Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | BIBLIA INASEMA NINI KUHUSU UHAI NA KIFO?

Maoni ya Biblia Kuhusu Uhai na Kifo

Maoni ya Biblia Kuhusu Uhai na Kifo

Simulizi la uumbaji kwenye kitabu cha Mwanzo katika Biblia linasema kwamba Adamu, mwanadamu wa kwanza, aliambiwa hivi na Mungu: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:​16, 17) Maneno hayo yanaonyesha waziwazi kwamba iwapo Adamu angetii amri ya Mungu, hangekufa bali angeendelea kuishi katika bustani ya Edeni.

Kwa kusikitisha, badala ya kuchagua kutii ili aishi milele, Adamu aliamua kupuuza amri ya Mungu na kula tunda alilokatazwa baada ya kupewa tunda hilo na Hawa, mke wake. (Mwanzo 3:​1-6) Madhara ya kutotii amri hiyo yanatuathiri sisi pia. Mtume Paulo alielezea hali hiyo hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:​12) Bila shaka, “mtu [huyo] mmoja” ni Adamu. Hata hivyo, alifanya dhambi gani, na kwa nini ilileta kifo?

Jambo ambalo Adamu alifanya, yaani, kukataa kimakusudi kumtii Mungu au kuvunja sheria yake, ni dhambi. (1 Yohana 3:4) Na kama ambavyo Mungu alikuwa amemwambia Adamu, adhabu ya dhambi ni kifo. Ikiwa Adamu na wazao ambao angepata baadaye wangeendelea kutii amri ya Mungu, hawangekuwa na dhambi na kwa hiyo hawangepatwa na kifo. Mungu hakuwaumba wanadamu wafe, bali waishi milele.

Kama Biblia ilivyosema, hakuna shaka kwamba kifo “[kimeenea] kwa watu wote.” Lakini je, kuna sehemu fulani ya mwanadamu inayoendelea kuishi baada ya mtu kufa? Huenda wengi wakajibu ndiyo, kwamba sehemu fulani inayoitwa nafsi, haifi. Lakini hilo lingemaanisha kwamba Mungu alimdanganya Adamu. Jinsi gani? Ikiwa sehemu fulani ya mwanadamu huendelea kuishi mahali pengine baada ya kifo, basi haingekuwa kweli kwamba kifo ni adhabu ya dhambi, kama Mungu alivyomwambia Adamu. Biblia inasema: “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Waebrania 6:​18) Ukweli ni kwamba Shetani ndiye aliyesema uwongo alipomwambia Hawa hivi: “Hakika hamtakufa.”​—Mwanzo 3:4.

Hivyo basi swali ni; Ikiwa fundisho la kutokufa kwa nafsi ni la uwongo, ni nini hutendeka mtu anapokufa?

BIBLIA INAFUNUA UKWELI WA MAMBO

Simulizi la uumbaji katika kitabu cha Mwanzo linasema hivi: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” Usemi “nafsi hai” unatokana na neno la Kiebrania ne’phesh, * linalomaanisha kiumbe anayepumua.​—Mwanzo 2:​7.

Hivyo, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba mwanadamu hakuumbwa akiwa na nafsi isiyoweza kufa. Badala yake, kila mwanadamu ni “nafsi hai.” Hiyo ndiyo sababu hakuna andiko katika Biblia linalotaja kuhusu “nafsi isiyoweza kufa.”

Ikiwa Biblia haisemi kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa kama wengine wanavyodai, kwa nini dini nyingi hufundisha jambo tofauti? Misri ya kale inatoa jibu la swali hilo.

FUNDISHO LA KIPAGANI LASITAWI

Herodoto, mwanahistoria Mgiriki wa karne ya tano K.W.K., alisema Wamisri walikuwa “kikundi cha kwanza cha watu kilichotetea fundisho la kutokufa kwa nafsi.” Wababiloni pia ni taifa lingine la kale lililoamini fundisho hilo. Kufikia mwaka wa 332 W.K., Aleksanda Mkuu aliposhinda Mashariki ya Kati, wanafalsafa Wagiriki walikuwa wameeneza fundisho hilo, na muda mfupi baadaye, lilienea katika Milki yote ya Ugiriki.

Hakuna andiko katika Biblia linalotaja kuhusu “nafsi isiyoweza kufa”

Katika karne ya kwanza W.K., madhehebu mawili maarufu ya Kiyahudi, ambayo ni Waesene na Mafarisayo, yalifundisha kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Kitabu The Jewish Encyclopedia kinasema: “Fundisho la kutokufa kwa nafsi liliwafikia Wayahudi baada ya kuanza kupokea mawazo ya Wagiriki hasa kupitia falsafa ya Plato.” Vivyo hivyo, Josephus, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza alisema fundisho hilo halitokani na Maandiko Matakatifu, bali linatokana na “imani ya wana wa Ugiriki,” aliyoiona kuwa mkusanyo wa hekaya zao.

Kadiri tamaduni za Wagiriki zilivyoenea, watu waliodai kuwa Wakristo walianza pia kukubali fundisho hilo la kipagani. Kulingana na mwanahistoria Jona Lendering, “ilikuwa rahisi kuunganisha falsafa ya Plato na Ukristo kwa sababu ya nadharia ya Plato kwamba mwanzoni nafsi zetu zilikuwa mahali pazuri na sasa zinaishi ulimwengu uliopotoka.” Hivyo, fundisho la kipagani kuhusu kutokufa kwa nafsi likapenya katika kanisa la “Kikristo” na kuwa sehemu kuu ya imani yake.

“KWELI ITAWAWEKA NINYI HURU”

Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alitoa onyo hili: “Neno lililoongozwa na roho linasema kwa hakika kwamba katika vipindi vya nyakati za mwisho wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha na mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:⁠1) Bila shaka, maneno hayo yalithibitika kuwa ya kweli! Fundisho la kutokufa kwa nafsi ni moja kati ya “mafundisho ya roho waovu.” Biblia haiungi mkono fundisho hilo, na chanzo chake ni falsafa na dini za kale za kipagani.

Kwa kupendeza, Yesu alisema hivi kutuhusu: “Nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:​32) Tunapopata ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia, tunawekwa huru kutokana na mafundisho yasiyomheshimu Mungu na mazoea yanayoungwa mkono na dini nyingi za ulimwengu huu. Kwa kuongozea, kweli iliyo katika Neno la Mungu inatuweka huru kutokana na utumwa wa tamaduni na ushirikina unaohusianishwa na kifo.​—Ona sanduku “ Wafu Wako Wapi?

Muumba wetu hakukusudia wanadamu waishi duniani kwa miaka 70 au 80 na kisha waende kuishi milele mahali pengine. Kusudi kuu la Mungu ni kwamba wanadamu waishi milele hapa duniani wakiwa watoto wake watiifu. Kusudi hilo linaonyesha jinsi ambavyo Mungu anawapenda wanadamu na hakika litatimia. (Malaki 3:6) Mtunga zaburi aliongozwa kutangaza maneno haya yenye kutia moyo: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​—Zaburi 37:29.

 

^ fu. 9 Tafsiri nyingine za Biblia kama vile Biblia Habari Njema hutafsiri neno hilo kuwa “kiumbe hai,” Verbum Bible hutafsiri neno hilo kuwa “kiumbe chenye uzima,” na Union version hutafsiri neno hilo kuwa “nafsi hai.