Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kufikia Makubaliano

Jinsi ya Kufikia Makubaliano

KIKWAZO

Wewe na mwenzi wako wa ndoa mna maoni yanayotofautiana kuhusu jambo fulani. Kihalisi, kuna mambo matatu mnayoweza kufanya:

  1. Unaweza kusisitiza kishupavu hadi atende unavyotaka.

  2. Unaweza kumruhusu shingo upande atende anavyotaka.

  3. Mnaweza kufikia makubaliano.

Lakini huenda ukasema, ‘Mimi sipendezwi na wazo hili la kukubali-kubali maoni kwani inaonekana mwishowe sote tutakosa tunachokitaka!’

Uwe na hakika kwamba kufikia makubaliano kuhusu jambo fulani hakumaanishi kwamba mtabaki bila furaha. Lakini kabla ya kuchunguza jinsi mnavyoweza kufikia makubaliano, kuna mambo kadhaa unayopaswa kujua kuhusu ustadi huu wa kufikia makubaliano.

UNACHOPASWA KUJUA

Ili mkubaliane mnahitaji ushirikiano. Kabla ya kufunga ndoa, huenda ulizoea kujiamulia mambo. Lakini sasa mambo yamebadilika, hivyo wewe na mwenzi wako wa ndoa mnahitaji kutanguliza masilahi ya ndoa yenu badala ya kila mmoja kutanguliza mambo yake binafsi. Badala ya kuliona jambo hilo kuwa kikwazo, fikiria kuhusu faida za kufanya hivyo. Alexandra, mwanamke aliyeolewa anasema hivi: “Uamuzi wa watu wawili unaweza kuleta suluhisho bora zaidi la jambo kuliko uamuzi wa mtu mmoja.”

Ili mkubaliane hampaswi kushikilia mambo kishupavu. Mshauri wa ndoa anayeitwa John M. Gottman aliandika hivi: “Si lazima ukubali mambo yote ambayo mwenzi wako wa ndoa anasema au kuamini, lakini unapaswa kuwa na mtazamo mzuri ili uzingatie maoni yake. Ukijikuta katika hali ambapo mwenzi wako wa ndoa anaeleza maoni yake lakini wewe umekunja mikono kifuani huku ukitikisa kichwa kuonyesha kwamba jambo analosema haliwezekani, jua kwamba hamtafikia makubaliano.” *

Ili mkubaliane mnahitaji kuwa na usawaziko. Hakuna mtu ambaye angependa kuishi na mwenzi wa ndoa anayeamini kwamba “ni lazima maoni yake yafuatwe kwa sababu ndiyo bora zaidi.” Hali huwa nzuri kila mmoja anapokuwa tayari kukubali maoni ya mwenzake. June, mwanamke aliyeolewa anasema hivi: “Nyakati nyingine mimi huamua kumfurahisha mume wangu kwa kukubali maoni yake, na nyakati nyingine yeye pia hukubali maoni yangu. Hivyo ndivyo ndoa inavyopaswa kuwa, yaani, kutoa na kupokea na si kupokea tu.”

 UNACHOWEZA KUFANYA

Anza mazungumzo kwa njia nzuri. Mara nyingi jinsi mnavyoanza mazungumzo ndivyo mtakavyomaliza. Mkianza mazungumzo kwa maneno makali, kuna uwezekano mkubwa kwamba hamtafikia makubaliano. Kwa hiyo fuata shauri hili la Biblia: “Jivikeni . . . huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Sifa hizo zitakusaidia wewe na mwenzi wako mwepuke mabishano na badala yake mzingatie jinsi ya kusuluhisha tatizo mnalokabili.—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 4:6.

Zungumzieni mambo mnayokubaliana. Ikiwa jitihada zenu za kufikia makubaliano zinageuka na kuwa mabishano makali, huenda ikawa kwamba wewe na mwenzi wako mnakazia fikira kupita kiasi mambo ambayo mnatofautiana. Badala ya kufanya hivyo, kazieni fikira mambo mnayokubaliana. Ili mjue ni mambo gani mnayokubaliana, fanyeni hivi:

Kila mmoja wenu atengeneze orodha yenye safu mbili. Kwenye safu ya kwanza, andika mambo unayopendelea sana. Katika safu ya pili, orodhesha mambo unayohisi kwamba mnaweza kufikia makubaliano. Kisha zungumzieni mambo mliyoandika. Huenda mkatambua kwamba mnakubaliana katika mambo mengi kuliko mlivyowazia. Mkifanya hivyo itakuwa rahisi kufikia makubaliano. Hata ikiwa kuna mambo kadhaa msiyokubaliana, orodha hizo zitawasaidia muone pande zote za tatizo mnalokabili.

Tafuteni suluhisho pamoja. Huenda ikawa rahisi kusuluhisha matatizo fulani. Hata hivyo, mume na mke wanaweza kuimarisha uhusiano wao wanaposhughulikia matatizo mazito pamoja badala ya kila mmoja kujiamulia mambo kivyake.—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 4:9.

Uwe tayari kubadili maoni yako. Biblia inasema hivi: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Mume na mke wakipendana na kuheshimiana, itakuwa rahisi kwa kila mmoja wao kuzingatia maoni ya mwenzake na hata kuyakubali. Mume anayeitwa Cameron anasema hivi: “Kuna mambo fulani ambayo mtu hapendelei kufanya, lakini anaanza kuyapenda kwa sababu mwenzi wake anayapenda.”—Kanuni ya Biblia: Mwanzo 2:18.

^ fu. 12 Kutoka kwenye kitabu “Kanuni Saba za Kuifanikisha Ndoa” (cha Kiingereza).