Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutimiza Jukumu Lako Ukiwa Mzazi

Kutimiza Jukumu Lako Ukiwa Mzazi

Je, unakumbuka mara ya kwanza kabisa ulipombeba mtoto wako aliyetoka tu kuzaliwa?

Huenda baada ya muda mfupi ulianza kushtuka ulipotambua kwamba mtoto wako atahitaji mwongozo kwa miaka mingi. Upesi ulitambua kwamba ulikuwa na daraka kubwa.

INGAWA majukumu ya mzazi yamekuwa magumu tangu zamani, ni magumu hata zaidi leo. Kwa nini? Kwa sababu hali katika ulimwengu wa leo ni ngumu hata zaidi kuliko zilivyokuwa ulipokuwa mtoto. Baadhi ya matatizo ya kiadili ambayo watoto wanakabili​—kwa mfano, wanapotumia Intaneti—​hayakuwapo makumi ya miaka iliyopita.

Unaweza kumsaidiaje mtoto wako akabiliane na maadili yaliyozorota katika ulimwengu wa leo? Yafuatayo ni mapendekezo matatu.

1 Mjulishe viwango vyako waziwazi.

Kadiri watoto wanavyokua, wao hupata habari nyingi sana zisizo sahihi kuhusu maadili—habari fulani wanapata kutoka kwa marafiki wao na nyingi kutoka kwenye vyombo vya habari. Uvutano mbaya kama huo huonekana waziwazi watoto wanapokuwa matineja. Hata hivyo, uchunguzi unaonyesha kwamba wanapokabiliwa na maamuzi makubwa maishani, vijana wengi huthamini zaidi maoni ya wazazi wao kuliko yale ya vijana wenzao.

Jambo unaloweza kufanya. Wazazi katika Israeli la kale walitiwa moyo kuzungumza na watoto wao mara nyingi ili wakazie viwango vinavyofaa akilini mwao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Fanya vivyo hivyo na mtoto wako. Kwa mfano ikiwa unaishi kupatana na viwango vya Biblia vya maadili, mwambie mtoto wako sababu inayokufanya uhisi kwamba kufuata viwango hivyo kunamsaidia mtu awe na maisha bora.

2 Msaidie mtoto wako aelewe matokeo.

Biblia inasema: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Wagalatia 6:7) Kanuni ya kwamba kila tendo lina matokeo inaweza kuonekana katika kila sehemu ya maisha. Fikiria kuhusu mambo uliyojionea ulipokuwa mtoto. Bila shaka ulijifunza masomo muhimu zaidi kutokana na mambo ambayo ulifanya na ukajionea matokeo ya matendo yako.

Jambo unaloweza kufanya. Ukitumia mifano halisi, mweleze mtoto wako jinsi wale waliochagua kufanya mambo yasiyofaa walivyoteseka au jinsi wale waliochagua kufanya mambo yanayofaa walivyofaidika. (Luka 17:31, 32; Waebrania 13:7) Pia, usimkinge mtoto wako dhidi ya madhara ya makosa yake. Kwa mfano, tuseme mwana wako anavunja kitu cha kuchezea cha mvulana mwingine. Unaweza kumwambia mwana wako ampe mvulana huyo moja kati ya vitu vyake mwenyewe vya kuchezea. Mwana wako hatasahau somo hilo kuhusu kuheshimu vitu vya wengine.

3 Msaidie mtoto wako awe na tabia nzuri.

Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Mtoto hujulikana kwa matendo yake, kama tabia yake ni njema na aminifu.” (Methali 20:11, Biblia Habari Njema) Kadiri watoto wanavyokua, wao huonyesha watakuwa watu wa aina gani. Kwa kusikitisha, baadhi yao hujulikana kwa sababu ya tabia mbaya. (Zaburi 58:3) Lakini wengine hutokeza sifa nzuri, zinazostahili kusifiwa. Kwa mfano, mtume Paulo aliliandikia kutaniko fulani hivi kuhusu kijana Timotheo: “Sina mtu mwingine yeyote aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mambo yenu.”​—Wafilipi 2:20.

Jambo unaloweza kufanya. Mbali na kukazia matokeo ya matendo yake, kama ilivyotajwa awali, msaidie mtoto wako afikirie angependa kujulikana kwa sifa gani. Wanapokabiliwa na hali fulani ngumu, vijana wanaweza kujifunza kufanya maamuzi yanayofaa kwa kujiuliza maswali yafuatayo:

  • Ninataka kuwa mtu wa aina gani?​—Wakolosai 3:10.

  • Mtu wa aina hiyo angefanya nini anapokabiliwa na hali hii?​—Methali 10:1.

Biblia ina mifano mingi halisi ya wanaume na wanawake ambao matendo yao yaliwatambulisha kuwa watu wazuri au wabaya. (1 Wakorintho 10:11; Yakobo 5:10, 11) Tumia mifano hiyo kumsaidia mwana au binti yako asitawishe sifa zinazofaa.

Machapisho ya Mashahidi wa Yehova yanaweza kukusaidia kuona jinsi unavyoweza kutumia kanuni za Biblia katika familia yako na jinsi ya kuwasaidia watoto wako kufanya hivyo pia.