Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NJIA YA MAISHA INAYOLETA FURAHA

Upendo

Upendo

WANADAMU WANAHITAJI SANA UPENDO. Hakuna ndoa, familia, au urafiki unaoweza kusitawi bila upendo. Hivyo basi, ni wazi kwamba upendo ni muhimu sana ili kuwa na afya nzuri ya akili pamoja na furaha. Hata hivyo, “upendo” unamaanisha nini?

Upendo tunaozungumzia hapa si ule wa kimahaba, ambao bila shaka una umuhimu wake pia. Badala yake, tunazungumzia aina ya upendo wa juu zaidi ambao humchochea mtu kuhangaikia kutoka moyoni hali za wengine, na kuwa tayari hata kutanguliza masilahi yao. Ni upendo unaoongozwa na kanuni za Mungu, lakini ambao unahusisha pia hisia na wororo.

Biblia inafafanua upendo kwa njia nzuri inaposema: “Upendo ni wenye subira na fadhili. Upendo hauna wivu. Haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, . . . hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:4-8.

Upendo wa aina hiyo “haushindwi kamwe” katika maana ya kwamba unadumu milele. Kwa kweli, upendo huu huimarika kadiri muda unavyopita. Na kwa kuwa ni wenye subira, fadhili, na tayari kusamehe, upendo wa aina hii “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Hivyo, mahusiano yanayoongozwa na upendo huu ni yenye furaha na salama, licha ya kutokamilika kwa wale wanaohusika. Kwa mfano, hebu fikiria muungano wa ndoa.

KUUNGANISHWA NA “KIFUNGO KIKAMILIFU CHA MUUNGANO”

Yesu Kristo alifundisha kanuni muhimu sana za ndoa. Kwa mfano, alisema: “‘Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’ . . . Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:5, 6) Andiko hilo linatupatia kanuni mbili muhimu.

“HAO WAWILI WATAKUWA MWILI MMOJA.” Ndoa ndio uhusiano wa karibu zaidi kwa wanadamu, na upendo huwasaidia waume na wake wasitoke nje ya muungano huo na kuwa “mwili mmoja” na mtu mwingine ambaye si mwenzi wao. (1 Wakorintho 6:16; Waebrania 13:4) Kutoka nje ya ndoa kunaweza kufanya wenzi wasiaminiane na hata kuvunja ndoa. Ikiwa familia ina watoto, wanaweza kuathirika sana kihisia, na wakahisi hawapendwi, hawapo salama, au hata wakawa na hasira.

“KILE AMBACHO MUNGU AMEUNGANISHA.” Ndoa pia ni muungano mtakatifu. Wenzi wanaotambua na kuheshimu ukweli huo hujitahidi kuimarisha ndoa yao. Hawatafuti njia za kuvunja ndoa yao matatizo yanapotokea. Upendo wao ni imara na thabiti. Upendo wa aina hiyo “huvumilia mambo yote,” na kuwachochea wenzi watatue matatizo yao ili kudumisha amani na umoja katika ndoa.

Watoto hunufaika sana wanapokuwa na wazazi wanaopendana bila ubinafsi. Binti anayeitwa Jessica anasema hivi: “Baba na mama yangu wanapendana na kuheshimiana kikweli. Ninapomwona mama akimheshimu baba, hasa anaposhughulika na sisi watoto, ninatamani kuwa kama yeye.”

Upendo ndio sifa kuu ya Mungu. Biblia inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Hivyo, haishangazi kwamba Yehova anaitwa pia “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Sisi pia tutakuwa wenye furaha tukijitahidi kuiga sifa za Muumba wetu, hasa upendo. Andiko la Waefeso 5:1, 2 linasema: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.”