Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya Furaha ya Familia

Utafanya Nini Kijana Wako Akitilia Shaka Imani Yako?

Utafanya Nini Kijana Wako Akitilia Shaka Imani Yako?

Wanapoendelea kukomaa, vijana wengi huamua kufuata dini ya wazazi wao. (2 Timotheo 3:14) Lakini wengine hawafanyi hivyo. Utafanya nini mtoto wako anayeendelea kukua anapoanza kutilia shaka imani yako? Makala hii itazungumzia jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyokabiliana na hali hiyo.

“Sitaki kufuata dini ya wazazi wangu tena. Nataka kuiacha.”​—Cora, 18. *

UNASADIKI kwamba dini yako inafundisha ukweli kumhusu Mungu. Unaamini kwamba Biblia inafundisha njia bora zaidi ya maisha. Hivyo basi, ni jambo la kawaida kwako kujitahidi kumfundisha mtoto wako viwango vya Biblia. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Lakini namna gani ikiwa mtoto wako anapoendelea kukua anaacha kupendezwa na mambo ya kiroho? Namna gani akianza kutilia shaka imani ambayo alionekana kupendezwa nayo alipokuwa mtoto?—Wagalatia 5:7.

Ikiwa jambo kama hilo linatokea, usiamue kwamba umeshindwa na wajibu wako ukiwa mzazi Mkristo. Mambo mengine yanaweza kuhusika, kama tutakavyoona. Hata hivyo, kumbuka jambo hili: Njia utakayotumia kushughulikia shaka za kijana wako inaweza kufanya avutiwe zaidi au ajitenge zaidi na imani yako. Ikiwa utamlazimisha kijana wako afuate imani yako, utakuwa umeanzisha mapambano makali ambayo ni vigumu kushinda.—Wakolosai 3:21.

Ni vema zaidi kufuata himizo la mtume Paulo. Aliandika hivi: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, mwenye sifa za kustahili kufundisha, akiendelea kujizuia chini ya uovu.” (2 Timotheo 2:24) Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba ‘unastahili kufundisha’ ikiwa kijana wako anatilia shaka imani yako?

Uwe Mwenye Utambuzi

Kwanza, jitahidi kutambua mambo ambayo huenda yanamchochea kijana wako awe na maoni hayo. Kwa mfano:

  • Je, anahisi akiwa mpweke na bila marafiki katika kutaniko la Kikristo? “Kwa sababu nilitaka kuwa na marafiki, nilianzisha urafiki na wanafunzi fulani shuleni, na hilo liliathiri maendeleo yangu ya kiroho kwa muda mrefu. Niliacha kupendezwa na mambo ya kiroho hasa kwa sababu ya marafiki hao wabaya, na sasa ninajuta sana.”​—Lenore, 19.

  • Je, anakosa kujiamini, na hivyo kufanya iwe vigumu kuzungumza kuhusu imani yake? “Nilipokuwa shuleni, nilisita kuzungumza pamoja na wanafunzi wenzangu kuhusu imani yangu. Niliogopa kwamba wangeniona kuwa mtu asiye wa kawaida au kuniita ‘mvulana wa Biblia.’ Watoto waliojiendesha kwa njia tofauti na wengine walikosa marafiki, na sikutaka hilo linipate.”​—Ramón, 23.

  • Je, anahisi kwamba amelemewa na jukumu la kuishi kupatana na viwango vya Kikristo? “Ninahisi kana kwamba ahadi ya Biblia ya uzima wa milele iko juu ya ghorofa ndefu, na hata sijaanza kupanda ngazi za ghorofa hiyo; niko mbali, mbali sana na ngazi hizo. Woga wa kupanda ngazi hizo umekuwa mwingi sana hivi kwamba nimefikiria kuacha imani yangu.”​—Renee, 16.

Zungumzieni Jambo Hilo

Ni mambo gani yasiyoonekana ambayo huenda kijana wako anakabili? Njia bora ya kujua ni kumuuliza! Hata hivyo, uwe mwangalifu ili mazungumzo yasigeuke na kuwa mabishano. Badala yake, fuata himizo la Yakobo 1:19: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ Uwe mwenye subira unaposhughulika naye. Tumia “ustahimilivu wote na ufundi wa kufundisha,” kama vile tu ambavyo ungeshughulika na mtu ambaye si wa familia yako.—2 Timotheo 4:2.

Kwa mfano, ikiwa kijana wako hataki kuhudhuria mikutano ya Kikristo, jaribu kutambua ikiwa kuna jambo lingine linalomsumbua. Lakini fanya hivyo kwa subira. Mzazi hawezi kufanikiwa akitenda kwa njia ifuatayo.

Mwana: Sitaki kwenda kwenye mikutano tena.

Baba: [kwa ukali] Unamaanisha nini unaposema hutaki kwenda?

Mwana: Nahisi tu kwamba mikutano inachosha!

Baba: Unahisi hivyo kumhusu Mungu? Mungu anakuchosha? Hilo ni jambo baya sana! Mradi unaishi katika nyumba yetu, utahudhuria mikutano pamoja nasi, upende usipende!

Mungu anataka wazazi wawafundishe watoto wao kumhusu na pia anataka watoto wawatii wazazi wao. (Waefeso 6:1) Hata hivyo, hungetaka mtoto wako ajiunge nawe katika utendaji wako wa kiroho kama desturi tu na kuandamana nawe kwenye mikutano ya Kikristo shingo upande. Ikiwezekana, ungependa afanye hivyo kwa sababu anatambua umuhimu wa mikutano na anampenda Yehova.

Utafanikiwa zaidi ikiwa utatambua mambo yasiyoonekana ambayo huenda yanafanya mtoto wako awe na mtazamo huo. Ukiwa na hayo akilini, ona jinsi ambavyo yale mazungumzo kati ya baba na mwana yangefanywa kwa njia yenye matokeo mazuri zaidi.

Mwana: Sitaki kwenda kwenye mikutano tena.

Baba: [kwa utulivu] Kwa nini unahisi hivyo?

Mwana: Nahisi tu kwamba mikutano inachosha!

Baba: Linaweza kuwa jambo lenye kuchosha kuketi kwa muda wa saa moja au mbili. Ni nini hasa kinachofanya uhisi umechoka sana?

Mwana: Sijui. Ninafikiri ingekuwa afadhali kama ningekuwa mahali pengine.

Baba: Hivyo ndivyo marafiki wako wanavyohisi?

Mwana: Hilo hasa ndilo tatizo langu! Sina rafiki yeyote wakati huu. Tangu rafiki yangu wa karibu ahame, ninahisi kana kwamba sina mtu wa kuzungumza naye! Kila mtu anafurahia maisha. Ninahisi ni kama nimetengwa na wengine!

Kwa kumchochea kijana wake ajieleze, baba huyu anatambua jambo lisiloonekana wazi, ambalo katika kisa hiki ni upweke. Pia, anamfanya kijana wake amwamini na hivyo kufanya kijana huyo ajihisi huru kuzungumza naye wakati ujao.​—Ona sanduku kwenye ukurasa huu lenye kichwa  “Uwe Mwenye Subira!”

Baada ya muda, vijana wengi wanatambua kwamba wanaposhinda tatizo ambalo huenda lingewazuia kufanya maendeleo ya kiroho, kwa kawaida wao huhisi vizuri zaidi kujihusu na kuhusu imani yao. Mfikirie Ramón, kijana aliyetajwa mapema ambaye aliogopa kujitambulisha shuleni kuwa Mkristo. Mwishowe, Ramón aliona kwamba kuzungumza kuhusu imani yake halikuwa jambo gumu kama alivyowazia, hata alipodhihakiwa. Anasema:

“Pindi moja, mvulana fulani shuleni alikuwa akinifanyia mzaha kwa sababu ya dini yangu. Nilijawa na wasiwasi na kutambua kwamba wanafunzi wote darasani walikuwa wakisikiliza. Kisha nikaamua kubadili mazungumzo na kumuuliza kuhusu imani yake. Nilishangaa kuona kwamba alikuwa na wasiwasi mwingi zaidi kuliko mimi! Kisha, nikatambua kuwa vijana wengi wanaamini mafundisho fulani ya kidini, lakini hawayaelewi. Angalau mimi ninaweza kueleza mambo ninayoamini. Kwa kweli, inapohusu kuzungumzia imani, wanafunzi wenzangu ndio wanaopaswa kuwa na wasiwasi, sio mimi!”

JARIBU KUFANYA HIVI: Mchochee kijana wako ajieleze kwa kumuuliza jinsi anavyohisi kuhusu kuwa Mkristo. Kwa maoni yake, kuna faida gani? Kuna matatizo gani? Je, faida ni nyingi kuliko matatizo? Ikiwa ndivyo, jinsi gani? (Marko 10:29, 30) Kijana wako anaweza kuandika mawazo yake kwenye karatasi akitumia safu mbili. Anaweza kuandika matatizo kwenye safu ya kushoto na faida kwenye safu ya kulia. Kuchunguza mambo aliyoandika kunaweza kumsaidia kijana wako atambue tatizo lake na kujaribu kulitatua.

“Nguvu za Kufikiri” za Kijana Wako

Wazazi na wataalamu wameona kwamba kuna tofauti kubwa kati ya jinsi watoto wadogo wanavyofikiri na jinsi vijana wanaobalehe wanavyofikiri. (1 Wakorintho 13:11) Kwa kawaida, watoto wadogo hawachanganui mambo wanayofundishwa. Lakini vijana wanaobalehe wanataka kuelewa mambo kwa undani zaidi. Kwa mfano, mtoto mdogo anaweza kufundishwa kwamba Mungu aliumba vitu vyote. (Mwanzo 1:1) Hata hivyo, kijana anayebalehe anaweza kujiuliza maswali kama vile: ‘Ninajua jinsi gani kwamba kuna Mungu? Mbona Mungu mwenye upendo aruhusu uovu uwepo? Kwa nini niamini kwamba Mungu amekuwepo sikuzote?’​—Zaburi 90:2.

Huenda ukahisi maswali kama hayo yanaonyesha kwamba imani ya kijana wako imeanza kufifia. Ukweli ni kwamba hiyo inaweza kuwa ishara ya maendeleo. Kwa kweli, kuuliza maswali ni sehemu muhimu ya ukuzi wa kiroho wa Mkristo.​—Matendo 17:2, 3.

Zaidi ya hayo, kijana wako anajifunza kutumia ‘nguvu zake za kufikiri.’ (Waroma 12:1, 2) Kwa hiyo, ataelewa “upana na urefu na kimo na kina” cha imani ya Kikristo kwa njia ambayo hangeweza kuelewa alipokuwa mtoto. (Waefeso 3:18) Huu hasa ndio wakati wa kumsaidia kijana wako aelewe sababu ya kuamini mambo anayofundishwa ili asitawishe usadikisho wenye nguvu kuhusu imani yake.​—Methali 14:15; Matendo 17:11.

JARIBU KUFANYA HIVI: Zungumzia mambo ya msingi pamoja na kijana wako, na kuchunguza tena habari ambazo huenda wewe na yeye mliziona kuwa za kawaida tu. Kwa mfano, mchochee afikirie maswali kama haya: ‘Ni nini kinachonisadikisha kwamba kuna Mungu? Ni mambo gani ninayoona ambayo yananithibitishia kwamba Mungu ananijali? Kwa nini ninaamini kwamba nitafaidika kwa kutii sheria za Mungu?’ Uwe mwangalifu ili usimlazimishe kijana wako akubali maoni yako. Badala yake, msaidie asitawishe usadikisho wake mwenyewe. Kwa njia hiyo itakuwa rahisi zaidi kwake kuwa na uhakika kuhusu imani yake.

‘Alishawishiwa Kuamini’

Biblia inamtaja kijana Timotheo aliyejua maandiko matakatifu “tangu utoto mchanga.” Hata hivyo, mtume Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.” (2 Timotheo 3:14, 15) Kama Timotheo, huenda umemfundisha kijana wako viwango vya Biblia tangu utotoni. Hata hivyo, sasa unahitaji kumshawishi ili asitawishe usadikisho wake mwenyewe.

Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1, kinasema: “Maadamu kijana wako anaishi na wewe, una haki ya kutazamia afuate ratiba yako ya kiroho. Hata hivyo, lengo lako ni kumsaidia kijana wako ampende Mungu kutoka moyoni, wala si kijuujuu tu.” Ukiwa na lengo hilo akilini, unaweza kumsaidia kijana wako awe “imara katika imani” ili hiyo iwe njia yake ya maisha, bali si yako. *​—1 Petro 5:9.

^ fu. 4 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 40 Kwa habari zaidi, soma gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2009, ukurasa wa 10-12, na kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1, ukurasa wa 315-318.

JIULIZE . . .

  • Ninatenda jinsi gani mtoto wangu anapotilia shaka imani yangu?

  • Ninaweza kutumia jinsi gani habari iliyo katika makala hii ili kuboresha jinsi ninavyotenda?