Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni?

Je, Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni?

Je, Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni?

JIONI iliyotangulia kuuawa kwa Yesu na baada ya mlo wa mwisho pamoja na mitume wake, Yesu aliwaahidi kwamba angewapatia thawabu ya kwenda mbinguni. Alisema hivi: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. Kama sivyo, ningaliwaambia ninyi, kwa sababu ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali.” (Yohana 14:2) Kwa nini Yesu angewatayarishia mahali mbinguni? Watafanya nini huko?

Yesu alijua kwamba wanafunzi wake wangekuwa na kazi ya pekee. Jioni hiyohiyo, alisema hivi: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:28, 29) Mungu alikuwa amemwahidi Yesu kwamba angekuwa Mfalme ambaye angetosheleza moja kati ya mahitaji ya maana sana ya wanadamu, yaani, uhitaji wa serikali nzuri. Yesu atawakomboa watu kutoka katika mateso na atawaponda wale wanaowaonea. Ingawa Yesu atakuwa na raia “mpaka miisho ya dunia,” kiti chake cha ufalme kitakuwa mbinguni.—Zaburi 72:4, 8; Danieli 7:13, 14.

Hata hivyo, Yesu hatatawala akiwa peke yake. Ndiyo sababu aliwaahidi mitume wake makao mbinguni. Walikuwa wa kwanza kuchaguliwa ili ‘watawale wakiwa wafalme juu ya dunia.’—Ufunuo 5:10.

Ni watu wangapi wanaoenda mbinguni? Sawa na serikali nyingine, watawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu ni wachache wakilinganishwa na watu wote ambao wataishi chini ya mamlaka ya Ufalme huo. Yesu aliwaambia hivi wale ambao watatawala pamoja naye: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” (Luka 12:32) Mwishowe, hilo “kundi dogo” litakuwa na hesabu ya watu 144,000. (Ufunuo 14:1) Hesabu hiyo ni ndogo ikilinganishwa na mamilioni ya watu ambao watapata uzima wa milele duniani wakiwa raia washikamanifu wa Ufalme huo.—Ufunuo 21:4.

Kwa hiyo, si watu wote wazuri wanaoenda mbinguni. Mtume Petro alisema hivi waziwazi kuhusu Mfalme Daudi aliyekuwa mtu mzuri: “Daudi hakupanda mbinguni.” (Matendo 2:34) Yohana Mbatizaji alikuwa mtu mzuri. Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba hangekuwa na pendeleo la kutawala akiwa mfalme mbinguni. Yesu alisema: “Kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mkuu kuliko Yohana Mbatizaji; lakini mtu aliye mdogo zaidi katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.”—Mathayo 11:11.

Je, Utapata Thawabu Ambayo Watu Wazuri Watapata?

Mtu anapaswa kufanya nini ili apate thawabu ya kuishi milele duniani? Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Ona kwamba Mungu anachochewa na upendo kuwapa watu wote ulimwenguni nafasi ya kuishi milele, lakini ni wale tu ‘wanaoamini’ ndio hasa wanaopata thawabu hiyo.

Imani inapaswa kutegemea ujuzi sahihi. (Yohana 17:3) Unaweza kuonyesha kwamba wewe ni mtu mzuri kwa kujifunza mengi zaidi kuhusu kusudi la Yehova kwa mwanadamu. Tenda kwa imani kulingana na yale unayojifunza. Na uwe na hakika kwamba unaweza kupata uzima wa milele.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Biblia Inasema Nini?

Swali:

Ni nini kinachowapata watu wazuri wanapokufa?

Jibu:

“Wafu, hawajui lolote kamwe.”MHUBIRI 9:5.

Swali:

Watu wazuri wana tumaini gani la wakati ujao?

Jibu:

“Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Yesu] na kutoka.”YOHANA 5:28, 29.

Swali:

Watu wengi walio wazuri wataishi wapi?

Jibu:

“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”ZABURI 37:29.