Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hukataa kwa Heshima Kujihusisha Katika Sherehe za Kizalendo?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hukataa kwa Heshima Kujihusisha Katika Sherehe za Kizalendo?

 Mashahidi wa Yehova wanaheshimu serikali na nembo za taifa. Tunakubali kwamba wengine wana uhuru wa kuchagua ikiwa watasema kiapo cha uaminifu, watasalimu bendera, au kuimba wimbo wa taifa.

 Hata hivyo, tukiwa Mashahidi wa Yehova tumeamua kwamba hatutashiriki katika mambo hayo kwa sababu tunaamini kwamba hayapatani na mafundisho ya Biblia. Tunathamini sana wengine wanapoheshimu imani yetu kama tu sisi tunavyoheshimu wengine walio na imani tofauti na yetu.

Katika makala hii

 Ni kanuni gani za Biblia zinazohusika?

 Kimsingi uamuzi wetu unategemea kanuni hizi mbili za Biblia:

  •   Ni Mungu peke yake anayestahili ibada yetu. Biblia inasema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Kwa kawaida, viapo vya uaminifu na nyimbo za taifa zinatia ndani ahadi kwamba mtu atajitoa kabisa kwa taifa lake au kulipenda zaidi ya kitu kingine chochote. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova wanahisi kwamba ni kosa kwao kushiriki katika sherehe kama hizo.

     Vilevile, Mashahidi wa Yehova wanahisi kwamba kusalimu bendera ni tendo la ibada, au ibada ya sanamu, ambayo inapingwa na Biblia. (1 Wakorintho 10:14) Baadhi ya wanahistoria wanakiri kwamba bendera za taifa ni alama za kidini. Mwanahistoria Carlton J. H. Hayes * aliandika hivi: “Ishara kuu ya uzalendo ambayo huabudiwa na wengi ni bendera.” Mwandishi Daniel P. Mannix alisema hivi kuwahusu Wakristo wa mapema: “Wakristo walikataa . . . kutoa dhabihu kwa maliki Mroma, jambo ambalo sasa ni sawa na kukataa kuisalimu bendera.” *

    Ingawa Mashahidi wa Yehova hawasalimu bendera, kwa upande mwingine, hawawezi kuiharibu, kuichoma moto, au kuikosea heshima, bendera au nembo nyingine ya taifa.

  •   Wanadamu wote ni sawa machoni pa Mungu. (Matendo 10:34, 35) Biblia inasema kwamba Mungu “alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja.” (Matendo 17:26) Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba ni kosa kutukuza jamii yoyote au kuliona taifa lolote kuwa bora kuliko lingine. Tunaheshimu watu wote, iwe wanatoka wapi au wanaishi wapi.​—1 Petro 2:17.

 Vipi ikiwa sheria inatulazimu kushiriki?

 Mashahidi wa Yehova hawapingi serikali. Tunaamini kwamba serikali ni sehemu ya “mpango wa Mungu” na ameruhusu mpango huo uwepo. (Waroma 13:1-7) Pia, tunaamini kwamba Wakristo wanapaswa kuzitii serikali.​—Luka 20:25.

 Vipi ikiwa, sheria za serikali zinapingana na sheria za Mungu? Katika visa fulani, inawezekana kutuma ombi la kisheria kwa serikali na kuiomba kurekebisha sheria fulani. * Lakini mabadiliko yasipofanywa, kwa heshima, Mashahidi wa Yehova wanachagua “kumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”​—Matendo 5:29.

 Je, Mashahidi wa Yehova wanaunga mkono masuala ya kijamii na kisiasa?

 Hapana. Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono upande wowote inapohusu masuala ya kijamii au ya kisiasa. Tunapokataa kusema kiapo cha uaminifu, kusalimu bendera, au kuimba wimbo wa taifa, hatufanyi hivyo eti kwa sababu tunaegemea upande fulani wa kisiasa. Badala yake, inapohusu sherehe hizo za kizalendo, tunafanya maamuzi hayo kwa sababu tunashikamana na imani yetu inayotegemea Biblia.

^ Kitabu Essays on Nationalism, ukurasa wa 107-108.

^ Kitabu The Way of the Gladiator, ukurasa wa 212.