:23, 24

  • Shirikiana na marafiki ambao watakutia moyo, walio na maoni chanya, na wenye fadhili lakini ambao pia wako tayari kukuambia ukweli unapokosea.—Methali 13:20

  • Unapomkosea mtu, kubali makosa yako na uombe msamaha haraka iwezekanavyo. Unapofanya amani na wengine, utapata amani ya moyo.—Mathayo 5:23, 24

KUTUMIA KANUNI ZA BIBLIA HULETA MATOKEO MAZURI!

Baada ya kujifunza Biblia, Patricia, aliyenukuliwa awali, alijifunza kuwa mwenye kusamehe. Aliandika hivi: “Ninajihisi huru kutokana na hasira iliyokuwa ikiharibu maisha yangu. Siteseki tena na siwafanyi wengine wateseke pia. Kanuni za Biblia zinathibitisha kwamba Mungu anatupenda na anataka tuwe na maisha mazuri.”

Mwanamume anayeitwa Ron anasema: “Nisingeweza kudhibiti mawazo na matendo ya wengine. Lakini ningeweza kudhibiti mawazo na matendo yangu. Ili niwe na amani, nilihitaji kuondoa kinyongo. Niliona amani kuwa tofauti na kinyongo kama kaskazini ilivyo mbali na kusini. Nisingeweza kuwa maeneo yote mawili kwa wakati mmoja. Sasa nina dhamiri safi.”

^ fu. 8 Chanzo: Tovuti ya Mayo Clinic na Johns Hopkins Medicine na jarida Social Psychiatry and Psychiatric Epidemiology.