Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tendo Moja la Fadhili za Kikristo

Tendo Moja la Fadhili za Kikristo

MIAKA 60 iliyopita katika mji mmoja mdogo huko Gujarat, India, baba ya John alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. John pamoja na ndugu na dada zake watano, na pia mama yao walikuwa Wakatoliki waliofuata sana dini, na hivyo walipinga imani ya baba yao.

Siku moja, baba ya John alimwomba John apeleke bahasha kwa ndugu mmoja wa kutaniko lake. Hata hivyo, asubuhi hiyo, John alikijeruhi kidole chake vibaya alipokuwa akifungua pipa kubwa la bati. Licha ya hilo, kwa kuwa alitaka kumtii baba yake, alikifunga kwa kitambaa kidole hicho kilichokuwa kikitoka damu na kwenda kwa miguu kupeleka bahasha aliyopewa.

John alipofika nyumbani kwa ndugu huyo, mke wake ambaye pia alikuwa Shahidi wa Yehova alipokea bahasha hiyo. Dada huyo aliona kidole cha John kilichokuwa kimejeruhiwa, naye akajitolea kumhudumia. Alileta kisanduku cha huduma ya kwanza, akasafisha kidole hicho kwa dawa na kukifunga. Kisha akamtayarishia John kikombe cha chai. Muda huo wote alikuwa akizungumza naye kwa njia ya kirafiki kuhusu Biblia.

Kwa sababu ya fadhili alizoonyeshwa na dada huyo, ubaguzi ambao John alikuwa nao kuelekea Mashahidi ulianza kupungua. Hivyo, John akamuuliza kuhusu mambo mawili ambayo baba yake aliamini lakini yaliyotofautiana na imani yake, yaani, ikiwa Yesu ni Mungu na ikiwa Wakristo wanapaswa kusali kwa Maria. Kwa kuwa Shahidi huyo alikuwa amejifunza Kigujarati, lugha ya asili ya John, alimjibu John kwa kutumia Biblia na akampa kijitabu “Habari Njema Hizi za Ufalme” katika Kigujarati.

Baadaye, John alipokuwa akisoma kijitabu hicho, alitambua kwamba alikuwa akisoma kweli za Biblia kwa mara ya kwanza. Alienda kwa kasisi wake na kumuuliza maswali yaleyale mawili. Kasisi huyo alikasirika na kumrushia John Biblia huku akipaza sauti: “Umekuwa Shetani! Nionyeshe ni wapi katika Biblia panaposema kwamba Yesu si Mungu. Nionyeshe ni wapi panaposema kwamba hatupaswi kumwabudu Maria. Nionyeshe!” John alishtushwa sana na kitendo cha kasisi huyo hivi kwamba akamwambia, “Sitakanyaga tena kamwe kanisa Katoliki.” Na hakurudi tena!

John alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi, akachukua msimamo upande wa ibada ya kweli, na kuanza kumtumikia Yehova. Baada ya muda, wengine katika familia yake walifanya vivyo hivyo pia. Leo, John bado ana kovu alilopata miaka 60 hivi iliyopita kwenye kidole cha shahada cha mkono wake wa kulia. Anakumbuka kwa furaha sana lile tendo moja la fadhili za Kikristo lililomvuta kwenye ibada safi.—2 Kor. 6:4, 6.