Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anaweza Kujuta?

Je, Mungu Anaweza Kujuta?

Mkaribie Mungu

Je, Mungu Anaweza Kujuta?

WAAMUZI 2:11-18

KWA kuwa hatujakamilika, nyakati nyingine tunajuta. Kwa mfano, huenda tukahisi vibaya tunapogundua kwamba tumekosea. Kwa kushangaza, Biblia inasema kwamba Yehova anaweza kujuta. Huenda ukasema, ‘Lakini Mungu ni mkamilifu, hakosei!’ Hata hivyo, Mungu anajuta kwa njia gani? Jibu linaweza kutusaidia kuelewa jambo fulani linaloshangaza sana: Yehova ana hisia, na matendo yetu yanaweza kuathiri hisia zake. Fikiria maneno yaliyorekodiwa kwenye Waamuzi 2:11-18.

Kitabu cha Biblia cha Waamuzi kinazungumzia kipindi chenye msukosuko katika historia ya taifa la Israeli. Taifa hilo lilikuwa limeingia Kanaani, nchi ambayo Mungu alikuwa amemwahidi Abrahamu. Kwa karne ambazo zingefuata, njia ya maisha ya Waisraeli ingefafanuliwa kwa maneno haya manne: uasi, uonevu, dua, na ukombozi. *

Uasi. Wakishawishiwa na Wakanaani, Waisraeli ‘walimwacha Yehova’ na kuanza kufuata miungu mingine; hasa ‘walianza kutumikia Baali na sanamu za Ashtorethi.’ * Uasi huo ukaongezeka na kuwa uasi-imani. Si ajabu kwamba Waisraeli ‘walimtia uchungu Yehova,’ Mungu aliyewakomboa kutoka katika nchi ya Misri!—Mstari wa 11-13; Waamuzi 2:1.

Uonevu. Pindi kwa pindi hasira ya uadilifu ilimchochea Yehova kutowalinda watu wake waliomwasi. Hivyo, Waisraeli walianguka “mkononi mwa adui zao” ambao walikuja na kupora nchi yao.—Mstari wa 14.

Dua. Waisraeli walipopatwa na mateso makali, walijuta kwa sababu ya mwenendo wao mbaya na wakamlilia Mungu awasaidie. Maneno “kuugua kwao kwa sababu ya wakandamizaji wao” yanaonyesha kwamba walitoa dua. (Mstari wa 18) Walitoa dua kwa Mungu tena na tena. (Waamuzi 3:9, 15; 4:3; 6:6, 7; 10:10) Mungu alifanya nini?

Ukombozi. Mungu alisikiliza kilio cha Waisraeli na ‘kujuta.’ Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘kujuta’ linaweza kumaanisha “kubadili mawazo au nia.” Kitabu kimoja cha marejeo kinasema: “Yehova alipoona wakiugua alibadili nia yake ya kuwaadhibu na badala yake akawakomboa.” Kwa rehema zake, Yehova ‘aliwasimamishia waamuzi,’ ambao waliwakomboa watu wake kutokana na adui zao.—Mstari wa 18.

Je, uliona kilichomfanya Mungu ajute, au kubadili nia yake? Ni kwa sababu watu wake walibadili mtazamo wao. Fikiria jambo hilo kwa njia hii: Baba mwenye upendo anaweza kumwadhibu mtoto wake aliyekosea, labda kwa kumnyima mambo fulani. Lakini anapogundua kwamba kwa kweli mtoto huyo amesikitika sana, baba anaweza kuamua kuondoa adhabu hiyo.

Mfano huo unatufunza nini kumhusu Yehova? Tukifanya dhambi kwa makusudi hasira yake inawaka, lakini tukitubu kutoka moyoni anatusamehe. Inagusa moyo sana kufikiria kwamba yale tunayofanya yanaweza kumhuzunisha au kumkasirisha Mungu. Kwa nini usijifunze jinsi unavyoweza kuufanya ‘moyo wa Yehova ushangilie’? (Methali 27:11) Hutajuta kamwe.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Andiko la Waamuzi 2:11-18 linaeleza kwa ufupi jinsi Waisraeli walivyojiendesha, na sura zinazofuata zinaeleza jambo hilo kwa undani.

^ fu. 6 Baali alikuwa mungu mkuu wa Wakanaani, na Ashtorethi alikuwa mungu wa kike ambaye alionwa kuwa mke wa Baali.